Monday, June 16, 2014

Fao la elimu la mfuko wa pensheni wa PPF



  
Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya wasichana, Marian, iliyoko Bagamoyo mkoani Pwani, ambao wanasoma na kulipiwa ada na PPF kupitia fao la elimu baada ya wazazi wao kufariki dunia, kutoka kushoto na madarasa yao kwenye mabano ni Debora Kibona (Kidato cha tatu), Eileen Amon Urio, (Kidato cha tatu) na Rosalia Faustin Madulu (Kidato cha Kwanza)

 Na Christian Gaya, majira machi 17, 2014
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Kanisa Katoliki, Muadhama Policarp Kadinali Pengo ameupongeza mfuko wa pensheni wa PPF kwa udhamini wa siku ya familia wa shule za Marian zilizopo Bagamoyo mkoa wa Pwani, na jinsi alivyofurahishwa na juhudi za Marian zilizoanza kujenga chuo kikuu cha sayansi cha Marian Bagamoyo


Shule ya Marian iliyoko Bagamoyo mkoa wa Pwani imeshaanza tayari kujenga chuo kikuu cha sayansi ikiwa  na lengo la kuwapa motisha kwa wanafunzi wanaopenda kujiendeleza na masomo ya sayansi na kutimiza ndoto zao za kuwa wanasayansi wanaotegemewa na jamii ya Kitanzania. Haya yalitamkwa na meneja wa shule za marian nchini padri  Valentiono Bayo Siku ya Familia ya Marian iliyokuwa imedhaminiwa na Mfuko wa Pensheni wa PPF.

Alisema wazo la kuanzisha chuo kikuu cha sayansi lilianza tangia miaka 13 iliyopita (2003) na kwa miaka yote utawala na uongozi wa marian umekuwa ukiandaa na kutimiza mipango na kwamba mpaka sasa majengo ya kemia, fizikia na bailojia yako hatua ya juu zaidi

“Tunalenga kutoa wanasayansi wa kutosha kwa siku zijazo. Kwa kufanya hivi tunaiunga mkono serikali kwa vitendo katika zake juhudi na nguvu zake za kuendeleza sekta ya sayansi na kuwa na wanasayansi wa kuaminika nchini” anasema Bayo.

Kulingana na Bayo chuo kikuu kitakuwa sehemu ya shule za marian nchini ili kuwezesha kutoa elimu kutoka shule ya awali mpaka hatua ya juu
“Chuo kikuu hiki kitaanza chini ya mwavuli wa chuo kikuu cha St Augustine Tanzania  (SAUT). Shule ya marian ilianza na wanafunzi 42 na wanafunzi 4 kwa mwaka 2007 lakini mpaka sasa  shule za marian imeandikisha wanafunzi wapatao zaidi ya 1,000.” Alibainisha.
Kwa upande wa meneja wa uhusiano na masoko wa PPF Bi Lulu Mengele anasema mpaka sasa mfuko wa pensheni wa PPF umetumia shilingi za kitanzania zipatazo bilioni 4.6 kutoka katika mfuko wa elimu wa kudhamini watoto wa wanachama wa PPF waliofiwa na wazazi wao  wanaosoma shule mbalimbali hapa nchini zikiwemo shule za Marian tangia mwaka 2003

