Thursday, August 3, 2017

Mradi Bomba la Mafuta kupaisha Bandari ya Tanga


Picha Na 1
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo (kulia) akielezea Mradi wa Bomba la Kusafirisha Mafuta Ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi katika Bandari ya Tanga nchini Tanzania unaotarajiwa kuzinduliwa Agosti 05, 2017 huko Chongoleani mkoani Tanga katika mahojiano maalum kwenye kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kupitia  kituo chake cha TBC1 jijini Dar es Salaam tarehe 03 Agosti, 2017. Kushoto ni mwongozaji wa kipindi hicho, Elisha Elia
Picha Na 2
Mwongozaji wa kipindi cha Jambo Tanzania kutoka Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), Elisha Elia (kushoto) akifafanua jambo katika mahojiano hayo. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo.
Picha Na 3
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo akielezea utekelezaji wa Miradi ya Umeme Vijijini Awamu ya Tatu inayosimamiwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwenye kituo cha redio cha TBC
……………………
Na Greyson Mwase, Dar es Salaam
Naibu  Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi  Juliana Pallangyo amesema  kuwa Bandari ya  Tanga inatarajia kuwa  ya kimataifa kabla na  baada ya...
kukamilika kwa Mradi  wa  Bomba la  Kusafirisha Mafuta  Ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi katika Bandari ya  Tanga nchini  Tanzania.
Dkt. Pallangyo aliyasema hayo tarehe 03 Agosti, 2017 jijijni  Dar es Salaam kupitia mahojiano maalum  kwenye  kipindi cha  Jambo  Tanzania  kinachorushwa na  Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kupitia kituo chake cha TBC1 lengo likiwa ni kuelezea uzinduzi wa Mradi wa  Bomba  hilo  utakaofanyika Agosti 05, 2017.
Alisema kiasi cha  Dola za Marekani milioni 200 kinatarajiwa kupatikana kama kodi wakati wa ujenzi na kuongeza kuwa mradi utatoa takribani ajira 10,000 kwa watanzania  hususan katika maeneo yatakayopitiwa na miundombinu  ya Bomba hilo.
Alisema  Serikali  kupitia  Wizara ya Nishati na Madini imejipanga katika kuhakikisha  kila  mwananchi aliye karibu na miundombinu ya Bomba hilo anakuwa sehemu ya uchumi wa bomba husika kupitia  ajira na utoaji wa huduma mbalimbali.
Aidha, alitoa  rai kwa wananchi husuan waliopo katika maeneo yatakayopitiwa na bomba hilo kujinga na Jumuiya ya Watoa Huduma Katika Sekta ya Mafuta na Gesi Tanzania (ATOGS) itakayokuwa na  jukumu la kuwaunganisha watoa huduma wote na kuwapa elimu ya namna bora ya kupata mikopo katika  taasisi za serikali na kutoa huduma bora kwa kampuni zitakazojenga  bomba hilo.
Akielezea usalama wa bomba hilo, Dkt. Pallangyo alisema Serikali imepanga mkakati maalum wa utoaji elimu kwa wananchi waishio karibu na miundombinu ya Bomba ili wawe walinzi na kufunga mfumo maalum wa usalama kwenye Bomba.
Katika hatua nyingine,  akielezea maandalizi ya  Tanzania kuelekea kwenye  uchumi wa Gesi na Mafuta, Dkt. Pallangyo alisema Serikali kupitia  Wizara ya Nishati na Madini imekuwa ikitoa ufadhili kwa wataalam wake na wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo ya Sayansi kwenda kusoma nje ya nchi masuala ya Mafuta na Gesi.
Aliongeza kuwa, kozi kuhusu masuala  ya Mafuta na Gesi imekuwa ikitolewa katika  vyuo  vikuu kama vile  Chuo Kikuu cha  Dar es Salaam (UDSM),  Chuo Kikuu cha  Dodoma (UDOM) na Chuo cha Madini Dodoma (MRI).
Akielezea utekelezaji wa Miradi ya Umeme  Vijijini Awamu ya Tatu inayotekelezwa na Wakala wa Nishati  Vijijini (REA), Dkt. Pallangyo alisema utekelezaji  utahusisha vipengele  vitatu ambavyo ni pamoja na  kusambaza umeme katika maeneo ambayo hayajafikiwa kabisa na miundombinu ya umeme na kuongeza wigo wa usambazaji  umeme katika  vijiji ambavyo vimefikiwa na miundombinu ya umeme lakini baadhi ya maeneo na vitongoji  havikuungwa.
Aliendelea kueleza kuwa Kipengele cha Tatu kinahusisha usambazaji wa umeme   utokanao na vyanzo vya Nishati Jadidifu kwenye maeneo yaliyo mbali  na  gridi hususan  visiwani.
Alisisitiza kuwa lengo la REA Awamu ya Tatu ni kuhakikisha kuwa vijiji vyote nchini vinafikiwa na umeme ifikapo mwaka 2021
Wakati huo huo, akielezea mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maji wa Stiegler’s Gorge wenye uwezo wa kuzalisha Megawati 2100, Dkt Pallangyo alisema kuwa maandalizi yameshaanza kwa  timu ya wataalam kupitia tafiti mbalimbali zilizowahi kufanywa  kuhusu mradi huo na kubadilishana uzoefu na wataalam kutoka nchi ya  Ethiopia ambao ni wazoefu kwenye  ujenzi wa mabwawa na mitambo ya kuzalisha  umeme kwa njia ya maji.
Alisema kukamilika kwa mradi huo kutapelekea nchi kupata Umeme wa uhakika na kuchochea kuongezeka kwa uwekezaji kwenye uchumi wa Viwanda.

No comments :

Post a Comment