Sunday, August 4, 2019

TANESCO SIMIYU YASEMA KUNA MWAMKO MKUBWA WA WANANCHI WA MKOA HUO KUTUMIA FURSA ZA UMEME KWA KUPANUA SHUGHULI ZA KILIMO NA VIWANDA


 Meneja wa TANESCO Mkoani Simiyu Bi. Rehema Mashinji (katikati), akitoa elimu ya matumizi bora na sahihi ya umeme kwa wananchi (hawapo pichani) waliotembelea banda la TANESCO kwenye maonesho ya Nanenane viwanja vya Nyakabindi, nje kidoko ya mji wa Bariadi mkoani Simiyu Agosti 4, 2019.
 Wananchi wakielimishwa kuhusu shughuli za TANESCO lakini pia matumizi sahihi na yaliyo bora ya umeme
 Bi. Mashinji (kushoto), akimsikiliza mwananchi huyu aliyekuwa kitaka ufafanuzi kuhusu masuala ya umeme.
 Wananchi wakiwa na vipeperushi vyenye maelezo ya kina kuhusu shughuli za TANESCO lakini pia matumizi bora na sahihi ya umeme.
 Mtaalamu wa TANESCO (kulia), akitoa elimu kwa Mzee Mtaka, baba wa Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka, ambaye alitembelea banda la Shirika hilo kujielimisha kuhusu masuala ya umeme Agosti 4, 2019.


NA K-VIS BLOG/Khalfan Said, Simiyu
SHIRIKA la Umeme Nchini TANESCO mkoani Simiyu, limesema kumekuwepo na mwamko mkubwa wa wananchi wa mkoa huo kutumia umeme kama kichocheo cha upanuzi wa shughhuli zao za kiuchumi.
Meneja wa TANESCO Mkoani Simiyu, Mhandisi, Rehema Mashinji ameyasema hayo leo Agosti 4, 2019  katika maonesho ya Nanenane viwanja vya Nyakabindi mkoani humo  kuwa, kuboreka kwa hali ya umeme kumeleta msukumo mpya ambapo wananchi wameanzisha mashamba makubwa ya umwagiliaji ambapo pampu za kusukuma maji zinatumia umeme.
Alitoa mfano kuwa yupo mwekezaji mmoja mzawa wilayani humo ambaye anaendesha kilimo kikubwa cha umwagiliaji, TANESCO imemuwekea umeme wa kutosha kuhudumia mashamba yake.
“Sisi TANESCO mkoani Simiyu tuko vizuri, tumewezesha wananchi wengi kuanzisha mashamba makubwa ya kilimo cha umwagiliaji huko Busega ambao wanalima mwaka mzima, upande wa ufugaji tumewezesha kuanzishwa kwa viwanda vya kusindika maziwa na kuhusu uvuvi tumepeleka umeme kwenye soko kuu la Ramadi na wananchi wanauza samaki na kufanya kazi masaa 24 kila siku tumewapelekea huduma ya umeme na wameweka taa.” Alifafanua Mhandisi Mashinji.
Alisema Simiyu ni wakulima wakubwa wa pamba, na tayari mkoa unatarajia kuanzisha kiwanda cha kutengeneza vifaa tiba kupitia pamba, na sisi kama Shirika tuko tayari kuwapelekea umeme pindi mipango ya kuanzisha kiwanda hicho itakapokamilika.
“Tunategemea kuanzishwa kwa viwanda vingi Zaidi vya kutengeneza vifaa tiba huko Dutwa hapa Simiyu.” Alifafanua.
Mhandisi Mashinji amemshukuru Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani kwa kutoa punguzo kubwa kwa wananchi ambapo wananachi wakitaka kuunganisha umeme hususan vijijini gharama ni Shilingi elfu 27,000/= tu.
“Wananchi wengi waombe umeme ili tuwaunganishie, na kwabahati nzuri Simiyu umeme umetawanyika kila kona na nia yetu umeme umfikie kila mwananchi hadi wa pembezoni.” Alisisitiza Meneja huyo wa TANESCO mkoani Simiyu.
Aidha alisema, wataalamu wa TANESCO waliopo katika maonesho ya Nanenane hapa Nyakabindi hivi sasa, wanatoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi bora na sahihi ya umeme, lakini pia jinsi ya kutunza miundombinu ya umeme na wawe mabalozi wa Shirika dhidi ya wahalifu wa miundombinu ya umeme kwenye maeneo yao kwa kutoa taarifa pindi wanapohisi kuna uhalifu unataka kufanyika.

No comments :

Post a Comment