Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Simbachawene akitoa
ufafanuzi kwa Umma kuhusu agizo alilolitoa Rais Dkt John Magufuli hivi
karibuni juu ya kusitisha zoezi la kuwahamisha Wafanyabiashara ndogo
ndogo maarufu Wamachinga, kulia kwake ni Mkurugenzi Idara ya Tawala za
Mikoa TAMISEMI Susan Chekani na kushoto kwake ni Naibu Katibu Mkuu Ofisi
ya Rais TAMISEMI (Afya) Dk. Zainab Chaula.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Simbachawene akitoa maelezo
kwa waandishi wa habari juu ya kutoeleweka vema Agizo la Rais Dkt. John
Magufuli kuhusu zoezi la usitishaji wa kuwaondoa Wafanyabiashara ndogo
ndogo katikati ya miji na kuwatafutia maeneo rafiki kufanyia biashara
zao kushoto kwake ni Naibu Katibu TAMISEMI (Afya) Dk. Zainab Chaula.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) George Simbachawene akitoa Agizo
juu ya Shule za Sekondari za Makuyuni (Arusha) na Milundikwa (Rukwa)
ambazo majengo yake yalikuwa ni makambi ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT)
na baadae Halmashauri zikapewa kuyatumia majengo hayo kama shule za
Bweni na kwa sasa zinarejeshwa tena mikononi mwa Jeshi kutokana na
kuongezeka kwa shughuli za Jeshi.
……………….
Serikali imewaagiza Wakuu wa Mikoa, Wilaya
na Mamlaka ya Serikali za Mitaa wameagizwa kuhakikisha wanatekeleza
agizo la Rais Dk.John Magufuli la kuwatafutia maeneo ya kufanyia
biashara Wafanyabiashara ndogo ndogo ‘wamachinga’ na si kuwaacha wafanye
biashara zao kiholela.
Kauli hiyo ilitolewa leo na Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(Tamisemi),
George Simbachawene alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini
Dodoma.
Amewataka wakuu hao kuwawekea Wamachinga
utaratibu wa kupangiwa maeneo ya shughuli zao yenye wateja wa kutosha,
miundombinu rafiki na washirikishwe katika michakato yote wakati wa
maandalizi ya maeneo hayo.
Amefafanua kuwa Rais Magufuli alisitisha
zoezi la kuwaondoa kiholela wamachinga kutoka katika maeneo wanayofanyia
biashara zao kwasasa hadi pale mamlaka husika zitakapoandaa maeneo
maalum kwa ajili yao.
“Maagizo ya Rais yameonesha namna
anavyowapenda na kuwathamini wamachinga na aliweka msisitizo
wasiondolewe mpaka pale yatakapotengwa maeneo mbadala,”amesema
Simbachawene.
Amebainisha utaratibu wowote wa kuwapangia
maeneo mapya uzingatie ushirikishwaji ili kuondoa msuguano wakati wa
kuwahamisha na kwamba pale inapowezekana wapangiwe maeneo ya katikati ya
mji ikibidi kuteua mitaa mahsusi kwa utaratibu utakaowekwa ili wafanye
biashara zao.
Pamoja na maelezo hayo, Simbachawene
amesema Rais alisisitiza kwamba maagizo yake juu ya wamachinga hayana
maana kuwa kwasasa wamachinga wafanye biashara zao kwenye barabara za
kupita magari na watembea kwa miguu au kwenye hifadhi za barabara.
Amewasisitiza wakuu hao kujipanga
kutekeleza maagizo ya rais kwa ufasaha, weledi na umakini mkubwa ili
kuwasaidia wamachinga kufanya biashara zao na kujipatia kipato na
kuzitaka mamlaka za serikali kuheshimu shughuli zao.
Wakati huo huo, Simbachawene amewaagiza
Makatibu Tawala wa Mikoa ya Rukwa na Arusha watafute shule ndani ya
mikoa yao na kuwapanga wanafunzi ambao wameondolewa shule za sekondari
Makuyuni na Milundikwa ambazo majengo yake yamerudishwa Jeshi la Kujenga
Taifa(JKT).
Amesema serikali imelazimika kuwaondoa
wanafunzi 254 wa shule ya Makuyuni wa kidato cha kwanza hadi cha tatu na
katika shule ya Milundikwa wanafunzi 120 wa kidato cha tano na sita.
Pia amesema walimu na watumishi wasio
walimu ambao walikuwa wakifundisha katika shule hizo wapangiwe kwenye
shule watakazopelekwa wanafunzi hao.
Ametaka utekelezaji huo wa agizo hilo
ufanyike kabla shule hazijafunguliwa januari 2017 na lizingatie
kutowavuruga wanafunzi wa kidato cha sita ambao tayari wamesajiliwa
kufanya mtihani wa Taifa mwezi mei, 2017.
No comments :
Post a Comment