Sunday, April 28, 2019

WAZIRI MKUU AWAAGA WATALII 1,000 KUTOKA ISRAEL

PMO_8348
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akisalimiana na Waziri wa Maliasili na Utalii Khamis Kigwangala, wakati akiwasili kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA, kuwasalimia na kuwaaga Watalii kutoka nchini Israel Aprili 27, 2019.
PMO_8368
Wasanii wa kabila la Kimasai, wakitoa burudani kwa Watalii kutoka nchini Israel Aprili 27, 2019, kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA
PMO_8400
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akizungumza na Waziri wa Maliasili na Utalii Khamis Kigwangala, kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA, alipofika kuwasalimia na kuwaaga Watalii kutoka nchini Israel Aprili 27, 2019.
PMO_8415 PMO_8426
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akizungumza na Watalii kutoka nchini Israel, kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA, wakati akiwaaga Aprili 27, 2019
PMO_8422 PMO_8423
Watalii kutoka nchini Israel, wakimsikiliza Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA, kabla ya kuondoka nchini, Aprili 27, 2019.
PMO_8440
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akimvalisha kikoi Mkurugenzi wa Kampuni ya Another World Shlomo Carmel, iliyoleta Watalii 1000 kutoka nchini Israel, kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA Aprili 27, 2019. Kulia ni Waziri wa Maliasili na Utalii Khamis Kigwangala.
PMO_8545
Waziri  Mkuu Kassim Majaliwa, akiagana na watalii kutoka nchini Israel, kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa KIA Aprili 27, 2019. Kulia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Another World Shlomo Carmel. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
…………………..
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka watalii kutoka Israel wakawe mabalozi wazuri
wa kuitangaza Tanzania pindi wakirudi  huko kwao.

Ametoa wito huo leo mchana (Jumamosi, Aprili 27, 2019) kwenye uwanja wa ndege wa Kilimanjaro (KIA) wakati akiwaaga watalii 274 walioondoka nchini leo mchana kurejea kwao.

Watalii hao ni miongoni mwa watalii 1,000 waliowasili nchini tangu Aprili 20, mwaka huu na kutembelea maeneo kadhaa ya vivutio kwenye ukanda wa Kaskazini.

Kundi la kwanza liliondoka jana usiku, la pili leo mchana, la tatu litaondoka leo saa 10 jioni na la mwisho litaondoka leo saa 2 usiku. 

Waziri Mkuu amewaomba watalii hao wapange muda wao na watafute fursa nyingine ya kuja Tanzania kutembelea mbuga nyingine za ukanda wa Kusini pamoja fukwe nzuri za Zanzibar. 

“Tumefarijika sana na ujio wenu na tunaamini mtaenda kutangaza mazuri mliyoyaona kwa wengine. Tunazo mbuga nyingine za Rubondo, Katavi, Ngorongoro, Ruaha, Selous, fukwe nzuri za Zanzibar na mlima Kilimanjaro,” amesema. 

Pia amewashukuru mawakala wa utalii nchini pamoja na Mkurugenzi wa kampuni wakala wa utalii ya Another World kutoka Israel Bw. Carmel Shlomo kwa kuamua kuitangaza Tanzania kama kivutio namba moja cha utalii barani Afrika. 

Kwa upande wake, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla aliwashukuru watalii hao kwa kuamua kuitembelea Tanzania licha ya kuwa wangeweza kwenda maeneo mengine yaliyo jirani na Israel. 

“Natambua uchovu mlionao sababu ya urefu wa safari kutoka Israel hadi hapa, lakini nawashukuru kwa uamuzi wenu wa kuja Tanzania katika kipindi hiki ambacho tunafanya maboresho kwenye sekta ya utalii ili tuweze kutoa huduma bora zaidi,” alisema. 

Alisema Tanzania ina vivutio vingi vya utalii na hii inawezekana kwa sababu iliamua kutenga zaidi ya robo ya ardhi yake kwa ajili ya mbuga na hifadhi za taifa za wanyama.

Pia alizishukuru kampuni za utalii za Tanzania na Israeli kwa kushirikiana kuleta watalii wengi kiasi hicho. Alizitaja kampuni hizo kuwa ni Excellent Guides, Mauly Tours and Safaris, Matembezi, Leopard Tours and Safaris, African Queen Adventures na TAWISA zote za kutoka Tanzania. Kamuni za kutoka Israeli ni Another World, My Trip, Camel na Safari Company.

Kwa upande wao, baadhi ya watalii kutoka Israel wamesema wamevutiwa na waliyaona hapa nchini na wameahidi kurudi tena ili watembelee vivutio vingine zaidi. 

Bibi Naomi Peer Moscovich na mabinti zake Dana na Lihi wamesema wamevutiwa na wingi wa wanyama waliowaona lakini pia wameguswa na ukarimu wa watu waliokutana nao. 

“Tunaondoka na neno moja kubwa nalo ni kwamba hatutaisahau Tanzania (we say Unforgettable Tanzania) na tutarudi tena hivi karibuni,” alisema Dana Peer Moscovich ambaye ni dada yake Lihi. 

Hafla ya kuwaaga watalii hao ilihudhuriwa pia na Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii nchini, Jaji Thomas Mihayo, Katibu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Adolf Mkenda na Wakuu wa Mikoa ya Kilimanjaro na Arusha. Mama Anna Mghwira na Bw. Mrisho Gambo. 

No comments :

Post a Comment