Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Korea,
Mhe. Lee Nak-yon atafanya ziara ya kikazi nchini kwa mwaliko wa mwenyeji
wake, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim
Majaliwa Majaliwa (Mb.), kuanzia tarehe 21 hadi 23 Julai 2018. Ziara
hiyo itakuwa ya
kwanza kufanywa na kiongozi wa ngazi ya juu kutoka
Jamhuri ya Korea tangu nchi zetu mbili zianzishe mahusiano ya
kidiplomasia mwaka 1992.
Madhumuni ya ziara hiyo ni
kuimarisha ushirikiano na uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo
mbili na kufungua zaidi fursa za ushirikiano wa kibiashara na kiuchumi
katika ngazi na sekta mbalimbali. Mhe. Waziri Mkuu Lee atafuatana na
ujumbe mzito wa maafisa wa Serikali, wabunge na wafanyabiashara wakubwa.
Ujumbe wa wafanyabiashara utakaoongozana na Mhe. Lee unatarajiwa
kukutana na wenzao wa Tanzania katika Mkutano wa Pili wa Jukwaa la
Wafanyabiashara uliopangwa kufanyika jijini Dar es Salaam tarehe 23
Julai 2018. Mkutano wa kwanza ambao ulikuwa na mafanikio makubwa
ulifanyika Seoul mwezi Februari 2018.
Mhe. Lee Nak-yon atawasili nchini
saa kumi na mbili na nusu jioni (12:30) ya tarehe 21 Julai 2018 na
atapokelewa na mwenyeji wake Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Siku inayofuata, Waziri Mkuu
Lee na mwenyeji wake Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), watafanya
mazungumzo rasmi jijini Dar es Salaam na baadaye watashuhudia uwekaji
saini wa mkataba wa kuondoa hitaji la visa kwa wenye hati za kusafiria
za kidiplomasia na za utumishi (diplomatic and official/service
passport). Aidha, Mhe. Lee atakutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa ajili ya kusalimiana.
Jamhuri ya Korea ni mshirika
mkubwa wa maendeleo wa Tanzania ambapo kupitia Shirika la Kimataifa la
Maendeleo (KOICA) na Mfuko wa Ushirikiano wa Uchumi na Maendeleo (EDCF)
yamekuwa yakitoa misaada na mikopo mingi ya masharti nafuu kwa Tanzania
ikiwemo misaada ya fedha katika bajeti, ujenzi wa miundombinu ya jamii,
mafunzo ya muda mfupi na mrefu, wataalamu mbalimbali wa kujitolea, vifaa
na mashine kwa ajili ya sekta mbalimbali ikiwemo ya afya.
Baadhi ya miradi ambayo
imegharamiwa na Serikali ya Korea ni pamoja na Mradi wa kuboresha Huduma
ya Mama na Mtoto katika Hospitali ya Chanika, Mradi wa Mfumo wa Usajili
wa Meli na Mabaharia kwa Njia ya Mtandao Zanzibar, Mradi wa Ujenzi wa
Hospitali ya Taifa ya Taaluma na Tiba (MUHAS) kampasi ya Mloganzila na
ujenzi wa daraja katika mto Malagarasi.
Vile vile, Korea ni mshirika
mkubwa katika kusaidia maendeleo ya Bara la Afrika ambapo hivi karibuni
katika mkutano wa Sita wa Jukwaa la Ushirikiano wa Kiuchumi kati ya
Korea na Africa (KOAFEC VI) uliofanyika mwezi Mei 2018, Busan, Korea
ambapo Serikali ya Korea ilitangaza msaada wa Dola za Marekani bilioni 5
kwa ajili ya Bara la Afrika kwa kipindi cha mwaka 2018/2020. Tanzania
ni miongoni mwa nchi zitakazonufaika na msaada huo.
No comments :
Post a Comment