Tuesday, October 13, 2020

NAIBU KAMISHNA WA UHIFADHI (UTALII NA HUDUMA ZA BIASHARA ) ATEMBELEA VITUO VINAVYOSIMAMIWA NA TAWA MKOANI TABORA


…………………………………………………………….

NA FARIDA SAIDY.

Naibu Kamishna Bw.Imani Nkuwi amefanya ziara ya kikazi katika vituo vilivyo chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) vilivyopo Mkoani Tabora na

kuzungumza na watumishi wa vituo vya Kanda Dhidi ya Ujangili ya Magharibi (KDU), Pori la Akiba la Ugalla, Pori la Akiba Luganzo Tongwe, na  Pori la Akiba Wembere

Ziara  hiyo iliyofanyika tarehe 12.10.2020 pamoja na mambo mengine Naibu Kamishna Nkuwi alitoa ufafanuzi kwa watumishi hao kuhusu mabadiliko mbalimbali yaliyofanywa na Serikali katika Shirika pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakibili watumishi kwenye vituo vyao.

Aidha, alitumia vikao hivyo kuwahimiza watumishi kufanya kazi kwa uzalendo, ueledi na kudumisha upendo miongoni mwao ili kuiwezesha TAWA kufikia malengo yake,huku akisisitiza kuzingatia Tunu za TAWA zilizoanishwa katika mpango kazi wao.

Naibu Kamishna Nkuwi alitoa ufafanuzi kwa watumishi kuhusu mabadiliko mbalimbali yaliyofanywa na Serikali katika Taasisi za Uhifadhi zilizopo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa lengo la kuboresha utendaji.

Ambapo moja ya  mabadiliko ni  Kifungu cha 10 cha Sheria Uhifadhi wa Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009 kupitia Sheria za marekebisho mbalimbali Na. 02 ya mwaka 2020 ambayo imeanzisha rasmi Jeshi la Uhifadhi wa Wanyamapori na Misitu (Wildlife and Forest Conservation Service – WFCS).

Kufuatia mabadiliko hayo, Wizara kwa kushirikiana na Taasisi za uhifadhi inaandaa kanuni na miongozo za kutekeleza Sheria ya Jeshi la Uhifadhi. Hivyo, aliwataka watumishi kubadilika kutoka mfumo wa kiraia na kuishi kwa kufuata taratibu za kijeshi. 

Pia Sheria imetoa baadhi ya mamlaka kwa watumishi ikiwepo ya kukamata, kupeleleza, kufanya shughuli za intelijensia na kushughulikia mashauri yanayohusisha mifugo kwa njia ya compound.

Kwa upande wao Watumishi walimweleza Naibu Kamishna Nkuwi kuhusu changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo kwenye vituo vyao vya kazi ambazo nyingi alizitolea ufafanuzi na maelekezo namna ya kuzitatua ikiwa ni pamoja na kuandaa mapendekezo,

Aidha akijibu changamoto za watumishi aliwaasa kujiepusha na kushawishika kupokea rushwa katika utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha haki na sheria inafuatwa hasa wanapokamata majangili na Mifugo ndani ya hifadhi zetu tunazosimamia.

Mwisho aliwapongeza watumishi hao kwa kazi nzuri na ya kizalendo wanaoyoifanya ya kusimamia raslimali ya wanyamapori kwa uaminifu kwa niaba ya watanzania.

 

No comments :

Post a Comment