Wednesday, October 7, 2020

BILIONEA LAIZER AFANYA MAOMBI KULAANI MAUAJI YA MLINZI WAKE








Bilionea i Saniniu Laizer akiwa katika maombi maalumu
katika eneo la mgodi wake uliopo Mererani mkoani Manyara, sehemu
ambayo mlinzi wake Manase Wiliam (47)aliuwawa kikatili hivi karibuni
maombi. Hayo ni ya kulaani kitendo hicho na kutaka aliyehusika
apatikane.

mchungaji Joshua Laizer akifanya maombi katika mgodi wa bilionea
Saniniu ambapo ameeleza kuwa tukio hilo ni baya na linapaswa
kulaaniwa na kila mtu na kumwomba Mungu awaonyeshe waliotenda uhalifu
huo wa kinyama ndani ya siku saba ili sheria iweze kuchukua mkondo
wake (picha na Woinde Shizza, Mereran.i)



Na Woinde Shizza, Michuzi Tv -Arusha

SIKU chache  baada ya kutokea tukio la kifo cha kutatanisha kwa
mlinzi wa mgodi wa bilionea Saniniu Laizer anayefahamika kwa jina la Manase William(47) kuuawa na watu wasiojulikana, bilionea huyo amefanya maombi maalumu katika eneo la tukio na kulaani kitendo hicho na kutaka aliyehusika apatikane.

Maombi hayo ya aina yake yamefanyika mapema Leo katika Mgodi wa Laizer
uliopo Mererani, Mkoani Manyara, kwa kuwahusisha wafanyakazi wote wa
mgodini hapo pamoja ambapo Laizer ameshika udongo kutoka eneo ambao mlinzi huyo alikutwa ameuawa .

"Nimeamua kufanya maombi haya na wafanyakazi wangu ili kama kuna
waliohusika wapo hapa waweze kuumbuliwa mapema na serikali iweze
kuchukua hatua mapema." amesema Laizer.

Laizer alisema ameumizwa sana na tukio hilo ambalo halikuwahi kutokea
katika mgodi wake, Ni tukio la kwanza ndio maana ameamua kufanya maombi
hayo ya kulaani tukio hilo lisijirudie tena na kama kuna mfanyakazi
wake alihusika, Mungu atamfichua.

" Marehemu ameajiriwa na ni mdhamini wa mgodi wangu.... hana muda
mrefu tangu aanze kufanyakazi na alikuwa kijana mwema hana makuu na
mtu yoyote ila mimi naamini aliyehusika si mtu wa hapa ndani atakuwa
ametoka nje na eneo langu la mgodi"amesema Laizer.

Aidha Laizer ameongeza kuwa yeye anamwamini Mungu na mali anayoipata
inatokana na maombi ya imani yake hivyo anaamini kwa kupitia maombi
hayo mhusika wa tukio hilo atapatikana kwa kuwa anamwamini Mungu.

Akiongoza ibada hiyo mchungaji Joshua Laizer alieleza kuwa tukio hilo
ni baya na linapaswa kulaaniwa na kila mtu na kumwomba Mungu
awaonyeshe waliotenda uhalifu huo wa kinyama ndani ya siku saba ili
sheria iweze kuchukua mkondo wake.

"Damu ya Manase inalia hapa ardhini, tutashika udongo huu mahala damu
yake ilipomwagika sisi hatumjui aliyemuua tunamwomba mungu atuonyeshe
ndani ya siku saba" amesema mchungaji Joshua.

Akinukuu maandiko matakatifu ya bibilia, amesema kumbukumbu la Torati
la 27 mstari 24 na 25 na 'alaaniwe mtu yoyote ampigaye mwenzake kwa
siri na alaaniwe yoyote atakayemuua mwenzake pasipo na kosa '.


Marehemu Manase anadaiwa kuuawa na watu wasiojulikana septemba 27
mwaka huu katika mgodi wa laizer na mwili wake kukutwa eneo la tukio
na Marehemu atazikwa siku ya Jumamosi oktoba 10 mwaka huu kijijini
kwao Ilkiding'a wilayani Arumeru.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Manyara, Paul Kasabago alisema hadi sasa
jeshi hilo linawashikilia watu saba wakiwemo wafanyakazi wa Laizer
wakihusishwa na tukio hilo.


 

No comments :

Post a Comment