Waziri wa Nishati Dkt Medard
Kalemani (wa tatu kutoka kulia) akisikiliza maelezo ya namna mtambo wa
gesi asilia uliopo eneo la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam unavyofanya kazi
wakati wa hafla ya uzinduzi wa matumizi ya gesi asilia chuoni hapo,
Februari 1, 2020.

Waziri wa Nishati Dkt Medard
Kalemani akikagua migahawa iliyounganishiwa gesi asilia iliyopo Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam pamoja na baadhi ya nyumba zilizounganishiwa
nishati hiyo katika eneo la Mwenge Mlalakuwa, Februari 1, 2020.
………………………………………………………………………………………………
Veronica Simba – Dar es Salaam
Waziri wa Nishati Dkt. Medard
Kalemani amezindua matumizi ya gesi asilia katika Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam (UDSM), leo Februari 1, 2020 ambapo kwa hatua hiyo ya awali,
migahawa minne chuoni hapo imeanza kutumia huduma hiyo.
Akizungumza katika hafla hiyo ya
uzinduzi, Dkt Kalemani amesema dhamira ya serikali ya kutumia gesi
asilia inayopatikana nchini kwa maendeleo ya Taifa iko palepale tofauti
na wanavyoamini baadhi ya watu kuwa nishati hiyo haipewi kipaumbele
katika matumizi yake.
“Gesi hii tutaendelea kuitumia sambamba na matumizi mengine ya nishati ikiwemo kuzalisha umeme ili kujenga uchumi wa viwanda.”
Akifafanua, Waziri amesema
mathalani, takribani asilimia 80 ya gesi inayozalishwa kwa sasa hapa
nchini inatumika kuzalisha umeme na kwamba umeme unaozalishwa na gesi
asilia kwa Tanzania ni asilimia 57 sawa na megawati 892, akibainisha
kuwa huo ni mchango mkubwa sana wa sekta ya nishati kwenye uchumi wa
nchi.
Hata hivyo amesema, pamoja na
kiasi kikubwa cha gesi kutumika kuzalisha umeme, kiasi kingine
kinatumika katika shughuli nyingine mbalimbali ambazo ni pamoja na
kuunganisha viwandani, kwenye makazi ya watu na migahawa kwa ajili ya
kupikia pamoja na kutumika katika magari.
Katika kuweka msisitizo wa
matumizi ya gesi asilia katika magari, Dkt Kalemani ametoa agizo kwa
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati pamoja na watendaji wakuu wa Taasisi
zote zilizo chini yake, kuhakikisha magari yote yanayoagizwa kuanzia
sasa, yawe ni yale yenye mfumo wa kutumia gesi badala ya petroli na
dizeli.
Akizungumzia faida za kutumia gesi
asilia kwa shughuli mbalimbali, amesema ni pamoja na utunzaji wa
mazingira kutokana na uwepo wa kiasi kidogo cha hewa ya ukaa pamoja na
gharama nafuu kwa mtumiaji ambayo inakadiriwa kuokoa asilimia 40
ikilinganishwa na gharama za aina nyingine za nishati.
Kuhusu mipango ya serikali
kusambaza gesi asilia kwa matumizi ya kupikia, Waziri ameeleza kuwa,
mpango huo umeanza kutekelezwa katika mikoa ya Dar es Salaam, Lindi,
Mtwara na Pwani na baadaye mikoa mingine pia itafikiwa.
No comments :
Post a Comment