Thursday, March 23, 2017

Wanachama PSPF kupata mikopo nafuu kupitia CRDB




Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni wa PSPF, Bw. Adam Mayingu, (kushoto), akizungumza jambo na Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya CRDB, Dkt. Charels Kimei, wakati wa uzinduzi wa ushirikiano baina ya taasisi hizi mbili ambapo PSPF sasa itawakopesha wanachama wake kwa kupitia Benki ya CRDB  kwenye maeneo ya elimu, viwanja na pesa za kuanzia maisha. 


Christian Gaya
Mfuko wa PSPF na CRDB wanalenga kupanua uwigo wa huduma na fursa kwa wanachama wa PSPF kujipatia huduma ya mikopo nafuu kwa kiwango cha riba  kilicho chini ya kile kinachotolewa katika soko na taasisi zingine za kifedha nchini. Mfuko umeona haja ya kushirikiana na CRDB kuanzisha huduma hii kupitia mtandao wa CRDB ulioenea nchi nzima nchini

Akizungumza kwenye hafla ya utiaji saini mpango huo, Mkurugenzi Mkuu  wa PSPF, Bw Adam Mayingu, anasema kuwa mpango huu wa kutoa mikopo kwa wanachama ulianza tangu Desemba 2014 kwa kupitia taasisi nyingine za kifedha.

Mikopo hiyo ni pamoja na mkopo wa elimu, mkopo wa kuanzia maisha na mkopo wa viwanja yaani nipo site na PSPF

Anafafanua ya kuwa kwa upande wa mkopo wa elimu, mwanachama anaweza kukopa kwa ajili ya kujiendeleza kielimu katika ngazi yeyote ya elimu. Ngazi hiyo ni  stashahada, shahada, shahada ya uzamili na hata mafunzo ya ufundi.
 
Mkopo wa elimu ni huduma nyingine inayolengwa na ushirikiano huu kati ya PSPF na CRDB.
 
"Kupitia huduma hii mwanachama wa PSPF atafaidi matunda ya uanachama wake kwa kuweza kupata mkopo utakaomwezesha kujiendeleza kielemu na kuzifikia ndoto za kupata elimu ya juu. mkopo huu utatolewa kwa mwanachama wa PSPF aliyechangia katika mfuko kwa muda usiopungua miezi 24" Mayingu anasema.

Kwa upande wa mkopo wa kuanzia maisha, anasema mwanachama aliyepata ajira kwa mara ya kwanza huwa na mahitaji yake muhimu na kwa kutambua hilo, PSPF kwa kushirikiana na CRDB wameanzisha  mpango huu ambapo mwanachama anaruhusiwa kukopa mishahara yake ya miezi miwili ili aweze kujipanga na maisha mapya ya ajira. Na kurejesha mkopo huu kupitia makato madogo madogo ya mshahara wake kwa kipindi cha miaka miwili hadi mitano.

"Ni kweli usiopingika wengi wa waajiriwa wapya hukutana na changamoto kadha ikiwa ni pamoja na ile ya kumudu gharama za kuanza maisha pale wanapoajiriwa katika maeneo yao ya kazi. kwa kuzingatia hilo mfuko ulianzisha mkopo huu kumwezesha mwajiriwa mpya kujiandaa na changamoto hizi mpya kimaisha" Mayingu anafafanua.

Anaendelea kufafanua ya kuwa chini ya makubaliano haya ya PSPF na CRDB, mwanachama wa PSPF aliyechangia katika mfuko kwa kipindi cha kati ya miezi 6 na kisichozidi miezi 12 ataweza kupata mkopo huu nafuu kupitia CRDB ili kumwezesha kumudu gharama za awali kama vile: kulipia kodi ya nyumba, kununua fenicha za ndani, kununua nyenzo za usafiri, kununua kiwanja au shamba pamoja na kugharamia shughuli mbalimbali za kijamii.

Kuhusu mkopo wa viwanja  kwa wanachama, anasema  kuwa  huduma hii itawawezesha wanachama wa PSPF kukopa na kumiliki viwanja vya makazi ambavyo vinapatikana  maeneo mbali mbali ya nchi.

“Lengo  kubwa hapa ni kuwawezesha wanachama wa PSPF kumiliki viwanja vya makazi vilivyopimwa iii kuwaepusha dhidi ya ujenzi katika makazi holela, ambayo yamekuwa na gharama kubwa kuliko makazi yaliyopangiliwa”,anasema.