Lulu anasema PPF ni mfuko wa pekee nchini unaotoa fao hili la elimu ambalo hutolewa kwa watoto wa mwanachama anayefariki akiwa katika akiwa katika ajira na tayari amekwisha changia miaka 3 au zaidi.
“Kwa muda wa miaka ipatayo 11 sasa tumekuwa tukitoa udhamini wa elimu kwa wanafunzi. Kwa mfano mwaka jana 2013 mfuko ulitumia shilingi milioni 813 kwa ajili ya kununuliwa vifaa na kulipia ada za wanafunzi wapatao 1,467 kuanzia shule ya awali mpaka sekondari” alisema. Wakati kwa mwaka 2012 pekee Mfuko ulisomesha watoto 1,333 kwa kuwalipia jumla ya shilingi milioni 682 katika shule 765 kutoka Tanzania Bara na Visiwani katika shule za msingi na sekondari.” Lulu anabainisha
 “Elimu ni nyezo muhimu katika maisha ya binadamu. Kutokana na nguvu ya elimu katika kukuza uchumi wa nchi, mataifa mengi duniani yaliyopata maendeleo ya kijamii na kiuchumi yamewekeza katika sekta ya elimu. Hakuna taifa lolote duniani ambalo linaweza kupata maendeleo bila watu wake kuwa na elimu na kwa maana hiyo hakuna maendeleo bila elimu. Elimu ndiyo inamfanya binadamu kuwa daktari, rubani, mhandisi na mtaalamu katika nyanja mbalimbali. Kwa kutambua hilo uwekezaji katika sekta hiyo umekuwa ukiongezeka. Leo hii kumesikika vilio vingi nchini vikilenga mazingira bora na fursa zaidi katika sekta ya elimu vinavyotokana na watu wengi kutambua nguvu ya elimu kwa vizazi vijavyo. Mfuko wa Pensheni wa PPF kwa kutambua umuhimu wa elimu mwaka 2003 ulianzisha fao la elimu. Sababu ya msingi iliyousukuma Mfuko huo kuanzisha fao hilo ni kutokana na umuhimu wa watoto wa mwanachama kuendelea kupata elimu hata baada ya mzazi wao kufariki” Anasema.
Lulu anaeleza ya kuwa Mfuko wa pensheni wa PPF ulianzisha fao la elimu kwa kuanza na watoto watatu ambao wazazi wao walifariki wakiwa katika ajira. Kuweza kubuni na kutoa fao la elimu kwa watoto wa Wanachama wenu waliofariki wakiwa kazini kwa kipindi cha miaka 11 sasa.  Kwa kufanya hivi mfuko wa pensheni wa PPF umewezesha watoto hawa kupata elimu, ambayo huenda wengeikosa kwa vile tu wazazi wao wametangulia mbele ya haki, na kwa rasilimali watu iliyoelimika kwa siku za usoni kwa taifa. 

Anaendelea kufafanua ya kwamba fao la elimu ni kati ya mafao saba yanayotolewa na Mfuko.  Anasema fao hili hujumuisha ulipaji wa karo za shule na mahitaji mengine ya mwanafunzi husika  yaani  kwa mtoto wa mwanachama aliyefariki kama vile sare, vifaa, usafiri na chakula kwa kuzingatia mshahara wa mzazi aliyekuwa mwanachama wa PPF.
“Gharama za ada na matumizi mengine hulipwa moja kwa moja kwenye shule ambazo watoto wanasoma bila kupitia kwa mzazi aliyebaki au mlezi, jambo ambalo linatoa uhakika kwamba fedha zinatumika kwa matumizi yaliyokusudiwa. Sababu za mfuko kuamua kuanzisha fao la elimu ni baada ya mfuko wa PPF kufanya utafiti yakinifu na kugundua kuwa watoto wengi wa wanachama wao wanashindwa kuendelea na masomo baada ya wazazi wao kufariki kwa kushindwa kulipa ada za shule na mahitaji mengine muhimu. Na imechangiwa na kwamba wengi wa ndugu wa marehemu na wasimamizi wa mirathi kuwa na vipaumbele vyao tofauti, ikiwemo kugawa urithi bila kuwawekea elimu kama kipaumbele kwa watoto wengi wa wanachama aliyefariki wakati yuko kazini.” Lulu anasema ambaye ndiye meneja uhusiano na masoko wa PPF.
Anabainisha ya kuwa fao la elimu hutolewa kwa watoto wasiozidi wanne wa mwanachama aliyefariki akiwa katika ajira baada ya kuchangia katika mfuko huo kwa miaka mitatu au zaidi. Fao hilo la elimu ni kati ya mafao saba yanayotolewa na mfuko wa pensheni wa PPF na limewavutia wengi wanaotambua nguvu ya  elimu na kujiunga na PPF ili waweze kufaidika na fursa zinazotolewa na Mfuko huo likiwamo fao la elimu linalotolewa baada mwanachama kufariki.
Ikumbukwe katika sherehe ya kutimiza miaka kumi tangia kuanzishwa kwa fao hilo pia kulikuwa na shuhuda za wanafunzi waliosomeshwa na wanaosomeshwa na Mfuko akiwemo Pascalia Thobias (19) wakati huo ambaye alikuwa amekata tamaa baada ya baba yake kufariki akiwa darasa la nne. Alisema, “Baba alipofariki nilijua ndio mwisho wangu wa kupata elimu kwa sababu baba ndiye aliyekuwa akifanya kazi na mama hakuwa na kazi ya kumuingizia kipato, nilijua kuwa huo ndiyo mwisho wa elimu yangu. Ila PPF ilianza kunilipia ada toka mwaka 2003 nikiwa darasa la nne mpaka kidato cha nne ambapo niliweza kufaulu vizuri” kwa kupata daraja la kwanza.

