Thursday, August 3, 2017

WCF ni mkombozi kwa wanaoumia, kufariki wakiwa kazini



Mkurugenzi Mkuu wa WCF Masha Mshomba (kulia), akimkabidhi Dk.Arnold Mtenga, cheti cha ushiriki wa mafunzo ya tathmini ya ajali na majeraha kwa mfanyakazi aliyeumia wakati akitekeleza majukumu yake mahala pakazi.


Na Christian Gaya. Mtanzania, Alhamis, Agosti 3, 2017
Watu wenye kipato cha chini hutumia muda mwingi mahali pa kazi huku kipato kikiwa hakitoshi kumudu maisha. Katika nchi yoyote ile uhalali au kukubalika kwa uchumi kunategemea haki za msingi za ajira, sawa na uwezo wa ...
kufanya kazi unaohitajika ili uchumi kukua.
Pia kuimarika kwa haki za kazi na za kijamii kunategema soko la kiuchumi lenye ufanisi na linalofanya kazi vizuri. Hii inaendana na kubadili mtindo wa siku zote wa uzalishaji duni, mapato ya chini na kuhatarisha maisha kazini na nafasi yake kuchukuliwa na utekelezaji wa kanuni za kimsingi za haki mahali pa kazi pamoja na ajenda ya mazingira bora ya kazi, pamoja na mkakati wa kuhakikisha usalama na fursa kwa wafanyakazi.

Dira iliyowekwa na shirika la kazi duniani inasema “Iwapo mazingira ya kazi yaliyopo yanajumuisha udhalimu, ugumu wa maisha na ufukara kwa idadi kubwa ya watu na hivyo kusababisha vurugu kubwa sana kiasi kwamba yanahatarisha amani na utulivu duniani; uboreshaji wa mazingira hayo unahitajika kwa haraka sana”.

Shirika la kazi duniani limeingiza dira hii katika ajenda ya kazi zenye staha ambayo inajumuisha matamanio ya watu ya kuwa na ajira ya kudumu yenye kuzalisha kipato ambayo inatoa kipato kwa haki, usalama mahali pa kazi na ulinzi wa kijamii, uhuru wa watu kueleza matatizo yao, kuandaa na kushiriki katika maamuzi ambayo yanaathiri maisha yao na kupata fursa usawa na kuwatendea haki.

Ili kukidhi matakwa ya mikataba ya kimataifa kuhusu fidia kwa wafanyakazi, Serikali ya Tanzania imeunda mfuko wa Fidia kwa wafanyakazi (WCF) ambao ni Taasisi ya Hifadhi ya Jamii.
Mkurugenzi mkuu wa WCF Masha Mshomba anasema Lengo la kuanzishwa kwa mfuko huu ni kushughulikia masuala ya Fidia kwa Wafanyakazi waliopo katika sekta ya umma na binafsi Tanzania bara ambao wataumia, kuugua ama kufariki kutokana na kazi wanazozifanya kwa mujibu wa mikataba ya ajira zao.
"Malengo yake ni kukidhi matakwa ya mikataba ya kimataifa kuhusu fidia kwa wafanyakazi kwa kulipa fidia stahiki pale mfanyakazi atakapoumia, kuugua ama kufariki, kutekeleza matakwa ya sera ya hifadhi ya jamii ya mwaka 2003, na kutekeleza matakwa ya kifungu cha 5 cha sheria ya fidia kwa wafanyakazi sura 263 marejeo ya mwaka 2015" anasema Mshomba.
Mfuko wa WCF una utaratibu wa kuwezesha kuharakisha malipo ya fidia kwa wafanyakazi ama wategemezi wao, una utaratibu mzuri wa  kupokea michango kutoka kwa waajiri na kufanya malipo.
"Kukuza na kuendeleza mbinu za kuzuia ajali, magonjwa ama kifo mahali pa kazi, kutoa huduma za ukarabati na ushauri nasaha na kukidhi matakwa ya kimataifa kuhusu fidia kwa wafanyakazi ndiyo baadhi ya malengo ya WCF", anasema.
Majukumu ya WCF ni kusajili waajiri wote, kufanya tathmini ya mazingira mahali pa kazi, kukusanya na kupokea michango kutoka kwa waajiri, na kuwekeza michango iliyokusanywa kwenye vitega uchumi.
"Mfuko hulipa fidia stahiki, hukuza mbinu za kuzuia ajali, magonjwa ama vifo vinavyotokana na kazi, hutoa elimu ya umma juu ya mfuko na hutunza kumbukumbu za matukio ya ajali, magonjwa ama vifo kutokana na kazi" Mshomba anataja zaidi majukumu ya mfuko.
Anasema mfuko huu wa fidia kwa wafanyakazi  unatoa mafao ya huduma ya matibabu, malipo ya ulemavu wa muda, malipo ya ulemavu wa kudumu, malipo kwa anayemhudumia mgonjwa, huduma za ukarabati na ushauri nasaha, msaada wa mazishi na malipo kwa wategemezi endapo mfanyakazi atafariki.
Christian Gaya ni mwanzilishi wa Kituo cha HakiPensheni Tanzania, mshauri na mtaalamu wa masuala ya pensheni. Kwa maelezo zaidi: gayagmc@yahoo.com unaweza kutembelea  www.hakipensheni monitor online na hakipensheni blog Simu +255 655 13 13 41 info@hakipensheni.co.tz

No comments :

Post a Comment