Wednesday, April 24, 2019

CHUO KIKUU MZUMBE CHAJIZATITI KUIMARISHA UTOAJI ELIMU KWA KUTUMIA TEKNOLOJIA WILAYANI MVOMERO


8I9A1609AA
Mgeni rasmi Mkurugenzi wa Wilaya ya Mvomero Bw. Florian Kyombo (mwenye kaunda suti –  kulia), akikabidhi msaada wa vitabu kwa shule ya msingi Mnyanza. Kulia kwake ni Prof. Lughano Kusiluka Makamu Mkuu wa Chuo kikuu Mzumbe (mwenye sare ya kitenge) na kushoto ni Mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Myanza Bw. Robert Ngelima na baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo.
8I9A1523A
Mwanafunzi wa Kidato cha sita Mark Malekela wa shule ya Sekondari Mzumbe, akionyesha moja ya kitabu alichotunga kwenye maadhimisho ya siku ya Vitabu Duniani yaliyofanyika Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi Kuu Morogoro. Maadhimisho hayo yalilenga kuhamasisha usomaji na utunzi wa vitabu Duniani.
8I9A1648AA 8I9A1654AA
Mgeni rasmi Mkurugenzi wa Wilaya ya Mvomero Bw. Florian Kyombo (mwenye kaunda suti –  kushoto), kwa pamoja na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe Pro. Lughano Kusiluka wakikabidhi msaada wa Vitabu kwa shule ya Sekondari ya Mzumbe na Adrian Mkoba zote za Kata ya Mzumbe wakati wa maadhimisho ya siku ya Vitabu Duniani yaliyofanyika Kampasi Kuu Morogoro.
8I9A1692AA 8I9A1711AA
Wakiwa katika picha ya pamoja ni Mgeni rasmi Mkurugenzi wa Wilaya ya Mvomero Bw. Florian Kyombo (mwenye kaunda suti –  katikati), Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe Pro. Lughano Kusiluka (mwenye sare ya kitenge – kulia), Mhe. Rachel Kingu Diwani wa Kata ya Mzumbe (Kushoto), Dkt. Albogast Musabila Mkurugenzi wa Makitaba na huduma za Kiufundi Chuo Kikuu Mzumbe ( mwenye sare ya Kitenge wa kwanza kulia) na Dkt. Hawa Petro Tundui ( wa kwanza kushoto) akimwakilisha Naibu     Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma. Kwa nyuma ni baadhi ya wafanyakazi wa Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi Kuu.
………………………….
Maadhimisho ya siku ya Vitabu Duniani yaliadhimishwa kwa aina yake na Chuo kikuu Mzumbe Aprili 23; 2019 ambapo mbali na maonyesho ya machapisho yaliyoandikwa na
Wanazuoni; Chuo hicho kilikabidhi msaada wa vitabu vya kiada na ziada kwa shule za Msingi na Sekondari zilizopo kwenye Kata hiyo.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvombero Bw. Florian Kyombo ambaye pamoja na mambo mengine alipongeza jitihada zinazofanywa na Chuo Kikuu Mzumbe katika kuchangia na kuboresha sekta ya elimu nchini hususani matumizi ya teknolojia hasa kipindi hiki cha Awamu ya Tano ya Uongozi ambapo elimu ni agenda inayopewa kipaumbele na hivyo kutolewa bila malipo kwa ngazi ya elimu ya Awali, Msingi na Sekondari.
“Ninatoa shukrani zangu za dhati  kwa msaada wa vitabu, shelfu na elimu mnayoendelea kuitoa kwa shule zetu kuhusu matumizi sahihi ya vitabu hivyo, sambamba na matumizi ya teknolojia ya utunzaji. Kwangu hili ni deni kuhakikisha tunatenga bajeti kuwezesha shule zingine za Msingi na Sekondari kwenye Kata 30 zilizopo kwenye Wilaya ya Mvomero zinaiga mfumo huu kwa kuifanya Kata ya Mzumbe kuwa ni ya kujifunzia.” alisisitiza.
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe Prof. Lughano Kusiluka amesema Chuo hicho kina wajibu wa kuhakikisha jamii  inayokizunguka inanufaika na uwepo wake kwa kusaidia katika masuala ya maendeleo ikiwemo kuinua kiwango cha elimu kwa kujenga hamasa ya usomaji wa vitabu, kuwakuwa hiyo ndiyo mbinu pekee inayoweza kuwapatia Wanafunzi  maarifa ya kutosha na kuweza kufikia ngazi zote za elimu hadi Chuo Kikuu.
Amesema “ Mpango wa kuzifikia na kutatua changamoto za Shule za Msingi na Sekondari  kwa jamii inayotuzunguka ni endelevu na ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati  wa nne (IV) wa Chuo Kikuu Mzumbe ambapo kwa awamu hii, tumetoa Vitabu vya kiada na ziada  kwa shule za Msingi Tangeni, Mnyanza,Vikenge, Masanze, Changarawe na Mzumbe na shule tatu za Sekondari  ambazo ni Mongola,Askofu Adrian Mkoba na Mzumbe; na tayari tumetoa msada wa Komputa na kutoa mafunzo ya matumizi ya programu mbalimbali ili kuziwezesha shule zetu kuendeshwa kisasa kwa kutoa mafunzo yanayoendana na wakati tulionao”.
Aidha; ameahidi Chuo Kikuu Mzumbe kuendelea kuwa chachu katika kuhamasisha usomaji na utunzaji vitabu wenye lengo la kurithishana elimu na ujuzi kwa manufaa mapana ya Taifa.
Siku ya Vitabu Duniani huadhimishwa kila mwaka Aprili 23; kwa lengo la kuhamasisha usomaji wa vitabu na kuwaenzi watunzi wa Vitabu duniani kote.

No comments :

Post a Comment