********************************
NA MWANDISHI WETU
CHAMA cha Wafanyakazi
wa Vyombo vya Habari Tanzania(JOWUTA) kimesisitiza umuhimu wa waandishi
wa habari nchini kuendelea kuzingatia maadili, kanuni na sheria katika
utekelezaji wa majukumu yao katika kipindi hiki cha mapambano dhidi ya
janga la ugonjwa wa homa kali ya mapafu COVID19.
Akitoa salamu za
maadhimisho ya siku ya Uhuru wa Habari Duniani leo, Mwenyekiti wa
JOWUTA, Claud Gwandu alisema uhuru wa habari, maadili, haki, usawa ni
nguzo muhimu za kuzingatiwa na wanahabari nchini katika kipindi hiki
kigumu ambapo dunia nzima inapambana na COVID-19.
“Tunapotekeleza
majukumu yetu muhimu ya kuhabarisha, kuelimisha na kuburudisha,
tunapaswa kuchukua tahadhari zote za kiusalama kwa kuepuka mikusanyiko
isiyo ya lazima, kuvaa vifaa kinga kama barakoa na kufuata maelekezo ya
wataalam wa afya ili kuepuka kupata maambukizi ya virusi vya corona.
Alisema JOWUTA
inaunga mkono kauli mbiu ya Siku ya Uhuru wa Habari 2020 ambayo
inasitiza waandishi kufanya kazi bila hofu ua upendeleo ili kuonesha
umuhimu wa uhuru wa vyombo vya habari hasa kipindi hiki cha maambukizi
ya virusi vya corona vinavyosababisha ugonjwa wa COVID-19.
Gwandu aliwataka
waandishi kuadhimisha siku hii kwa kukumbushana kusimamia maadili ya
uandishi wa habari kwa kuwa wao ni kioo cha jamii.
“Tunaadhimisha siku
ya uhuru wetu huku duniani ikipitia wakati mgumu wa mapambano dhidi ya
COVID-19 ni imani yangu kuwa tutasimamia maadili, uadilifu, haki, usawa,
kanuni na sheria zinazosimamia taaluma yetu,” alisema.
Mwenyekiyi huyo
alisema iwapo kundi hili litakuwa na mshikamano na ushirikiano na wadau
wa maendeleo na serikali malengo ya kuifikisha Tanzania ya viwanda na
uchumi wa kati itafanikiwa.
“Nasisitiza umuhimu
wetu kwenye jamii asitokee kati yetu anakubali kutumika kwa maslahi ya
mtu binafsi.Tambua utakuwa umesaliti Watanzania zaidi ya milioni 50,”
alisema.
Gwandu alitumia siku
hiyo kuwahamasisha waandishi wa habari nchini kujiunga na JOWUTA ili kwa
pamoja waweze kupigania haki zao za msingi.
Alisema jukwaa pekee
ambalo waandishi nchini wanaweza kufikisha malalamiko na changamoto zao
ni JOWUTA hivyo hawanabudi kujiunga kwa sasa.
No comments :
Post a Comment