Mwenyekiti wa Baraza la
Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambaye pia ni Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi akiongoza kikao cha baraza
kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu Msaidizi wa Baraza
hilo Renatha Miiruko.
Na Brighton James - JKCI,
WAFANYAKAZI wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kuepuka vitendo vya
rushwa ili waweze kutoa huduma bora ya bila upendeleo ya matibabu kwa
wagonjwa.
Rai hiyo imetolewa
leo na Asseri Mandari kutoka Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU)
makao makuu wakati akitoa mada ya rushwa sehemu ya kazi katika kikao cha
Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Taasisi hiyo kilichofanyika leo jijini Dar
es Salaam.
Mandari alisema
kuwa katika maeneo mengine ya Hospitali baadhi ya wagonjwa wanashidwa au
kuchelewa kupata huduma bora kutokana na mazingira ya rushwa kutawala.
“Ninawapongeza kwa
huduma bora ya matibabu ya moyo mnayoyatoa kwa wananchi jambo la muhimu ni
kufanya kazi zenu kwa kufuata maadili ya utumishi wa Umma,
kuwaheshimu wateja wenu bila ya kuwabagua kutokana na hali zao za maisha,
kutumia lugha nzuri kwa wateja na kutunza siri ya kazi zenu”, alisisitiza
Mandari.
Aliendelea kusema
kuwa athari zinazotokana na vitendo vya rushwa ni pamoja na kushuka
kwa pato la taifa kutokana na kushindwa kufikia malengo yaliyowekwa, kudumaza
mipango ya maendeleo na kuchochea umaskini kwa mtu mmoja mmoja au zaidi.
Athari zingine ni
wananchi kukosa imani na Serikali iliyopo madarakani, kushuka kwa kiwango
cha uwajibikaji kazini , kukwamisha utoaji wa haki na kuongezeka kwa maovu.
Akitoa mada kuhusu
kazi na uendeshaji wa majukumu ya baraza Mkurugenzi Msaidizi wa Mabaraza kutoka
Ofisi ya Waziri Mkuu,Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu Andrew Mwalwisi alisema baraza haliwezi kuwepo kama chama cha
wafanyakazi hakipo hivyo basi wajumbe wahakikishe wanawahamasisha
wafanyakazi ili wajiunge na chama hicho.
Alisema wajumbe ni
viongozi hivyo basi wanatakiwa kuwa na taarifa sahihi za maeneo yao ya
kazi na kushiriki kikamilifu katika vikao vya baraza la Wafanyakazi kwa
kutoa mapendekezo na ushauri wa kitu gani Menejimenti ifanye ili kuboresha
utoaji wa huduma na maslahi ya wafanyakazi na siyo kufanya maamuzi.
Kwa upande wake
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza
Prof. Mohamed Janabi aliwashukuru wajumbe wa baraza hilo kwa kazi nzuri
wanayoifanya ya kuhakikisha kuwa huduma bora ya matibabu ya magonjwa ya moyo
inatolewa kwa wananchi.
“Mimi pamoja na
Menejimenti yangu tutahakikisha kuwa maoni yote yaliyotolewa katika kikao hiki
tunayafanyia kazi ili kuboresha ufanisi wa kazi katika Taasisi yetu. Nanyi
wajumbe muhakikishe kuwa yale yote yaliyofundishwa na kujadiliwa katika
kikao hiki mnaenda kuyafanyia kazi”,
“Boresheni
utendaji wenu wa kazi kwa kuhakikisha mnatoa huduma bora kwa wakati
ikiwemo kuwahudumia vizuri wagonjwa na wateja wetu wengine , kuwahi kufika
kazini na kuwepo eneo la kazi muda wote wa kazi kwa kufanya hivyo kutaongeza
ufanisi wa kazi na kupunguza malalamiko kutoka kwa wananchi”,
alisema Prof. Janabi.
No comments :
Post a Comment