Wednesday, September 1, 2021

Waziri Mkuu Aipongeza Mwanga Hakika Kwa Mafaniko Makubwa Ndani Ya Mwaka Mmoja.

Waziri Mkuu wa Tanzania, Mh.Kassim Majaliwa akikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa tawi la Mwanga Hakika microfinance Bank (MHB) lililopo Dodoma eneo la Kisumo plaza.Kushoto ni Naibu Spika wa Bunge, Dk.Tulia Ackson na kulia kwake ni mwenyekiti wa Bodi ya Mwanga Hakika Mhandisi Ridhuan Mringo na Naibu Gavana wa Benki Kuu (BoT) Dk.Bernad Kibesse.

Waziri Mkuu wa Tanzania, Mh.Kassim Majaliwa akizungumza wakati wa uzinduzi wa tawi jipya la saba la Benki ya Mwanga Hakika Microfinance Bank lililopo Dodoma.Kulia ni Waziri wa Kilimo Profesa Adolf Mkenda na Naibu Spika Dk.Tulia Ackson.Tawi hilo liliopo katika eneo la Kisumo Plaza litaweza kuhudumia wateja zaidi ya 100 kwa siku.

Waziri Mkuu wa Tanzania,Mh.Kassim Majaliwa amepongeza mafanikio makubwa yaliyofikiwa na benki ya Mwanga Hakika Microfinance Bank katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake ikiwamo kufungua tawi jipya la saba mkoani Dodoma.

 Katika jitihada za kuendeleza huduma kwa wateja Mwanga Hakika Microfinance Bank Limited [MHB] imefungua rasmi tawi lake la saba mkoani Dodoma, ikiwa ni jithada za kuhakikisha huduma za benki zinawafikia Watanzania wengi.

 Benki hiyo kwasasa imefikisha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake mwenzi Agosti 2020 baada ya muunganiko imara wa benki tatu zikiwa ni EFC Tanzania Microfinance Bank (EFC), Hakika Microfinance Bank (Hakika) na Mwanga Community Bank (MCB) zikiwa na mtaji wa kiasi cha shilingi Billion 40 ambao sasa umekuwa na kufikia kiasi cha Shillingi za Kitanzania Billion 78.

 Akizindua tawi hilo, Waziri Mkuu alisema Serikali imefurahishwa na hatua kubwa ambayo benki hiyo licha ya uchanga wake imeweza kuzifikia ikiwamo kuongeza mtaji hadi kufikia mtaji wa Shilingi 78 bilioni pamoja na kutengeneza faida ya takribani Sh90 bilioni.

 “Mwaka mmoja ni kipindi kifupi kwa kuuiwezesha benki hii kukua kwa kiwango hiki lakini hata kutanua wigo wa matawi kufikia saba, jambo hili linahitaji kupongezwa,” alisema

 “Niungane nanyi kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuendana na matakwa ya sasa ya matumizi ya TEHAMA ikiwa tuna lengo la kuboresha utoaji wa huduma na kufanya kuwa bora zaidi na zenye tija lakini pia zenye gharama nafuu,” alisema.

 Alisema hatua nyingine ni ukuaji wa mtaji ambao unaipa sifa ya benki hiyo kuwa benki kamili ya kibiashara akisema hatua hiyo itasaidia sana katika kufikia malengo ya mwaka 2025 ya kutoka kwenye uchumi wa kati wa chini kwenda uchumi wa kati ulio juu.

 Tawi hilo jipya lipo jengo la Kisumo Plaza jirani na Chako ni Chako. Aidha, tunategemea tawi la Dodoma kuhudumia takribani zaidi ya wateja 100 kwa siku.  

Akiongea  wakati wa uzinduzi, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Eng. Ridhuan Mringo alisema kuwa ufunguzi wa tawi la Dodoma ni sehemu ya mkakati wa kuwafikia Watanzania wengi, ili kuwapa huduma za kibenki kwa njia ya mtandao na kuweza kuwapatia suluhisho la shughuli za kiuchumi.

 “Kufungua tawi katika mji wa Dodoma ni fursa ya kipekee kwa banki yeyote ikiwemo Mwanga Hakika Banki. Kwa kuwa biashara zimeongezeka katika mji wa Dodoma hivyo MHB imejiweka katika kuhakikisha inawekeza katika fursa hii ya kiuchumi baada ya Serikali kuhamia rasmi Dodoma. Kwasasa kumekuwepo na miradi mingi inayoendelea (miradi ya keserikali na ya sekta Binafsi) hapa Dodoma na hivyo MHB inakusudia  kuiunga mkono”, alisema

 Hivi karibuni Benki Kuu ya Tanzania katika kuhakikisha uchumi unakuwa,  imetoa kiasi cha Shilingi Trilioni Moja kwa mabenki ili kuhakikisha  sekta za kifedha zinaendelea kutoa huduma za mikopo kwa riba nafuu.

  “Kwasasa Benki ya MHB ina mikopo inayofikia Billioni 40 na mpaka kufikia mwisho wa mwaka zitakuwa zimefikia Billioni 50. Hapa inaonyesha jinsi ambavyo MHB inachangia uwezeshaji katika sekta binafsi kifedha na wakati huohuo  kuchangia kuongeza kodi kwa maendeleo ya nchi yetu”, alisema Mhandisi Mringo.

Naibu Gavana wa Benki Kuu (BoT) Dk.Bernad Kibesse alisema ufunguzi wa tawi ni muendelezo wa azma ya BoT ya kuhakikisha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa watu wengi zaidi ‘Financial Inclusion’.

 “Hili ni jambo zuri kwa uchumi wetu hivyo kwa kushirikiana na benki za biashara na wawekezaji mbalimbali tutaendelea kuhakikisha asilimia kubwa ya watanzania wanafikiwa na huduma hizi za kifedha,” alisema.

No comments :

Post a Comment