Tuesday, November 26, 2013

SSRA NA MIONGOZO YA UTENDAJI KWA SEKTA YA HIFADHI YA JAMII.


 .



PICHANI: Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Uhamasishaji wa SSRA Sarah Kibonde Msika akiongea na waandishi wa habari kuhusu Miongozo ya Sekta ya Hifadhi ya Jamii iliyotolewa na SSRA. Kushoto kwake ni Mkurugenzi wa Sheria wa SSRA Ngabo Ibrahim

Na Christian Gaya majira 26 Novemba 2013

PICHANI: Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Uhamasishaji wa SSRA Sarah Kibonde Msika akiongea na waandishi wa habari kuhusu Miongozo ya Sekta ya Hifadhi ya Jamii iliyotolewa na SSRA. Kulia kwake ni Mkurugenzi wa Sheria wa SSRA Ngabo Ibrahim.


Muundo wa kisheria wa mifuko ya hifadhi jamii nchini ni moja changamoto zinazoikabili Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii nchini (SSRA). Mpaka sasa mifuko inaendelea na mtindo wa kuwaruhusu wanachama wake kutoa mchango ya pensheni wakati wowote anapopatwa na majanga kama vile kuacha kazi au kuachishwa kazi, magojwa, ulemavu, kuolewa na wanapofikia umri wa miaka 55 ya hiyari au 60 ya lazima. Na mwanachama anapotoa michango hiyo ya pensheni uhusiano kati ya mwanachama na mfuko unakoma hapo hapo. 


Udhaifu mwingine ni kwamba mafao yanatolewa na baadhi ya mifuko mengine hayatambuliwi na shirika la kazi (ILO) kifungu cha 102 cha mwaka 1952 na hata hivyo mifuko mengi hairekebishi pensheni au mafao yanayotolewa kulingana na mfumuko wa bei ya wakati huo au mwongozeko wa kima cha chini cha mshahara . 


Riba wanayopata mwanachama kutokana na michango yake kuwekezwa kwenye miradi mbalimbali na mfuko inaendelea  kuporomoka kila mwaka mfano mwaka 1996-1997 mfuko mmoja ulitoa riba kwa wanachama wake kwa asilimia 12 ½ ambayo mpaka sasa imefika riba ya asilimia 0.0034 kwa mwaka kulingana na maelezo ya taarifa ya hesabu za michango ya wanachama  


Na kwa vile mwanachama wanachukua michango yote ya pensheni kwa mkupuo hivyo muda mfupi mtu huyo anabaki kuwa maskini zaidi, na kupatwa mawazo na magonjwa hatimaye kufa haraka na hivyo idadi ya watu maskini inazidi kuongezeka nchini. Mifuko haishughuliki au kuhusika  kabisa na majanga  hivyo yote yanatupiwa kwa mwanachama aliyejitoa. 


Pamoja na hayo mifuko hii yote ina wigo mdogo sana wa wanachama na wale ambao ni wanachama wa hifadhi ya jamii ni asilimia 6 ya nguvukazi ya idadi ya watu watu nchini.  Mpaka kufikia mwaka 2012 kulikuwa na jumla ya wastaafu wapatao 70,522. Na mbinu zinazotumika za uendeshaji wa mifuko zimepitwa na wakati. Nchi kwa muda mrefu haina sera kwa ajili ya kusimamia utawala bora wa hifadhi ya jamii na kwa maendeleo ya hifadihi nchini. 


Siyo hivyo mifuko ya hifadhi ya jamii mpaka sasa haina utaratibu wa kuhamisha michango ya mwanachama kutoka mfuko mmoja wa hifadhi ya jamii kwenda mwingine endapo mwanachama atapata mwajiri mwingine anayechangia labda PPF badala ya NSSF na hata akihamishwa kwenda nchi jirani kama vile Kenya au Uganda kama wanachama chini ya jumuuiya ya afrika mashariki hivyo anaishia kutoa na kuitumia anavyojua yeye mwanachama


