Sunday, February 5, 2017

NI MUHIMU WANANCHI KUPATA TAARIFA ZA MIRADI YA UJENZI WA MIUNDOMBINU YA UMMA


   Cort-of-arms
  Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Ni jambo lisilopingika kuwa matumizi makubwa ya fedha za Serikali yanatumika katika ujenzi wa miundombinu ya Umma ambapo matumizi hayo yanahusisha karibu asilimia 53 ya Bajeti nzima ya nchi.

Tunaishukuru Serikali kwa kuweka kipaumbele katika suala hilo kwani ni muhimu kuwa na miundombinu mizuri na bora ili kutoa huduma bora kwa wananchi na kurahisisha ufanyaji kazi hivyo kuharakisha maendeleo ya nchi katika Nyanja zote muhimu zikiwemo za biashara, utalii na mawasiliano.
Miradi ya ujenzi ya miundombinu ya Umma inayoelezewa hapa ni ile ambayo inajengwa kwa fedha za Serikali kwa ajili ya matumizi ya wananchi wote ikiwemo ya barabara, hospitali na vituo vya afya,shule,vyuo,nyumba za kuishi pamoja na ofisi mbalimbali.
Jitihada hizo za Serikali kuhakikisha miundombinu ya Umma inaleta maendeleo imekuwa ikikwamishwa na changamoto mbalimbali zinazojitokeza pindi mradi husika unavyoanza kwani wahusika wanakuwa wanajiamulia jinsi ya kufanya ili mradi ujenzi husika umalizike.
Hali hiyo inapelekea Serikali kupata hasara kwa kupoteza fedha nyingi na kuambulia kubaki na majengo yasiyo na viwango ambayo mwisho wake hushindwa kutumika na kuilazimu Serikali kuanza upya ujenzi husika baada ya kubomoa.
Kwa kuwa Serikali hii ni sikivu na imejipanga kuhakikisha nchi inafika katika uchumi wa kati basi tunaamini mambo hayo hayana nafasi na hayawezi kutokea tena katika nchi hii watu kuachiwa uhuru wa kutumia vibaya fedha za Umma zinazotolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu.
Tunaamini kuwa maendeleo ya nchi yanachangiwa na wananchi wenyewe kwa njia ya ukusanyaji wa kodi na ushuru mbalimbali hivyo hata miundombinu ya umma inajengwa kwa kutumia fedha za wananchi zinazopatikana kwa njia ya ukusanyaji mapato.
Hivyo, ili kuifanya Serikali kuwa na taswira nzuri kwa wananchi wao pamoja na kuwafanya wananchi kuiamini Serikali yao ni vizuri kuwapa taarifa juu ya matumizi ya fedha hizo wanazozikusanya.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano,(Ujenzi), Mhandisi. Joseph Nyamuhanga amewahi kusema kuwa Sekta ya Ujenzi ni sekta moja wapo inayoonekana imekithiri kwa rushwa duniani kwa sababu takribani asilimia 10 hadi 30 ya Bajeti yake inapotea kwa njia ya rushwa na usimamizi mbaya hivyo ili kuondoa dhima hii ni lazima kukusanya na kutoa taarifa kwa wananchi juu ya ujenzi wa miundombinu hiyo.
Kuwapa taarifa wananchi juu ya miradi mbalimbali haswa ya ujenzi wa miundombinu kutaamsha ile hali ya watu kuona umuhimu wa kulipa kodi kwa sababu wanaona matumizi ya fedha wanazozikusanya.
Taarifa hizo pia zitaendeleza uwajibikaji na uwazi katika ujenzi wa miundombinu hiyo hivyo kupunguza vitendo vya rushwa,kujenga miundombinu inayoendana na thamani ya fedha zilizotolewa kwa ajili ya ujenzi husika pamoja na kujenga miundo mbinu bora na imara.
Ni muhimu kwa Serikali kupitia miradi yote iliyojengwa na inayoendelea kujengwa kwa kutumia fedha za Umma ili kugundua thamani halisi ya majengo hayo na kutoa taarifa kwa wananchi.
Jambo hili pia litasaidia vyombo husika vya kisheria kuwachukulia hatua watu wote walioshiriki kutumia vibaya fedha za wananchi kwa kujenga miundombinu iliyo chini ya kiwango au isiyoendana na thamani ya fedha iliyotolewa kwa ajili ya ujenzi husika.
Rai inatolewa kwa wizara na idara zinazohusika na ujenzi wa mioundombinu ya umma kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi juu ya mradi upi uko wapi na unathamani gani ili wananchi waweze kupima kama kiasi walichoambiwa kimetumika kina thamani ya fedha waliyoambiwa?
Pia ni muhimu wananchi wakaelimishwa juu ya umuhimu wa kuwa walinzi katika miundombinu hiyo ili isitokee watu wachache wakuihujumu kwani fedha nyingi za walipa kodi zimetumika.

No comments :

Post a Comment