Rosalia Madulu mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Marian ambaye alihudhuria Siku ya Familia ya Marian naye anaushukuru mfuko wa PPF kwa kuendelea kumdhamini katika masomo yake tangia mwaka 2007 wakati yuko darasa la II mara tu baba yake alipofariki.
“Baada ya kufa baba yangu mama alikata tamaa juu ya kunisomesha mimi pamoja na ndugu zangu wengine, lakini tunashukuru PPF kwa kutushika mikono yetu wanafamilia wote na kutupa nguvu kuanzia wakati huo mpaka leo.” Rozalia anasema.  

Lulu anasema suala la maamuzi ya mirathi limeendelea kusababisha ucheleweshaji wa mafao yanayotakiwa kutolewa na Mfuko kwa wasimamizi wa mirathi au wategemezi pale mwanachama anapofariki akiwa katika ajira. Hivyo basi, ni vyema wanachama wetu wote wajenge tabia ya kuandika wosia na hii itasaidia kupunguza na kuondoa malumbano ya mirathi ambayo imekuwa ni kero kwa wajane na watoto wa marehemu

“Fao la elimu hutolewa ili kugharamia sehemu au gharama zote zinazohitajika katika elimu ya mtoto wa mwanachama  aliyefariki na gharama hizi ni kuanzia elimu ya chekechea hadi kidato cha sita. Mfuko huu ulifikia uamuzi wa kuwasomesha watoto hao kutokana na kuwepo kwa tatizo kwa wasimamizi wa mirathi pindi wazazi wa watoto hao wanapopoteza maisha”. Lulu anasema.

Anasema ili fao hilo litolewe kinachohitajika ni kwa mwajiri anatakiwa kutoa taarifa PPF pindi mfanyakazi  wake aliyekuwa mwanachama wa mfuko wa pensheni wa PPF anapofariki dunia pamoja na nakala ya cheti cha kifo na maelezo muhimu kuhusu mtoto au watoto wa marehemu majina kamili na majina ya shule .

Lulu anasema ya kuwa kila mtoto anagharamiwa na mfuko wa pensheni wa PPF kiasi kisichozidi 1/12 ya mshahara wa mwaka wa mwanachama aliyefariki akiwa katika ajira. Na kiasi hicho hutolewa kila mwaka kwa kila mtoto katika shule anayosoma mtoto ili kugharamia mahitaji ya elimu ya mtoto yanayohitajika katika  shule hiyo

Sifa na utaratibu wa utoaji wa fao la elimu pamoja na nyaraka zinazohitajika ni rahisi sana kwa wanachama na familia zao kuzipata  kwa “mfano mara wanapopata fomu ya maombi ya mafao ya elimu kutoka kwa mwajiri wa marehemu aliyekuwa mwanachama wa mfuko, maelezo ya shule anayosoma kila mtoto ikiwemo pia akaunti ya shule hiyo pamoja na nakala ya cheti cha kuzaliwa kilichothibitishwa kwa kila mtoto malipo yanaandaliwa mara moja na kuingizwa kwenye akaunti husika” Bi Lulu anasema