Mpaka sasa mdhibiti na msimamizi wa mifuko ya hifadhi ya jamii (SSRA)  ameanza kuleta marekebisho ya baadhi ya vifungu vya sheria  kwa awamu kwa mfano waajiri wote katika utumishi wa umma na sekta binafsi wanapaswa kuzingatia matakwa ya sheria hii kwa kuwapa fursa watumishi wapya kujiunga na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya lazima wanayoitaka. Bado ni changamoto kubwa sana kwa SSRA kuleta na kufanya marekebisho haya yote.  kwani  mpaka sasa haya mashirika ya hifadhi ya jamii kila moja ina wizara yake inayoisimamia na kuwa utaratibu na kanuni tofauti za uendeshaji wa mifuko hii. Matokeo yake ni kwamba kiwango cha michango, mfumo wa mafao, na sifa za kupata mafao na hata mipako na vipa umbele vinatofautiana kabisa kwa kila mfuko. Kumekuwepo na fofauti kubwa kwenye ukokotoaji wa mafao na hata tofauti kubwa ya mafao kati ya mifuko

Mpaka sasa hakuna utaratibu ulioanzishwa wa kuruhusu haki za mafao ya mwanachama kuhamishwa kutoka mfuko mmoja hadi mwingine. Matokeo yake wafanyakazi wamekuwa wakipoteza baadhi ya haki zao za mafao wakati wakihama kutoka sehemu moja ya mwajiri hadi mwajiri mwingine. Pia hii imechangia sana kuongezeka kwa tabia ya kuondoa michango ya pensheni kabla haijakomaa. 


Kumekuwa hakuna soko huru la hifadhi ya jamii ambalo linaweza kumruhusu hata taasisi za watu binafsi au sekta za watu binafsi kuendesha mifuko ya hifadhi ya jamii kwa muda mrefu ingawa kwa sasa wameruhusu lakini muundo rasmi haujatoka bado kutoka kwa mdhibiti na msimamizi wa hifadhi ya jamii (SSRA) ; kumekuwepo na ukosefu wa takwimu sahihi; gharama kubwa za uendeshaji wa mifuko, uelewa mdogo wa hifadhi ya jamii kwa watunga sera, waajiri na waajiriwa na umma kwa ujumla.  kila mfuko una sera yake ya uwekezaji, wigo finyu wa hifadhi ya jamii kwa Watanzania yote kwa pamoja ikiwa imesajili asilimia mbili tu ya Watanzania wote.  


Miongozo ya uwekezezaji wa rasilimali za mifuko hii ya hifadhi ya jamii ingawa imetolewa tayari lakini haijaanza kutumika na baadhi ya mifuko. Mapungufu yaliyomo kwenye mfumo huu wa hifadhi ya jamii ambayo yanahitajika kutatuliwa na sera hii ya hifadhi ya jamii. Watu waliomo katika mifuko hii ya hifadhi ya jamii ni wale tu ambao wameajiriwa kwenye sekta iliyo rasmi
Mamlaka ya usimamizi na udhibiti wa sekta ya hifadhi ya jamii (SSRA) iliundwa kwa sheria Na 8 ya hifadhi ya jamii ya mwaka 2008 kwa lengo la kusimamia na kudhibiti sekta ya hifadhi ya jamii kwa manufaa ya wanachama na kwa taifa kwa ujumla. Hivyo basi Mamlaka ilianza kazi rasmi mwaka 2010 ingawa baadaye ilifanyiwa marekebisho chini ya kifungu cha sheria namba 5 cha mwaka 2012

Na jukumu kubwa la mamlaka ni kusimamia shughuli zote za hifadhi ya jamii nchini ikiwa ni pamoja na mifuko yote ya hifadhi ya jamii iliyo anzishwa kwa sheria ya bunge ambayo ni mifuko ya pensheni, mifuko ya akiba ,mifuko ya bima ya afya na mifuko ya hiari na kuhakikisha kwamba mifuko inakuwa endelevu ,inaendeshwa kwa kufuata kanuni na taratibu za kisheria, wanachama wanapata taarifa za mifuko yao ,mafao yanaboreshwa na serikari inapunguziwa mzigo .Dhana kubwa ya hifadhi ya jamii ni kwa ajili ya kuhusisha taratibu za ulinzi dhidi ya majanga ya kiuchumi na ya kijamii yanayosababishwa na kukoma au kupungua kipato kutokana na maradhi, uzazi, kuumia kazini, ukosefu wa ajira, ulemavu, uzee, kifo na kuongezeka kwa gharama za matibabu. 


