Sunday, September 20, 2020

TANESCO YABORESHA HALI YA UMEME URU KILIMANJARO

**************************************

Shirika la umeme Tanzania (TANESCO) limeendelea na uboreshaji hali ya upatikanaji wa umeme (voltage improvement) maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Kata ya Uru Mashariki mkoani Kilimanjaro.

Bw. Emmanuel Msafiri ambaye ni msimamizi wa Kitengo cha Ujenzi TANESCO Mkoa wa

Kilimanjaro, alisema kuwa Shirika limejenga njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovolti 11 yenye urefu wa kilometa 1.5 pamoja na kuongeza mashine umba moja kubwa ili kusaidia kuimarisha hali ya upatikanaji umeme katika Kata ya Uru Mashariki.

Mradi huo wa kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Kata ya Uru umetekelezwa na TANESCO kwa kutumia wataalamu wake wa ndani.

Aidha, kuimarika kwa umeme kwenye Kata ya Uru Mashariki kumesaidia kuboresha huduma katika kituo cha Afya Kyaseni ambapo kwa sasa kina hudumia takribani wagonjwa elfu kumi na tatu kwa mwaka.

Msaidizi wa Mganga Mfawidhi, katika kituo cha Afya Kyaseni Dkt. Emmanuel Makundi ameishukuru TANESCO kwa kuboresha hali ya upatikana umeme.

“Kuboreka huku kwa huduma ya umeme kumesaidia kuboresha huduma katika kituo chetu cha Afya, sasa tanauweza wakufanya upasuaji mbalimbali kwa sababu kuna umeme wa uhakika unaoweza kuwasha mashine mbalimbali ambapo awali ilikua haiwezekani” alisema Dkt. Makundi.

Mhudumu wa Afya, Matron Temba aliongeza kuwa, huduma ya umeme imewasaidia katika kuboresha huduma kwenye kituo hicho cha Afya kwani awali walikua wana wazalisha wakina mama kwa kutumia taa za chemli, kitu ambacho kilikua ni cha hatari.

Nao Wananchi wa Kata ya Uru Mashariki wametoa pongezi kwa Serikali kupitia TANESCO kwa kuboresha hali ya upatikanaji umeme katika kata hiyo.

 

No comments :

Post a Comment