Thursday, July 1, 2021

SBL yamwaga sh. Bilioni 2 kwa mabaa kupambana na Corona

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bia ya Serengeti Mark Ocitti (kulia) akifurahia jambo na baadhi ya wafanyakazi wa kampuni hiyo muda mfupi kabla ya uzinduzi wa programu ya Raise the Bar au Tunyanyuke Pamoja uliofanyika jijini Dar es Salaam.


Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bia ya Serengeti Mark Ocitti akizungumza wakati wa zinduzi wa kampeni ya Raise the Bar au Tunyanyuke Pamoja uliofanyika jijini Dar es Salaam. Kampeni hiyo inalenga kuyasaidia mabaa zaidi ya 2,000 katika mikoa ya Dar, Arusha Mwanza na Zanzibar.


Wafanyakazi wa Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) wakiwa katika picha ya pamoja muda mfupi baada ya uzinduzi wa zinduzi wa kampeni ya Raise the Bar au Tunyanyuke Pamoja uliofanyika jijini Dar es Salaam. Kampeni hiyo inalenga kuyasaidia mabaa zaidi ya 2,000 katika mikoa ya Dar, Arusha Mwanza na Zanzibar.

 Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) leo imetangaza mpango maalum wa

kuyasaidia mabaa kupambana na magonjwa ya kuambikiza ukiwamo ugonjwa wa Corona wenye thamani ya shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya kulinda afya za wateja pamoja na wahudumu


Msaada huu wa SBL unakuja wakati dunia ikikumbwa na wimbi la tatu la ugonjwa wa Corona huku nchi mbalimbali zikipambana kuwakinga raia wake ili kuhakikisha shughuli za kiuchumi zinaendelea kama kawaida.

Programu hii inayojulikana kama “Raise the Bar” au “Tunyanyuke Pamoja”, itadumu kwa kipindi cha miaka miwili kuanzia Julai 2021 na mabaa yatapata misaada ya vifaa na mafunzo baada ya kujiandikisha na kukidhi vigezo maalumu kupitia tovuti ya www.diageobaracademy.com.

Kwa mujibu wa mkurugenzi mtendaji wa SBL Mark Ocitti, mpango huu wa SBL ni mchango wa kampuni hiyo katika kuunga mkono jitihada za serikali kuwahamasisha watu na biashara kuweka mazingira safi ili kujikinga na magonjwa ya kuambukiza ikiwamo ugonjwa wa Corona.

“Katika programu hii, tutayasaidia mabaa kuwa na mazingira safi na salama ili kuweza kuwalinda wateja wanaopata huduma ya chakula na vinywaji dhidi ya magonjwa mbalimbali kiwamo ugonjwa wa Corona. Lengo letu ni kuyafanya yanyanyuke tena. Programu hii itayanufaisha mabaa zaidi ya 2,000 katika mikoa ya Dar Es Salaam, Mwanza, Arusha pamoja na Zanzibar,” alieleza wakati wa uzinduzi.

Programu hii ni sehemu ya kampeni ya kidunia inayofadhiliwa na kampuni mama ya Serengeti, Diageo unaolenga kusaidia mabaa kupambana na ugonjwa wa UVIKO19. Miji mingine inayonufaika na mradi ni amoja na Nairobi, Kampala, New York, London, Edinburgh, Dublin, Belfast, Mexico City, Sao Paulo, Shanghai, Delhi, Mumbai, Bangalore, Sydney.

Kwa mujibu wa Diageo, programu ya“Raise the Bar” au “Tunyanyuke Pamoja” ilibuniwa baada ya utafiti uliofanywa kwa wenye mabaa wakitafuta namna ya kuyasaidia kurudi kwenye biashara wakati wa kipindi cha Corona. Vipaumbele vilivyobainishwa ni pamoja na masuala ya usafi wa mazingira, misaada ya namna ya kufanya biashara kwa kuchukua tahadhari na vifaa vitakavyosaidia kujikinga.

“Raise the Bar au Tunyanyuke Pamoja, itayasaidia mabaa kwa kuyapatia wafanyakazi wake uwezo zaidi wa kujikinga na magonjwa ya kuambukza ikiwamo Corona na pia itatoa vifaa mbali mbali kama meza, viti, vitakasa mikono na vifaa vingine kulingana na mazingira ya baa husika. Lengo ni kuwahakikishia wateja usalama wa afya zao pindi wanapofika kupata huduma ya vinywaji au chakula,”alisema Ocitti.

Programu hii ipo wazi kwa mabaa yote, makubwa na madogo yaliyosajiliwa na ambayo yana leseni ya kuuza pombe katika mikoa ya Dar Es Salaam, Mwanza, Arusha na Zanzibar. Ili baa iweze kufikiriwa kupata msaada chini ya programu hii, ni lazima iwe ikifanya biashara walau mwaka mmoja kabla ya Corona kuingia hapa nchini.

Dirisha la maombi tayari limeshafunguliwa mabaa ili muweze kupata msaada, yanatakiwa kutembelea tovuti ya Diageo Bar Academy www.diageobaracademy.com na kujisajili. Wawakilishi was SBL watakuwa wakipita katika mabaa kwa ajili ya kuwaelekeza na kuwasaidia kuzisajili baa zenu.

“Serengeti ikiwa kama mdau wa baishara hapa nchini inapenda kuyasistiza mabaa yote yenye sifa katika mikoa niliyoitaja kuchangamkia fursa hii,” alisema.

No comments :

Post a Comment