Tuesday, January 29, 2019

NDITIYE AZITAKA KAMPUNI ZA SIMU ZA MKONONI ZIRUDISHE FAIDA KWA JAMII


JPEG NA. 1
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akimkabidhi Magdalena Makalla (akiwa wodi ya wazazi) neti na mashuka kwa niaba ya Serikali kutoka kwa kampuni ya Halotel kwa ajili ya Hospitali ya Makole, Dodoma. Wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji Halotel, Nguyen Van Son na wa pili kushoto ni Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo, Dkt. George Matiko
JPEG. NA 3
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa kwanza kulia) akikabidhi vifaa mbali mbali vya hospitali kwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Makole, Dodoma Dkt. George Matiko (wa pili kulia) kwa niaba ya Serikali kutoka kwa kampuni ya Halotel kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa. Wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu wa Mawasiliano, Wizarani Mhandisi Dkt. Maria Sasabo na katikati ni Mkurugenzi Mtendaji Halotel, Nguyen Van Son wakishuhudia
JPEG. NA. 2
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (katikati)  akishuhudia makabidhiano ya hundi ya shilingi milioni 20.6 kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. Binilithi Mahenge (wa kwanza kulia) kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji Halotel, Nguyen Van Son (wa tatu kushoto) kwa ajili ya kuanzisha kiwanda cha kufyatua matofali cha kikundi cha vijana, Dodoma
JPEG. NA. 4
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akiongea na wananchi wa Dodoma kabla ya kukabidhi hundi ya shilingi milioni 20.6 kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. Binilithi Mahenge (hayupo pichani) kwa ajili ya mradi wa  kufyatua matofali wa kikundi cha vijana, Dodoma
JPEG. NA. 5
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa kwanza kulia) kwa niaba ya Serikali akikabidhi moja ya kitanda kwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Makole, Dodoma Dkt. George Matiko (wa pili kulia) kutoka kwa Halotel kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa. Katikati ni Mkurugenzi Mtendaji Halotel, Nguyen Van Son
………………………………………………………………………………………………
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye amezitaka kampuni za simu za mkononi nchini kurudisha faida kwa jamii ambayo ni wateja wake na wanatumia huduma za mawasiliano za kampuni zao
Nditiye ameyasema hayo wakati akikabidhi vifaa mbali mbali vya hospitali kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa ikiwemo vitanda, neti, mashuka na aproni vyenye thamani ya zaidi ya
shilingi milioni sita kwa niaba  Serikali kwa Hospitali ya Makole iliyopo Dodoma vilivyotolewa na kampuni ya simu za mkononi ya Halotel
“Nitoe wito kwa kampuni nyingine za simu za mkononi ziige mfano wa Halotel wa kurudisha shukrani kwa wananchi,” amesema Nditiye
Pia ameongeza kuwa mawasiliano ni moja ya Sekta ambayo inashika nafasi ya tano kwa maswali Bungeni ikiwemo Sekta nyingine za maji, afya, elimu, umeme, barabara ambapo Wabunge wamekuwa wakiuliza maswali mara kwa mara kuhusu Sekta ya Mawasiliano ambapo inadhihirisha kuwa wananchi wanatambua na kuthamini mchango wa mawasiliano katika maisha yao ya kila siku kwa kuwa mawasiliano ni uchumi na ni maendeleo
Vile vile amezitaka kampuni za simu za mkononi nne zilizosaini mkataba na kupewa ruzuku na Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) mwezi Desemba mwaka jana ikiwemo Vodacom, TIGO, Halotel na Shirika la Mawasiliano Tanzania kujenga minara ya na kupeleka huduma za mawasiliano haraka kwa wananchi
Naye Mganga Mkuu wa Hospitali ya Makole, Dodoma Dkt. George Matiko akipokea misaada hiyo ameishukuru kampuni hiyo na kusema kuwa anaipongeza kwa kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muugano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli za kuboresha sekta ya afya kwa kujenga vituo vya afya nchi nzima na kuongeza fedha za kununua dawa, vitendanishi na vifaa tiba ambapo hadi sasa hospitali hiyo imepokea shilingi milioni 500 kutoka Serikalini ambapo zimewezesha ukarabati wa hospitali hiyo na kuongeza utoaji huduma kwa wanawake 2,000 waliojifungua na kufanya operesheni kwa wagonjwa 300
“Tunashukuru kwa jitihada zenu Halotel, mahitaji bado ni mengi, muendelee kutuunga mkono katika kuwahudumia wananchi,” amesisitiza Dkt. Matiko
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halotel, Tanzania Nguyen Van Son amesema kuwa wameamua kurudisha faida na kutoa shukrani kwa wananchi kwa kuwaunga mkono kwa kutumia huduma za kampuni yao ambayo imesambaa nchi nzima na inatoa huduma kwenye maeneo yote ya mijini na hasa vijijini 
Nguyen ameishukuru Serikali kwa kuweka mazingira wezeshi na rafiki yaliyowavutia kuweza nchini kwenye Sekta ya Mawasiliano na wamedhamiria kuendelea kushirikiana na Serikali na wananchi kwa ujumla ili kupanua huduma za mawasiliano na kuhakikisha kuwa zinakuwa za viwango, ubora na gharama nafuu kwa mtumiaji
Katika hatua nyingine, Nditiye kwa niaba ya Serikali, ameshuhudia makabidhiano ya hundi ya shilingi milioni 20.6 baina ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. Binilithi Mahenge na Nguyeni kwa ajili ya uanzishaji wa kiwanda cha kufyatua matofali cha kikundi cha vijana wa Dodoma ambapo makabidhiano hayo yamefanyika kwenye viwaja vya Barafu mjini humo
“Vijana wa Dodoma mtanufaika na Serikali kuhamia Dodoma, tumeona tuanzishe kikundi cha vijana ili waweze kuanzisha kiwanda cha kufyatua matofali na mradi huo utakuwa na vijana wa kutoka Jeshi la Kujenga Taifa ili wawasaidie ili baadae vijana waweze kuanzisha na kuendeleza viwanda vyao,” amesema Dkt. Mahenge
Pia, ametoa rai kwa vijana wajitokeze na kuchamkia fursa mbali mbali zilizopo mkoani humo na wasikubali kukaa bure, wajihusishe na shughuli za uzalishaji, wasikubali kukaa nyumbani na vijiweni

No comments :

Post a Comment