Thursday, April 26, 2018

WAFANYAKAZI TAASISI YA JKCI WAASWA KUENDELEA KUZINGATIA MAADILI YA KAZI



Katika kikao hicho mada mbalimbali zilijadiliwa  ikiwa ni pamoja na rushwa sehemu ya kazi, uendeshaji wa majukumu ya Baraza na kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Taasisi kwa mwaka wa fedha 2017/18.
  Mwenyekiti wa  Baraza la Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi akiongoza kikao cha baraza kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu Msaidizi wa Baraza hilo Renatha Miiruko.
Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakisikiliza mada ya rushwa sehemu ya kazi iliyotolewa na Asseri  Mandari  kutoka Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) makao makuu wakati wa kikao cha Baraza hilo kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.

Na Brighton James - JKCI,
WAFANYAKAZI wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kuepuka vitendo vya rushwa  ili waweze kutoa huduma bora ya bila upendeleo ya matibabu kwa wagonjwa.
Rai hiyo imetolewa leo na Asseri Mandari kutoka Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) makao makuu wakati akitoa mada ya rushwa sehemu ya kazi katika kikao cha Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Taasisi hiyo kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Mandari alisema kuwa katika maeneo mengine ya Hospitali baadhi ya wagonjwa  wanashidwa au kuchelewa kupata huduma bora kutokana na mazingira ya rushwa kutawala.
“Ninawapongeza kwa huduma bora ya matibabu ya moyo mnayoyatoa kwa wananchi jambo la muhimu ni  kufanya kazi zenu  kwa kufuata maadili ya utumishi wa Umma, kuwaheshimu wateja wenu bila ya kuwabagua kutokana na hali zao za maisha, kutumia lugha nzuri kwa wateja na kutunza siri ya kazi zenu”, alisisitiza Mandari.
Aliendelea kusema kuwa  athari zinazotokana na  vitendo vya rushwa ni pamoja na kushuka kwa pato la taifa kutokana na kushindwa kufikia malengo yaliyowekwa, kudumaza mipango ya maendeleo na kuchochea umaskini kwa mtu mmoja mmoja au zaidi.
Athari zingine ni  wananchi kukosa imani na Serikali iliyopo madarakani, kushuka kwa kiwango cha uwajibikaji kazini , kukwamisha utoaji wa haki na kuongezeka kwa maovu.
Akitoa mada kuhusu kazi na uendeshaji wa majukumu ya baraza Mkurugenzi Msaidizi wa Mabaraza kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu,Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu   Andrew Mwalwisi alisema baraza haliwezi kuwepo kama chama cha wafanyakazi hakipo hivyo basi  wajumbe wahakikishe wanawahamasisha wafanyakazi ili wajiunge na chama hicho.
Alisema wajumbe ni viongozi hivyo basi wanatakiwa kuwa na taarifa sahihi za maeneo yao ya kazi  na kushiriki kikamilifu katika vikao vya baraza la Wafanyakazi kwa kutoa mapendekezo na ushauri wa kitu gani Menejimenti ifanye ili kuboresha utoaji wa huduma na maslahi ya wafanyakazi na siyo kufanya maamuzi.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza  Prof. Mohamed Janabi aliwashukuru wajumbe wa baraza hilo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha kuwa huduma bora ya matibabu ya magonjwa ya moyo inatolewa  kwa wananchi.
“Mimi pamoja na Menejimenti yangu tutahakikisha kuwa maoni yote yaliyotolewa katika kikao hiki tunayafanyia kazi ili kuboresha ufanisi wa kazi katika Taasisi yetu. Nanyi wajumbe muhakikishe kuwa yale yote yaliyofundishwa na kujadiliwa  katika kikao hiki mnaenda kuyafanyia kazi”,
“Boresheni utendaji wenu wa  kazi kwa kuhakikisha mnatoa  huduma bora kwa wakati ikiwemo kuwahudumia vizuri wagonjwa na wateja wetu wengine , kuwahi kufika kazini na kuwepo eneo la kazi muda wote wa kazi kwa kufanya hivyo kutaongeza ufanisi wa kazi  na kupunguza  malalamiko kutoka kwa wananchi”,  alisema Prof. Janabi.

No comments :

Post a Comment