Katibu Mkuu Wizara ya Maji na
Umwagiliaji Prof. Kitila Mkumbo (wa pili kutoka kushoto) akikagua mradi
wa kuchimba visima virefu 20 katika eneo la Kimbiji na Mpera Kigamboni
Jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mtendaji Mkuu wa DAWASA
Mhandisi Romanus Mwangi’ngo (katikati) akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu
Wizara ya Maji na Umwagiliaji Prof. Kitila Mkumbo kuhusu utekelezaji wa
mradi huo utakaowanufaisha wakazi wa Jiji la Dar es Salaam na Kisarawe
Mkoani Pwani wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo
unaotarajiwa kuzalisha maji lita milioni 260 kwa siku.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya
Serengeti Limited inayotekeleza mradi huo Bw. Mehrdad Talebi (kulia)
akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu Wizara ya Maji na Umwagiliaji Prof.
Kitila Mkumbo kuhusu hatua iliyofikiwa katika kutekeleza mradi huo
mapema leo.
Moja ya Visima Virefu vyenye kina
cha Mita 600 vikitoa maji wakati wa majaribio yaliyofanyika ili
kuonesha uwezo wa visima hivyo kuzalisha maji.
Katibu Mkuu Wizara ya Maji na
Umwagiliaji Prof. Kitila Mkumbo akinywa maji yanayozalishwa na visima
hivyo mara baada ya kukagua mradi huo leo ikiwa ni sehemu ya ziara yake
kukagua miradi ya maji inayotekelezwa na DAWASA.
……………………………………………………………………………………
Frank Mvungi – Maelezo
Serikali inatekeleza mradi mkubwa
wa uchimbaji Visima virefu 20 wenye thamani ya bilioni 40 katika eneo
la Kimbiji na mpera vyenye kina cha mita 600 kila kimoja,
vitakavyowezesha
kuzalishwa kwa jumla ya lita milioni 260 za maji kwa
siku.
Akizungumza wakati wa ziara ya
kukagua maendeleo ya mradi huo unaotekelezwa na Mamlaka ya Maji Safi na
Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na
Umwagiliaji Prof. Kitila Mkumbo amesema dhamira ya Serikali ya Awamu ya
Tano ni kuhakikisha kuwa kila mtanzania anafikiwa na huduma ya maji
safi na salama kote nchini.
“Visima vya Kimbiji na Mpera ni
moja ya miradi ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali kupitia DAWASA
yenye lengo la kuongeza wingi wa maji katika eneo la huduma ya Mamlaka
hiyo kutoka lita milioni 300 hadi kufikia zaidi ya lita milioni 700
ambazo zinajumuisha maji yanayozalishwa katika vyanzo vya Ruvu Juu na
Ruvu Chini yatakayokidhi mahitaji hadi kufikia mwaka 2032.” Alisisitiza
Prof. Mkumbo
Akifafanua Profesa Kitila amesema
tayari visima 17 kati ya 20 vimeshachimbwa na baadhi vipo katika hatua
ya upimaji wa wingi wa maji (pump testing).
“Hali ya upatikanaji wa maji
katika Jiji la Dar es Salaam inaendelea kuimarika na nchini kwa ujumla
lengo likiwa kuwafikia watanzania kwa zaidi ya asilimia 95,” aliongeza
Prof. Mkumbo.
Aliongeza kuwa mradi huo pamoja
na ile ya Ruvu Juu na Ruvu chini sasa itaondoa kabisa tatizo la maji
katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo yote yanayohudumiwa na Mamlaka
hiyo ikiwemo Kigamboni, Mji mpya, Kongowe, Gongo la mboto, Pugu,
Chanika, Mbagala na Mji wa Mkuranga Mkoani Pwani na maeneo mengine ya
Jiji la Dar es Salaam.
Kwa upande wake Kaimu Mtendaji
Mkuu wa Mamlaka hiyo Bw. Romanus Mwangi’ngo amesema kazi ya usanifu wa
kulaza miundombinu ya kusafirishia maji imekamilika.
Mradi wa uchimbaji visima vya
Kimbiji na Mpera unatekelezwa na Serikali kupitia Kampuni ya NSPT ya
Iran na Serengeti ya Tanzania kwa gharama ya bilionii 40 za Tanzania
ukiwa na lengo la kumaliza changamoto ya upatikanaji wa maji katika Jiji
la Dar es Salaam.
No comments :
Post a Comment