Pamoja na hayo SSRA imepewa mamlaka makubwa ya kufanya tathmini ya mifuko ya hifadhi ya jamii, kuchukua hatua za kinidhamu pale inapobidi, kufanya kaguzi mbalimbali na kutekeleza wajibu mwingine wowote utakaohakikisha sekta ya hifadhi ya jamii inafanya kazi kwa ufanisi na kwa uongozi bora.  Majukumu ya mamlaka (SSRA) yameainishwa bayana chini ya kifungu cha 5(1) cha sheria ya mamlaka    ya usimamizi na udhibiti wa sekta ya hifadhi ya jamii kazi hizo ni pamoja na Kusajili mifuko, watunzaji na meneja wa uwezaji katika sekta ya hifadhi ya jamii. Kudhibiti/kurekebisha na kusimamia utendaji wa mifuko, watunzaji na meneja wa uwekezaji. Kuweka mazingira yakayopanua uwigo wa hifadhi ya jamii na kuongeza wanachama hasa kwenye sekta isiyo rasmi.


Mamlaka hii vile vile ina jukumu la kutoa miongozo ya utendaji sahihi na yenye ubora katika sekta ya hifadhi ya jamii. Kutetea na kulinda maslahi ya wanachama. Kuweka mazingira mazuri na yanayofaa kukuza na sekta ya hifadhi ya jamii. kuendeleza Kumshauri waziri juu ya sera na masuala ya utendaji kuhusiana na sekta ya hifadhi ya jamii.


Miongozo mengine ni pamoja na kupanga na kutangaza rasmi miongozo itakayo  tumika kwa mifuko, watunzaji na. Kusimamia na kupitia upya utendaji wa sekta ya hifadhi ya jamii. Kuanzisha mafunzo, kushauri, kuratibu na kutekeleza mabadiliko ya sheria katika hifadhi ya jamii. Kumteua mtu atakae simamia mifuko pale inapobidi. Kurahisisha upanuzi wa wigo wa hifadhi ya jamii kuwafikia wale ambao bado hawajafanikiwa ikiwa ni pamoja  na makundi/sekta zisizo rasmi . Kuendesha mipango ya elimu na uhamasishaji kwa umma juu ya masuala ya hifadhi ya jamii.
Vilevile Mamlaka  inajukumu la  kulinda, kutetea na kuendeleza maslahi ya wanachama wa sekta ya Hifadhi ya Jamii. Kwa kuzingatia haya, Mamlaka imetoa miongozo sita ambayo yote inalenga katika kuhakikisha kuwa sekta ya hifadhi ya jamii inakuwa bora na endelevu na hivyo kuboresha maisha ya wanachama na kuchangia maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Kwa upande wa uandikishaji wa wanachama Miongozo hii inalenga; Kuongoza Bodi za Mifuko ya hifadhi ya jamii  kufanya usajili wa wanachama kwa mujibu wa sheria; Kuhakikisha kwamba mwanachama mpya anapata haki yake ya kuchagua Mfuko wa Hifadhi ya Jamii anaopenda kujiunga nao; Kuondoa migongano kati ya Mifuko wakati wa uandikishaji wanachama wapya; Kuainisha taratibu kwa mwanachama wa Mfuko wa hiari kuhamia Mfuko wa lazima; Kuongeza  wigo wa wanachama katika sekta ya hifadhi ya jamii.


