Ni baada ya kupata jiwe jingine kubwa lenye uzito wa zaidi ya kilo 6
KWA
mara nyingine tena Bilionea Saniniu Laizer ameifanya Serikali kufika
Mirerani mkoani Manyara yaliko machimbo ya madini ya Tanzanite katika
hafla ya kukabidhi jiwe lingine la Tanzanite lenye uzito wa kilo 6.3317
lililopatikana katikati ya mwezi Juni katika mgodi wake uliopo katika
kitalu D ndani ya ukuta unaozunguka machimbo hayo katika eneo la
Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.
Jiwe
hili ni la tatu kupatikana na kuuzwa Serikalini baada ya mawe mengine
mawili kununuliwa na Serikali katika hafla iliyofanyika tarehe 24 Juni,
2020 mara baada ya mchimbaji huyo kuiarifu Serikali juu ya uwepo wa mawe
mawili yenye uzito mkubwa yaliyochimbwa mgodini kwake mnamo tarehe 17
Juni, 2020 yaliyokuwa na thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 7.
Imeelezwa
kwamba ndani ya muda mfupi baada ya Serikali kununua madini hayo kutoka
kwa mchimbaji huyo mdogo, mchimbaji huyo alitoa taarifa ya kupatikana
kwa jiwe jingine ambapo Serikali imeridhia kununua jiwe hilo na kuifanya
Serikali kuwa na mawe matatu ya tanzanite yenye uzito mkubwa kwa uzito
wa kufuatana ambapo zito zaidi lina kilo 9.27, kilo 6.33 na kilo 5.103.
Akizungumza
katika hafla iliyofanyika leo tarehe 03 Agosti, 2020, Waziri wa Madini,
Doto Biteko amewataka wachimbaji wadogo wa madini kuacha tabia ya
kutorosha madini na kueleza kuwa tabia hiyo haina faida yeyote kwao na
zaidi itawasababishia hasara kubwa na kupelekea kukamatwa na
kushughulikiwa na vyombo vya dola.
Waziri
Biteko aliendelea kubainisha kuwa, mnamo tarehe 17 Juni 2020 mgodi wa
bilionea Laizer ulizalisha kilo 32.872 za Tanzanite katika umbali wa
mita 1800 chini ya ardhi kwenye mgodi wake uliopo kitalu D uliokuwa na
thamani ya shilingi bilioni 8.4 ambapo malipo ya mrabaha na ada ya
ukaguzi yalikuwa ni shilingi milioni 507.5.
Akiendelea
kuchambua uzalishaji huo, Waziri Biteko alisema ndani ya kilo hizo 32
ndipo yalipopatikana mawe mawili yaliyokuwa na uzito mkubwa ambao
haujawahi kushuhudiwa katika historia ya nchi ambapo kipande kimoja
kilikuwa na uzito wa kilo 9.27 na kingine kikiwa na uzito wa kilo 5.103.
"Mnamo
tarehe 29 Juni, 2020, Serikali iliarifiwa juu ya kupatikana kwa kipande
kingine cha tanzanite chenye uzito wa kilo 6.33 kilichopatikana wakati
wa zoezi la kusafisha eneo la uzalishaji wa awali yaani ule wa tarehe 17
Juni, 2020 ambapo wachimbaji walikuwa na zoezi la kuondoa miamba
iliyokuwa ikikaribia kuanguka ili kuruhusu zoezi la uchorongaji na
ulipuaji mwingine kuendelea," Biteko alifafanua.
Biteko
alieleza kuwa, kwa mara nyingine Serikali imeridhia kununua kipande
hicho kwa gharama ya shilingi 4,846,537,271.12 kufuatia uthaminishaji
uliofanywa na wataalamu wa uthaminishaji madini ambapo shilingi
290,792,236.28 zimelipwa kama mrabaha na shilingi 48,465,372.71
zimelipwa kama ada ya ukaguzi.
Akizungumzia
faida za ukuta unaozunguka machimbo ya madini hayo ya Tanzanite, Waziri
Biteko alisema taifa limeshuhudia kuongezeka kwa maduhuli ambapo ndani
ya miaka miwili baada ya kujengwa kwa ukuta huo kiasi cha kilo 3,935.43
za tanzanite zenye thamani ya shilingi bilioni 53.141 zilizalishwa na
Wizara kukusanya mrabaha wa shilingi bilioni 3.9.
Biteko
aliendelea kusema kuwa Serikali imeridhia kununua kipande hicho kwa
gharama ya shilingi bilioni 4.8 kufuatia uthaminishaji uliofanywa na
wataalamu wa madini ambapo shilingi 290,792,236.28 imelipwa kama mrabaha
na shilingi 48,465,372.71 imelipwa kama ada ya ukaguzi.
Akizungumzia
kuhusu eneo la kitalu C, Waziri Biteko aliwataka wananchi wa Simanjiro
na Tanzania kwa ujumla kutokuvamia eneo hilo kwani Serikali ina taratibu
inazozifanya na zitakapokamilika taarifa itatolewa ili kuruhusu
shughuli kufanyika sawasawa na maamuzi yatakayofanyika.
Aidha, aliuhakikishia umma kuwa kamwe eneo hilo halitatolewa kwa wageni ili liweze kunufaisha wazawa na taifa kwa ujumla.
Kwa
upande wake, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango alisema kuwa
Sekta ya Madini ni muhimu kwa uchumi wa nchi na kukiri kutambua kazi
nzuri zinazofanywa na wachimbaji wa madini katika kukuza uchumi wa nchi.
“Baada ya ujenzi wa ukuta mapato yatokanayo na uchimbaji wa Tanzanite yameongezeka mara nne,” Waziri Mpango alisema.
Aidha,
Waziri Mpango ameipongeza kazi kubwa inayofanywa na Rais John Magufuli
kwa usimamizi madhubuti wa Sekta ya Madini na kuahidi kuendelea
kumwombea baraka za Mungu kwa mambo mazuri anayoifanyia nchi na wananchi
wake.
Kwa
upande wake, Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo amempongeza, Rais
Magufuli kwa namna anavyoisimamia sekta kwa kutoa maelekezo
yanayopelekea mafanikio mazuri yanayoonekana kwenye sekta.
Pamoja
na hayo Naibu Waziri Nyongo amempongeza mchimbaji Laizer kwa kupata
jiwe jingine na kuwaahidi wachimbaji wadogo kuwa serikali yao itawapa
ushirikiano wa kutosha kuhakikisha wananufaika na rasilimali madini
zilizopo nchini.
No comments :
Post a Comment