Sunday, April 11, 2021

WAZIRI UMMY AWATAKA WATUMISHI WA WIZARA YAKE KUFANYA KAZI KWA WELEDI NA UBUNIFU ILI KUKAMILISHA MALENGO WALIOJIWEKEA

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Ummy Mwalimu,akizungumza na watumishi wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe,akizungumza  wakati wa Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo jijini Dodoma.

Baadhi ya waandishi wa habari pamoja na washiriki wa kikao hicho wakifatilia Hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Ummy Mwalimu,alipokuwa akifungua  Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo jijini Dodoma.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Ummy Mwalimu,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo jijini Dodoma.

…………………………………………………………………………………………..

Na.Alex Sonna,Dodoma

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Ummy Mwalimu,amewataka watumishi wake wote nchini kuzingatia nidhamu, ubunifu, maadili na

weledi katika kazi zao ili kukamilisha malengo waliyojiwekea.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo,Mhe.Ummy amesema kuwa katika utekelezaji wa majukumu yao ni muhimu kuhakikisha linakuwa na uwiano kati ya tija na maslahi.

Waziri Ummy amesema kuwa ili tuweze kufikia malengo tuliyojiwekea ni lazima tufanye  kazi kwa tija,ufanisi,umoja,mshikamano na uwajibikaji,ili kutimiza wajibu wao katika nafasi walizonazo bila ya kujali cheo wala daraja na kuzingatia maadili,weledi na ubunifu katika kazi.

“Ili kupata matokeo mema ni vyema tukaweka uwiano kati ya tija na maslahi na tukumbuke utendaji bora wa kazi unaongeza tija, na ili tufanikiwe ni lazima tujitathimini, umekuja kazini asubuhi na jioni unaondoka jiulize kwa siku husika umefanya nini,”amesema.

Waziri Ummy amesema kuwa mabaraza ya wafanyakazi yapo kisheria hivyo yatumike katika kujadili kwa kina mambo yote waliyopanga ili tija iliyo kusudiwa ipatikane.

“Sote tunatambua kuwa Mabaraza ya Wafanyakazi ni Vyombo vya Kisheria vilivyoundwa chini ya Sheria ya Mashauriano katika Utumishi wa Umma ya Mwaka 2003 Kifungu cha 30(3) (The Public Service Negotiating Machinery, Act 2003) kwa lengo la kuongeza tija na uwajibikaji mahali pa kazi”.

Aidha Ummy ametoa maagizo kwa  Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ,kusimamia masuala ya mapato kwenye halmashauri huku akisema zilizopata hati safi baadhi zimefichwa na ubadhirifu na ufisadi wa fedha za umma.

“TUnapaswa kusimamia  mapato na matumizi, kusimamia masuala ya mgawanyo wa fedha za maendeleo,”amesisitiza.

 Awali Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe,amesema kuwa baraza hilo linalenga kuongeza tija na uwajibikaji mahala pa kazi na limekutana kwa ajili ya kujadili na kupitisha bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka 2020/21.

“Baraza la Wafanyakazi linaongeza ushiriki wa Wafanyakazi katika uendeshaji wa shughuli za Taasisi yao kama ilivyofafanuliwa katika Sheria ya Majadiliano ya Pamoja katika Utumishi wa Umma Sura 105” amesema Prof. Shemdoe.

 

No comments :

Post a Comment