Naibu Waziri, Ofisi ya Rais,
Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary
Mwanjelwa (Mb) akizungumza na watumishi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii
(TASAF) (hawapo pichani) wakati wa ziara yake ya kikazi alipowatembelea
ofisini kwao jijini Dar es Salaam kwa lengo la kuhimiza uwajibikaji.
Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw.
Ladislaus Mwamanga akieleza majukumu ya taasisi yake kwa Naibu Waziri,
Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.
Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) wakati wa kikao kazi cha Naibu Waziri huyo na
watumishi wa TASAF kilichofanyika Makao Makuu ya TASAF jijini Dar es
Salaam chenye lengo la kuhumiza uwajibikaji.
Baadhi ya watumishi wa Mfuko wa
Maendeleo ya Jamii (TASAF) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais,
Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary
Mwanjelwa (Mb) alipowatembelea ofisini kwao jijini Dar es Salaam kwa
lengo la kuhimiza uwajibikaji.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais,
Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary
Mwanjelwa (Mb), akiwa katika picha ya pamoja na menejimenti ya Mfuko wa
Maendeleo ya Jamii (TASAF) mara baada ya kuzungumza na watumishi wa
mfuko huo kwa lengo la kuhimiza uwajibikaji.
…………………………
Watumishi wa Mfuko wa Maendeleo
ya Jamii (TASAF) wametakiwa kuhakikisha wanufaika wa Mpango wa Kunusuru
Kaya Maskini wanahudumiwa vizuri kwa kupata ruzuku zao kwa
wakati ili
kuziwezesha kaya hizo kujikimu kimaisha na kuondokana na umaskini.
Hayo yamesemwa jijini Dar es
Salaam na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma
na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) wakati akizungumza na
watumishi wa TASAF makao makuu katika ziara yake ya kikazi yenye lengo
la kuhimiza uwajibikaji, kufahamu kwa kina majukumu ya TASAF na
kujiridhisha namna inavyotekeleza wajibu wake.
Mhe. Dkt. Mwanjelwa amesema, kwa
kuwahudumia vizuri wanufaika hao, TASAF pamoja na Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania itapata baraka za Mwenyezi Mungu ambaye kupitia
vitabu vyake vitakatifu ameelekeza kuwasaidia maskini na pia watakuwa
mfano bora wa kuigwa na nchini nyingine barani Afrika kwa kutekeleza
vema Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini
Mhe. Dkt. Mwanjelwa amewataka
watumishi wa TASAF kuwa tayari muda wote katika kuhakikisha kaya zote
maskini zinapata stahili zao kwa wakati na kufurahia matunda na
jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano za kuziwezesha kaya maskini
kuondokana na umaskini.
Aidha, Mhe. Dkt. Mwanjelwa
ameitaka TASAF kuhakikisha inaweka taratibu madhubuti za kisheria
zitakazowaadhibu na kuwadhibiti wote watakaobainika kufanya udanganyifu
kujipatia fedha za mpango wakati hawana sifa za kuwa wanufaika, lengo
likiwa ni kujenga nidhamu katika jamii ili fedha za Mpango wa Kunusuru
Kaya Maskini ziwafikie walengwa kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli anavyotaka.
Katika kutekeleza azma hiyo, Mhe.
Dkt. Mwanjelwa amewataka watumishi wa TASAF kufanya kazi kwa ari na
uzalendo mkubwa na kuipongeza TASAF kwa jitihada na mafanikio
waliyoyapata katika kuzinusuru kaya maskini mpaka hivi sasa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi
Mtendaji wa TASAF, Bw. Ladislaus Mwamanga amemhakikishia Mhe. Dkt.
Mwanjelwa kuwa, atahakikisha anasimamia vizuri utekelezaji wa Mpango wa
Kunusuru Kaya Maskini nchini kama alivyoelekeza, ili uwe ni mpango bora
zaidi katika bara la Afrika, na kuongeza kuwa, hadi sasa, tayari mpango
umeonekana kuwa ni miongoni mwa mipango bora barani Afrika kwani
umeweza kuboresha maisha ya kaya maskini ambapo utekelezaji wake
umewezesha kuzitambua kaya maskini, umesimamiwa vizuri, malipo
yanafanyika kwa wakati na hakuna ubadhilifu mkubwa wa fedha zilizotengwa
kwa ajili ya wanufaika.
Akithibitisha ubora wa mpango, Bw.
Mwamanga amesema, hivi sasa Rais wa Benki ya Dunia katika utekelezaji
wa majukumu yake ya kila siku, anapozungumzia programu za kupambana na
umaskini, haachi kuutaja Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini unaotekelezwa
nchini Tanzania kuwa ni bora na unasimamiwa vizuri.
Serikali ya Awamu ya Tano,
inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. John P. Magufuli aliyejipambanua kwa
vitendo kuwajali wanyonge, imedhamiria kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya
Maskini nchini kuwafikia walengwa katika kaya zote maskini nchini ili
walengwa hao waweze kunufaika na kuboresha maisha yao.
No comments :
Post a Comment