Mjumbe
wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu Mhandisi Ramo Makani akiuliza swali kwa
mwakilishi wa kampuni ya simu ya Vodacom (hayupo pichani) waliojenga mnara
kwenye eneo la kiwanda cha sukari cha Mkulazi kilichopo Morogoro wakati wa
ziara ya Kamati hiyo ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano. Wa kwanza
kushoto ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Moshi Selemani Kakoso na wa pili
kushoto ni Naibu Waziri wa Uchukuzi wa Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye.
NA
WUUM, MOROGORO
KAMATI
ya Bunge ya Miundombinu imeanza ziara ya kukagua upatikanaji wa huduma za
mawasiliano kwa wote kwenye maeneo mbali mbali nchini ambapo wamekagua uwepo wa
mawasiliano hayo kwenye eneo la kijiji cha Mkulazi kilichopo tarafa ya
Ngerengere mkoa wa Morogoro ambapo Serikali imedhamiria kuwekeza na kujenga
kiwanda cha sukari.
Mwenyekiti
wa Kamati hiyo Mhe. Moshi Selemani Kakoso akiongoza wajumbe wa Kamati yake,
wamefika kwenye eneo hilo la uwekezaji na kudhibitisha uwepo wa mawasiliano.
Kakoso ameushukuru Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kwa kutekeleza azma ya
Serikali ya kupeleka mawasiliano ambapo hamna mawasiliano na imewezesha nia ya
Serikali ya kuwekeza kwenye viwanda.
Kakoso
amewataka wananchi waitumie nafasi hii vizuri, minara inahitaji ulinzi ili
rasilimali iliyowekwa iweze kufanya kazi muda wote. “Wananchi watambue mradi ni
mali yao,” Kakoso amesema. Ameishukuru na kuipongeza UCSAF kwa kufanya kazi ya
kufikisha huduma za mawasiliano kwenye maeneo ambayo hayana mvuto wa kibiashara
kama haya ili kuwawezesha wananchi kupata huduma za mawasiliano. Amefafanua
kuwa eneo hili lina wakazi wachache lakini UCSAF imefikisha huduma za
mawasiliano. Pia tumeshuhudia eneo hili lina wanafunzi wanasoma, nashauri UCSAF
muwapatie vifaa vya TEHAMA ili kuwawezesha kusoma vizuri zaidi.
Naye
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye amesema kuwa
Serikali iliilekeza Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuwekeza na kujenga kiwanda cha
sukari katika eneo la Mkulazi lililopo Kata ya Mkulazi, tarafa ya Ngerengere
mkoa wa Morogoro. Nditiye ameishukuru Kampuni ya simu ya Vodacom kwa kushirikiana
na UCSAF kujenga mnara na kufikisha huduma za mawasiliano kwa wananchi ambapo
amekuta mawasiliano kweli yapo. “Mawasiliano ni uchumi na ni usalama”, Nditiye
amesema. “UCSAF imefanya kazi kubwa sana, huku hakuna kampuni yeyote inaweza
kujitokeza peke yake kuja kuwekeza mawasiliano kwenye eneo kama hili bila
kupata ruzuku ya Serikali,” amesema Nditiye. Ameongeza kuwa, uwepo wa mnara huu
utawawezesha wawekezaji kuwasiliana ndani na hata nje ya nchi.
Katibu
Mtendaji wa UCSAF, Mhandisi Peter Ulanga amesema kuwa Mkulazi ni eneo ni jipya
la uwekezaji ambapo linafanyiwa uwekezaji na mifuko ya hifadhi ya jamii ya PPF
na NSSF na wamepewa eneo hilo na Serikali kujenga kiwanda cha sukari tangu
mwaka 2016 ambapo walifika UCSAF na kuiomba ijenge na kufikisha huduma za
mawasiliano kwenye eneo hilo kwa kuwa hapakuwa na mawasiliano ya aina yoyote.
Katika kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano kwa upande wa viwanda
na uwekezaji wa kujenga viwanda, “sisi
tulipokea ombi hilo na kuwasiliana na kampuni za simu ambapo Vodacom walikubali
na walichukua ruzuku na kujenga mnara huo,” amesema Ulanga.
Amefafanua
kuwa UCSAF tuliipatia Vodacom shilingi milioni 140 za kujenga mnara huo ambapo
nao wenyewe Vodacom waliongeza fedha zao kwa kuwa ujenzi wa mnara huo
umegharimu kiasi cha shilingi milioni 300.
Mnara huu umeanza kufanya kazi tangu miezi miwili iliyopita ha hadi sasa
una miezi minne tangu ulipoanza kujengwa.
Ulanga
ameongeza kuwa tayari UCSAF imeshapokea maombi kutoka kwa wajenzi wa Stigglers
Gorge ya kufikisha na kuboresha
mawasiliano kwenye maeneo yao ya makambi
ili kuwawezesha kupata huduma za mawasiliano wakati wa ujenzi wa mradi
huo ili waweze kuwasiliana.
Mwakilishi
wa Kampuni ya Vodacom kutoka Makao Makuu ya kampuni hiyo iliyopo Dar es Salaam
Mhandisi wa Mawasiliano na Mipango Bwana David Mbogela amesema kuwa eneo hilo
halikuwa na mawasiliano ya aina yoyote hapo awali ambapo wao wamejenga mnara
huo kwa kushirikiana na UCSAF. Ameongeza kuwa mnara huo unatumia nishati ya
umeme wa jua na jenereta ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata mawasiliano
wakati wote kwa kuwa hakuna chanzo kingine cha nishati ya umeme.
Naye
mwanakiji wa kijiji cha Mkulazi aishie maeneo hayo Bwana Naize Omary Uzuri ameishukuru na kuipongeza Serikali kwa
kuwawezesha kupata huduma za mawasiliano kwa kuwa katika kijiji chao tangu
huduma za mawasiliano zianze kutumika nchini, kijiji chao hakijawahi kupata
huduma hiyo.
Naibu
Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akitoa ufafanuzi
kwa wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu wakati wa ziara yao ya kukagua
upatikanaji wa huduma za mawasiliano kwenye eneo la kiwanda cha sukari lililopo
kijiji cha Mkulazi, Morogoro. Wa kwanza kushoto ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo
Mhe. Moshi Selemani Kakoso na wa pili kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa
Mawasiliano kwa Wote Mhandisi Peter Ulanga
Mtendaji
Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote Mhandisi Peter Ulanga akiongea na
waandishi wa habari kuhusu ufikishaji wa huduma za mawasiliano kwenye eneo la kiwanda
cha sukari cha Mkulazi kilichopo Morogoro wakati wa ziara ya wajumbe wa Kamati
ya Bunge ya Miundombinu (wanaomsikiliza). Anayesikiliza kwa makini wa tatu
kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Mawasiliano, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano Mhandisi Anjelina Madete
No comments :
Post a Comment