Wednesday, November 17, 2021

STAMICO,BENKI YA KCB WAINGIA MAKUBALIANO YA KUTOA MIKOPO YA FEDHA KWA WACHIMBAJI

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Vennance Mwasse (kulia) na Mwakilishi wa Benki ya KCB, Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kiislamu wa Benki hiyo (Islamic Banking) Amour Muro (kushoto) wakibadilishana hati za makubaliano mara baada ya kutia saini makubaliano ya mashirikano katika kutoa mikopo kwa wachimbaji wadogo.


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

KATIKA kuendeleza sekta ya wachimbaji wadogo nchini Tanzania, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na Benki ya KCB wameingia makubaliano yanayolenga kushirikiana katika kutoa mikopo kwa wachimbaji wadogo kupata mikopo endelevu na kwa rahisi zaidi ili kufanya shughuli za uchimbaji zenye tija.

Akizungumza wakati wa tukio la utiwaji saini wa makubaliano hayo yaliyoingiwa leo Novemba 16,2021, jijini Dar es Salaam  Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Vennance Mwasse ameeeleza benki hiyo imekuwa ya kwanza kuingia makubaliano hayo yenye lengo la kuinua sekta ya wachimbaji wadogo wa madini na kwamba ushirikiano huo unakwenda kufungua ukurasa mpya.

DL.Mwasse amesema katika makubaliano hayo STAMICO itawajibika kutoa utaalam elekezi katika maeneo ya Jiolojia, Uchimbaji na Uchenjuaji Madini kwa miradi ya Wachimbaji Wadogo ambayo itafanya maombi ya mikopo na kuiwasilisha kwa Benki kabla ya utekelezaji wake.

"Kwa benki ya  KCB itawajibika kutoa mikopo kwa Wachimbaji Wadogo ambao watawasilisha maombi ya mikopo katika maeneo ya miradi ya uchimbaji madini itakayokidhi vigezo vya kupewa mikopo,"amesema  Dkt. Mwasse na kusisitiza makubaliano hayo yatakayodumu kwa muda wa miaka mitatu ,kuanzia mwaka huu wa 2021.

Ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa STAMICO pamoja na mambo mengine linatambua dhamana waliyonayo katika kusimamia na kuwaendeleza wachimbaji wadogo wa madini na jambo la kufurahisha eneo hilo limeendelea kupewa kipaumbele na ndilo linaongoza kwa utolewaji wa leseni za uchimbaji ambazo ni 34000.

Akizungumza kwa niaba ya Benki ya KCB , Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kiislamu Amour Muro amefafanua kuwa wanajisikia fahari kuingia makubaliano hayo yenye lengo la kuwawezesha wachimbaji wadogo katika kuwapa mikopo ya fedha na kwamba benki hiyo imekuwa ikitoa huduma ya mikopo isiyokuwa na riba, wachimbaji wadogo wanakaribishwa kupata mikopo hiyo hata kwa wale ambao sio Waislamu.

"Mpaka sasa Benki yetu tayari imeshatoa mikopo yenye thamani ya Shilingi Bilioni 4 kwa wateja wetu wote na sasa tupo tayari kuwafikia wachimbaji wadogo kwa kuwakopesa ili waweze kufanya shughuli zao,,"amesem Amour na kuongeza kuwa benki hiyo itatoa mikopo ya fedha kadri ya uhitaji wa wachimbaji wadogo huku akieleza benki hiyo hadi sasa imeshatoa mkopo wa Sh.bilioni nne na itaendelea kutenga fedha.

Wanasheria kutoka STAMICO na Benki ya KCB, Robert Ambrozi (wa kwanza kulia) na Antonia Kilama (wa kwanza kushoto) wakishuhudia makabidhiano ya hati za makubaliano kwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Vennance Mwasse (wa pili kulia) na Mwakilishi wa Benki ya KCB, Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kiislamu wa Benki hiyo (Islamic Banking) Amour Muro (wa pili kushoto) mara baada ya kumalizika zoezi la utiaji saini wa hati hizo katika Ofisi za STAMICO Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Vennance Mwasse (kulia) na Mwakilishi wa Benki ya KCB ambaye ni  Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kiislamu wa Benki hiyo (Islamic Banking) Amour Muro (kushoto) wakitia saini hati za makubaliano makubaliano ya mashirikano katika kutoa mikopo kwa wachimbaji wadogo Jijini Dar es Salaam.
Mwanasheria wa Benki ya KCB Antonia Kilama (kushoto) akikamilisha utiaji saini kwenye hafla hiyo fupi ya makubaliano hayo yaliyofanyika kwenye Ofisi za STAMICO Jijini dar es Salaam (kulia) ni Mwanasheria wa STAMICO Robert Ambrozi akishuhudia tukio hilo.

Maofisa wa STAMICO na  Benki ya KCB  wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa utiaji saini makubaliano hayo.

No comments :

Post a Comment