Alifafanua kuwa lengo kubwa la kuanzisha mikopo hiyo ni kuhakikisha kila mtanzania anatimiza ndoto  yake ikiwa ni katika masomo kupitia mkopo wa  elimu, ndoto yake nyingine kupitia mkopo wa kuanzia maisha au mkopo wa viwanja.
 Afisa Uhusiano Mwandamizi wa PSPF, Bw. Abdul Njaidi, akitoa hotuba ya ukaribisho
Anasema mkopo wa viwanja vya makazi ni eneo jingine linalolengwa na ushirikiano huu kati ya PSPF na CRDB. Huduma hii ilianzishwa na PSPF ili kuwawezesha wanachama wake pote nchini kumiliki na kuishi katika makazi bora yaliyopimwa. kupitia mkopo huu mwanachama wa PSPF anaondolewa ugumu unaotokana na gharama kubwa za kumiliki ardhi katika maeneo yaliyopimwa kisheria.

"Chini ya makubaliano haya kati ya PSPF na CRDB mwanachama yeyote wa PSPF aliyechangia katika mfuko kwa kipindi cha kati ya miezi 6 na kisichozidi miaka 60, anaweza kukopa mkopo huu kupitia CRDB na kurejesha mkopo huu kupitia makato madogo madogo ya mshahara wake kati ya kipindi cha miaka 2 hadi 5" anafafanua.

Anasema katika awamu hii ya pili ya utekelezaji wa huduma hii maeneo yafuatayo yamelengwa na mpango huu: Dar es salaam, Morogoro, Pwani, Dodoma, Songea, Tabora, Lindi, Singida, Arusha, Kagera, Mwanza, Iringa, Shinyanga, Mpanda, Katavi, Tanga, Kigoma na Mtwara.

"Mara zote PSPF inajivunia ubunifu ambao umeufanya mfuko huu kuwa wa kwanza hasa kwa upande wa mafao kwa wanachama . Ubunifu wa PSPF  umekuwa kivutio sio tu kwa wanachama wake bali pia kwa mifuko mingine ya pensheni nchini. Hivyo natoa wito kwa watanzania wenzetu kujiunga na PSPF ili waweze kunufaida na fursa hizi", Mkurugenzi mkuu wa PSPF ndugu Mayingu anasema.

Mayingu anataja ya kuwa hadi kufikia tarehe 17 Mwezi huu idadi ya wanachama walionufaika na mikopo  hiyo na idadi kwenye mabano ni  Elimu  (1,432)), mkopo wa kuanzia maisha  (847), mkopo wa viwanja (58).

“Kwa kushirikiana na benki ya CRDB ambayo ina mtandao mkubwa wa matawi hapa nchini tunaamini watanzania wengi watanufaika na mikopo hii na kwa kufanya hivyo tutakuwa tunatakeleza juhudi za serikali ya awamu ya tano ya kuhakikisha watanzania wengi zaidi wananufaika na huduma mbali mbali za Mifuko ya Hifadhi ya jamii”, anaeleza.


Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk Charles Kimei, anasema azma yao ni kuhakikisha kuwa ushirikiano na wadau wanamkomboa kiuchumi mwananchi  hususan mwenye kipato cha chini  kwa kumpatia  mkopo wenye riba ya asilimia 14 tu kwa mwaka. Kuhusu marejesho anasema ni kuanzia mwaka mmoja hadi miaka mitano.

Ushirikiano wetu na PSPF  bado una muendeleo ulio mpana kwani kwa pamoja tunadhamiria hapo baadae kuingiza sokoni mikopo kwa ajili ya wastaafu yaani ‘pensioners’.

Anasema mpango huu wa utoaji wa mikopo kwa wastaafu una lengo la kuleta faraja na kuwasaidia wastaafu katika kukidhi mahitaji yao mbali mbali ya kimaisha ikiwamo kulipia gharama za matibabu, ada za shule za watoto au wajukuu  na kuendesha biashara ndogo ndogo zitakazosaidia kupunguza ukali wa maisha ya kila siku.
 
 Dkt. Charles Kimei, akitoa hotuba yake kueleza jinsi benki yake ilivyofurahishwa na ushirikiano huo.
Dkt Kimei anafafanua kuwa  nia yao ni kujenga mazingira mazuri kwa wastaafu walio wanachama wa PSPF ili kustaafu kusiogopwe na kuonekana ni mwanzo wa kuanza kwa kipindi cha maisha ya shida yasiyokuwa na  matumaini.

“Tunataka kujenga tabia ya kuwafanya wafanyakazi wanapopata barua za kustaafu wasihuzunike kama ilivyozoeleka”,anadokeza
na kusema ya kuwa mwanachama wa PSPF anayetaka mkopo anatakiwa aende kwenye tawi lolote la benki ya CRDB ililopo karibu naye ili kupata huduma Dkt Kimei anasema

Christian Gaya ni mwanzilishi wa Kituo cha HakiPensheni Tanzania, mshauri na mtaalamu wa masuala ya pensheni. Kwa maelezo zaidi wasiliana kwa: gayagmc@yahoo.com unaweza kutembelea tovuti hakipensheni monitor online na hakipensheni blog Simu namba +255 655 13 13 41

No comments :

Post a Comment