Wednesday, January 12, 2022

MAREKANI KUWAJENGEA UWEZO VIONGOZI WANAWAKE WAFANYABIASHARA KUPITIA BIASHARA NA UWEKEZAJI




DAR ES SALAAM,

Naibu Waziri Mdogo wa Biashara wa Marekani anayeshughulikia Mashariki ya Kati na Afrika, Camille Richardson, aliendesha mkutano kwa njia ya mtandao kusaidia kujenga ubia kati ya wanawake wajasiriamali wa Marekani na wale wa Tanzania.

Mkutano huu uliopewa jina “Kuwaunganisha Wanawake Wajasiriamali wa Tanzania na Kwingineko (“Connecting with Women Entrepreneurs in Tanzania & Beyond”) na kuendeshwa na Naibu Waziri Mdogo Richardson ulikuwa ni mkutano wa 11 katika mlolongo wa mikutano ya kuwajengea uwezo wanawake ili waache urithi madhubuti kupitia biashara na uwekezaji (‘Women Empowered Leave Legacies Through Trade and Investment’-WELLTI). Mkutano wa Tanzania ulionyesha umuhimu ambao Wizara ya Biashara ya Marekani inaweka katika mahusiano ya kibiashara kati ya Marekani na Tanzania na ni sehemu ya ufuatiliaji wa ziara iliyofanywa kwa njia ya mtandao na Naibu Waziri Mdogo Richardson tarehe 22 na 23 Julai 2021.

“Wajasiriamali na wabunifu wanawake ni rasilimali kubwa sana ambayo tayari imeiva kwa kuingia nayo ubia wa kibiashara,” Alisema Naibu Waziri Mdogo Richardson na kuongeza kuwa “Programu za mabadilishano zinazofadhiliwa na Marekani zinaweza kutumiwa ili kuweza kukitumia kikamilifu chanzo hiki muhimu cha taarifa za masoko, kufikia mifumo ya ugavi na usambazaji na kupata wawakilishi wa bidhaa za Kimarekani nchini Tanzania.”

Katika mkutano huu, kikundi cha wafanyabiashara wanawake wa Kitanzania walichangia taarifa kuhusu masoko na zaidi ya makampuni 125 ya Kimarekani yenye nia ya kutafuta fursa za kibiashara katika kanda hii. Carol Ndosi, mwanzilishi mwenza wa Kampuni iitwayo Launch Pad Tanzania aliongoza jopo la watoa mada wa Kitanzania lililowajumuisha Dk. Victoria Kisyombe, mwanzilishi na Afisa Mtendaji Mkurugenzi Mkuu wa SELFINA; Miranda Naiman, Mbia Mwanzilishi wa Empower; na Mercy Kitomari, Mwanzilishi na Afisa Mtendaji Mkuu wa Notre Heritage Ltd. Watoa mada hawa waliangazia nguvu ya wajasiriamali wanawake katika kuyaletea faida makampuni ya Kimarekani yanayotaka kuingia au kupanua shughuli zake katika soko la Tanzania. Makampuni ya Kimarekani yapo katika nafasi nzuri zaidi ya kutumia rasilimali hii kutokana ma mtandao mpana wa wahitimu wa programu za mabadilishano waliopo Tanzania na barani kote Afrika.” Mtandao huu wa wahitimu unawajumuisha wahitimu wa Mpango wa Kujenga Uwezo wa Viongozi Vijana wa Afrika (YALI), wahitimu wa Mandela Washington Fellowship na wahitimu wa Programu ya Mafunzo kwa Wajasiriamali Wanawake (AWE).

Ushirikiano wa kibiashara kati ya Marekani na Tanzania ni wa kina sana ukienda sambamba na uhusiano rasmi baina ya nchi hizi mbili ambao mwaka huu umetimiza miaka 60. Hivi sasa makampuni ya Kimarekani yamewekeza nchini Tanzania kiasi cha Dola za Kimarekani bilioni 1.5 yakiajiri wafanyakazi 2,000. Katika mwaka 2020 Marekani na Tanzania zilifanya biashara yenye thamani ya jumla ya Dola za Kimarekani milioni 364, hivyo kuifanya Marekani kuwa mbia mkubwa kabisa wa kiabiashara wa tatu kwa Tanzania miongoni mwa wabia wake kutoka nje ya Afrika, na kwa jumla kuwa mshirika wa tano kwa ukubwa. Jumla ya biashara. Takwimu hizi za biashara na uwekezaji zinaonyesha haja ya kuongeza ubia na wajasiliamali wa humu nchini, ambapo wajasiriamali wanawake wa Kitanzania wanaweza kuwa na mchango na nafasi muhimu.

Mlolongo wa mikutano ya kuwajengea uwezo wanawake ili waache urithi madhubuti kupitia biashara na uwekezaji (WELLTI) ulizinduliwa na Wizara ya Biashara ya Marekani hapo Januari 2021 kama jukwaa la kuwaunganisha wanawake wajasiriamali wa Marekani na masoko ya kimataifa. Katika mwaka mmoja uliopita, mpango huu umekua kwa kasi katika nchi za Mashariki ya Kati na kilele chake kitakuwa mkutano mkubwa utakaoongozwa na Waziri wa Biashara wa Marekani Gina Raimondo utakaofanyika katika Siku ya Kimataifa ya Wanawake, mwezi Machi 2022 katika katika Banda la Marekani katika Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dubai (Dubai World Expo)

Kuhusu Kitengo cha Usimamizi wa Biashara za Kimataifa (International Trade Administration – ITA):

Kitengo cha Usimamizi wa Biashara za Kimataifa (ITA) katika Wizara ya Biashara ya Marekani ni rasilimali kubwa kwa Makampuni ya Kimarekani yanayoshindana katika soko la dunia. ITA ina zaidi ya wafanyakazi 2,200 wanaowasaidia wauzaji wa bidhaa nje ya nchi (exporters) wa Kimarekani katika zaidi ya miji 100 ya Marekani na masoko ya kimataifa zaidi ya 75. Kwa taarifa zaidi kuhusu ITA tembelea www.trade.gov.

No comments :

Post a Comment