Miongozo ya  uwekezaji, hii inalenga ; Kuelekeza Bodi za Mifuko kufanya maamuzi ya uwekezaji kwa mujibu wa sheria; Kuhakikisha uwekezaji wa Mifuko unaleta maendeleo bila kuhatarisha afya ya Mifuko, pamoja na kuhakikisha uwekezaji unafanywa kwenye maeneo yenye tija, kukuza uchumi wa nchi na kuboresha mafao ya wanachama; Kuhakikisha kwamba Mifuko muda wote inaweza kulipa wanachama wanaostahili mafao; Kuhakikisha kuwa utawala bora; unazingatiwa katika shughuli zote za uwekezaji na Kuhakikisha kuwa  wanachama wananufaika na uwekezaji unaofanywa na Mifuko.


Mamlaka vile vile imetoa miongozo ya takwimu inayolenga; Kuainisha kumbukumbu ambazo ni lazima zitunzwe na Mifuko; Kuelekeza mifumo ya kuandaa na kuweka taarifa za Mifuko; Kuelekeza taratibu za kutoa taarifa za wanachama na michango yao; Kuelekeza taratibu za kuhahikisha kwamba taarifa za Mifuko zinapatikana muda wowote zinapohitajika.


Pamoja na hayo mamlaka imeweza kuja na miongozo ya utawala bora wa bodi za Wadhamini inayolenga; Kukuza utawala bora katika bodi za Mifuko;  Kanuni za Mifuko kuzingatia vigezo vya utawala bora katika uendeshaji wake; Kuwaongoza wadhamini kutimiza wajibu wao kisheria; Kuweka sifa na masharti ya mtu kuwa mjumbe wa Bodi ya Mfuko; Kuweka viwango vya taratibu na miundo vya kukuza utawala bora; Kukuza na kuendeleza imani ya umma kwa Mifuko


Kwa upande mwingine Mamlaka imeaanisha miongozo ya tathmini za Mifuko inayolenga: Kuweka taratibu za namna ya kufanya tathmini za mifuko; Kuweka vigezo vya kuzingatia kwa makampuni na wataalum wanaotarajia kufanya tathmini za mifuko; Kufanikisha kupata taarifa  ya tathmini inayoeleweka na yenye taarifa sahihi.


Mamlaka imeweza kuja na taratibu za miongozo ya kujumulisha vipindi vya michango inayolenga: Kuainisha taratibu za kujumlisha vipindi vya michango kwa wanachama waliochangia katika Mifuko zaidi ya mmoja; Kuainisha masharti ya kuunganisha vipindi; na Kumsaidia mwanachama aliyechangia Mfuko zaidi ya mmoja kupata haki yake stahiki.


Imefikia wakati sasa mifuko ya hifadhi ya jamii inahitaji kubadilika kimtazamo na kidira imefika wakati ambapo mteja huenda akaonekana ni mfalme. Mifuko ya jamii nchini inahitaji kujua hili ili kujipanga upya na kuhakikisha ya kuwa inajali wateja wao hasa kwa kutoa huduma bora kwa wanachama na wastaafu pamoja na washika dau wengine kama vile  wamama, wababa na watoto tegemezi. Mashirika ya hifadhi ya jamii yanahitaji kupokea malalamiko ya wanachama wao na kujibu kwa muda muafaka ili kuwaridhisha kama wenye wachagiaji wa michango hiyo. Wanahitaji kutimiza ahadi wanazotoa kwa wanachama kwa wakati muafaka na siyo vinginevyo. 


Wakati umefika wa kubadilisha sheria zilizopitwa na wakati na ukiritimba, kila mmoja anahitaji kuingia uwanjani kwa kuuza sera zake ili kumvutia mteja. Mifuko inahitajika kubadilika juu ya suara hili la mabadiliko ya marekebisho ya sheria na miongozo ya utendaji ya sekta ya hifadhi ya jamii nchini 

Christian Gaya ni mwanzilishi wa kituo cha HakiPensheni Tanzania, mshauri na mtaalamu wa masuala ya hakipensheni. Kwa maelezo zaidi wasiliana kwa barua pepe: gayagmc@yahoo.com AU kwa habari zaidi za kila siku juu ya HakiPensheni unaweza kutembelea tovuti www.hakipensheni.blogspot.com simu namba +255 655 13 13 41

No comments :

Post a Comment