Friday, May 7, 2021

MSIGWA: HAKUNA MFUNGWA WA KISIASA TANZANIA

Msemaji Mkuu wa Serikali Ndugu Gerson Msigwa amesema hakuna tamko lolote lililotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kuhusu kuwaachia huru wafungwa wa kisiasa na kwamba Tanzania haina wafungwa wa aina hiyo.

Amesema zipo taarifa zinazoenea kwenye mitandao ya kijamii na zingine kuandikwa kwenye chombo cha habari cha nchi jirani kuwa Rais Samia Suluhu Hassan amewaachia huru wafungwa 12 wa kisiasa suala ambalo Msigwa amesema si kweli na kwamba Serikali inaandaa mpango wa kukichukulia hatua za kisheria chombo hicho.

"Ndugu zangu Watanzania, kuna taarifa zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii,na kuna chombo cha habari cha nchi jirani kimeziandika, kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amewaachia huru wafungwa 12 wa kisiasa Nchini, kwanza naomba muelewe kuwa hakuna mfungwa wa kisiasa Tanzania, puuzeni uzushi huo, pili tumewasiliana na ubalozi wetu wa Kenya ili kuangalia namna ya kuwachukulia hatua za kisheria" amesema Msigwa.

Aidha amevitaka vyombo vya habari vya nchini na nchi zingine, kutoa habari za ukweli kwa kuwasiliana na Serikali pindi wanapotaka kutoa taarifa zozote zinazohusu Tanzania, na sio kuzusha mambo ambayo hayana tija.

 

No comments :

Post a Comment