Anaeleza kuwa gharama za ada na matumizi mengine hulipwa moja kwa moja kwenye shule ambazo watoto wanasoma bila kupitia kwa mzazi aliyebaki au mlezi, jambo ambalo linatoa uhakika kwamba fedha zinatumika kwa matumizi yaliyokusudiwa.
Lulu anasema PPF imekuwa ikibeba majukumu ya mzazi ambaye amefariki akiwa kazini, kwa kuhakikisha watoto wake wanaendelea kupata elimu. Anatoa wito kwa wananchi kujiunga na PPF ili waweze kufaidika na mafao yanayotolewa na mfuko huo, likiwamo fao la elimu kwani limekuwa mkombozi kwa wanafunzi wengi nchini
Anaongeza kuwa mafanikio ya fao hilo hayapo tu katika idadi ya wanafunzi wanaowasomesha, bali pia katika matokeo ya mitihani yao baadhi ya watoto wanaofaidika na fao hilo hufaulu vizuri. "Kwa mfano katika matokeo ya mitihani ya kidato cha nne mwaka 2012 na 2013 miongoni mwa wanafunzi waliofaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza na la pili wapo wanaosomeshwa na PPF," anasema.
Anabainisha kuwa mbali na mafanikio hayo, pia fao hilo linakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwamo baadhi ya shule kushindwa kutuma ripoti za mitihani kwa PPF ambazo zingesaidia kutambua maendeleo ya wanafunzi hao, ili kujua namna bora zaidi ya kuboresha utoaji wa fao hilo
Lulu anawaomba wananchi wote kutoka katika sekta iliyo rasmi na isiyo rasmi na hata kwa wale waliojiajiri wenyewe na hata ambao ni wanachama wa mifuko mengine ya hifadhi ya jamii kujiunga na Mfuko wa Pensheni wa PPF kwa kutumia mfumo wa uwekezaji amana kama mfumo wa ziada kwa wanachama walio katika mfumo wa asili wa pensheni au walio katika mifumo ya lazima ya hifadhi ya jamii ili waweze kufaidika na fao la elimu na kuhakikisha maisha bora ya sasa na ya baadaye.
Changamoto nyingine ni katika kupata uhakika kuwa wanaosomeshwa ni watoto wanaostahili na si watoto wengine kwa majina ya watoto wa marehemu, hivyo inalazimu PPF kufanya uhakiki wa mara kwa mara jambo ambalo ni gharama kubwa.
Anasema waajiri wanatakiwa kutokuchelesha kutuma taarifa za vifo vya wafanyakazi wao mara wanapofariki.  "kwa sababu wasipotuma mapema inasababisha watoto wa marehemu wanachama kuchelewa kulipiwa ada, hususan pale kifo kinapotokea wakati mwaka mpya wa masomo” Lulu anasisitiza. Na changamoto nyingine ni kupata uhakika kuwa wanaosomeshwa ni watoto wanaostahili na si watoto wengine kwa majina ya watoto wa marehemu hivyo inalazimu PPF kufanya uhakiki wa mara kwa mara jambo ambalo ni gharama kubwa.
Lulu ambaye ni meneja wa mawasiliano na masoko kwa niaba  ya mkurugenzi mkuu wa mfuko wa pensheni wa PPF anawashauri watanzania ambao hawajajiunga na Mfuko huu kufanya hivyo mapema ili waweze kuwa sehemu ya wale wanaofaidika na mafao yanayotolewa ikiwa ni pamoja na fao la elimu. Anasema pia kwa ushirikiano wa uongozi, wafanyakazi, wanachama na wadau wote wa sekta ya hifadhi ya jamii nchini PPF itaendelea kuboresha huduma zake kwa wateja kama ilivyo kawaida yake kama ilivyofanya kwa kipindi chote chote cha miaka 35, tangu ilipoanzishwa mwaka 1978 hasa kwa kuhakikisha ya kuwa fao la elimu linatolewa kwa wakati na linaendelea kuwa bora zaidi.
Mfuko wa Pensheni wa PPF ulianzishwa Julai 1978 kwa sheria Namba 14 ya mwaka 1978 ambayo sasa inafahamika kama mfuko wa pensheni wa PPF yaani “PPF Pensions Fund Act” Sura ya 372 ya sheria za nchi yetu kama ilivyorekebishwa na sheria namba 5 ya mwaka 2012 kwa madhumuni ya kutoa mafao ya uzeeni na mafao mengine kwa wanachama wa Mfuko.  PPF ilianza ikiwa chini ya usimamizi wa Shirika la Bima la Taifa (NIC) kama Mfuko wa kwanza wa kuchangia wa Pensheni Tanzania kwa madhumuni ya kuandikisha wanachama, kukusanya michango, kuiwekeza pamoja na kulipa mafao ya muda mrefu na ya muda mrefu.
Mfuko huu wa PPF ulianzishwa ili kutoa huduma ya pensheni kwa wanachama katika utaratibu wa kuchangia. Huu ndio Mfuko wa kwanza wa pensheni Tanzania ulioanzishwa katika misingi ya kuchangia. Sheria ya Mfuko inaruhusu wanachama kutoka katika sekta rasmi na sekta isiyo rasmi kujiunga na Mfuko.

No comments :

Post a Comment