Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi
Ndg.Rehema Madenge akizungumza na wataalamu kutoka Ofisi ya Msajili wa
Hazina na Ofisi ya Rais (hawapo pichani) katika kikao cha awali cha
mrejesho wa maamuzi ya utwaliwaji wa Kiwanda cha Kuchakata Korosho Lindi
(BUKO) mkoani Lindi muda mfupi kabla ya Serikali kukitwaa.
Mkuu wa Wilaya ya Lindi mkoani
Lindi Ndg.Shaibu Issa Ndemanga (kushoto), na Katibu Tawala wa Mkoa wa
Lindi Ndg.Rehema Madenge (kulia) wakizungumza na wataalamu kutoka Ofisi
ya Msajili wa Hazina na Ofisi ya Rais (hawapo pichani) katika kikao cha
awali cha mrejesho wa maamuzi ya utwaliwaji wa Kiwanda cha Kuchakata
Korosho Lindi (BUKO) mkoani Lindi.
Mkuu wa Wilaya ya Lindi Ndg.Shaibu
Issa Ndemanga (meza kuu kushoto), Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi
Ndg.Rehema Madenge (meza kuu katikati) na Kaimu Msajili wa Hazina
Ndg.Peter Gwagilo (meza kuu kulia) wakizungumza na timu ya wataalamu
kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina na Ofisi ya Rais na Sekretarieti ya
Mkoa wa Lindi muda mfupi kabla ya Serikali kukitwaa Kiwanda cha
Kuchakata Korosho Lindi (BUKO) mkoani Lindi.
Mkuu wa Wilaya ya Lindi Ndg.Shaibu
Issa Ndemanga (meza kuu kushoto), Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi
Ndg.Rehema Madenge (meza kuu katikati) na Kaimu Msajili wa Hazina
Ndg.Peter Gwagilo (meza kuu kulia) wakizungumza na timu ya wataalamu
kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina na Ofisi ya Rais na Sekretarieti ya
Mkoa wa Lindi (hawapo pichani) muda mfupi kabla ya Serikali kukitwaa
Kiwanda cha Kuchakata Korosho Lindi (BUKO) mkoani Lindi.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi
Ndg.Rehema Madenge (aliyesimama) akitoa ufafanuzi wa jambo wakati wa
kikao cha Serikali na Mwekezaji wa Kiwanda cha Kuchakata Korosho Lindi
(BUKO) muda mfupi kabla ya Serikali kukitwaa Kiwanda hicho leo.
Kaimu Msajili wa Hazina Ndg.Peter
Gwagilo (aliyetupa kisogo) akitoa maelezo ya awali juu ya uamuzi wa
Serikali kuamua kukitwaa Kiwanda cha Kuchakata Korosho (BUKO) mkoani
Lindi kabla ya zoezi hilo. Wa pili kulia mwenye shati jeupe ni
Mkurugenzi mwekezaji wa kiwanda hicho Ndg.Luc Moshaly anayemiliki
Kampuni ya Uwekezaji Buko pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Lindi Ndg.Shaibu
Issa Ndemanga (kulia).
Mhasibu wa Kiwanda cha Kuchakata
Korosho Lindi (BUKO), Ndg.Emmanuel Saba akizungumza kwa jazba na
Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi kwa pamoja na wataalamu kutoka Ofisi ya
Msajili wa Hazina na Ofisi ya Rais (hawapo pichani) juu ya uamuzi wa
Serikali kuamua kukitwaa kiwanda hicho kabla ya zoezi hilo.
Mkurugenzi mwekezaji wa Kiwanda
cha Kuchakata Korosho Lindi na mmiliki wa Kampuni ya Uwekezaji Buko,
Ndg.Luc Moshaly, akizungumza na Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi kwa pamoja
na wataalamu kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina na Ofisi ya Rais juu ya
uamuzi wa Serikali kuamua kukitwaa kiwanda hicho kabla ya zoezi hilo.
Wataalamu kutoka Ofisi ya Msajili
wa Hazina na Ofisi ya Rais wakihakiki mali za Kiwanda cha Kuchakata
Korosho Lindi (BUKO) mkoani Lindi mara baada ya Serikali kukitwaa
kiwanda hicho tayari kwa hatua zinazostahili ili kupata mwekezaji
mwingine mwenye uwezo na nia njema ya kukifufua na kukiendesha kwa
maslahi ya Taifa.
Muonekano wa sasa wa sehemu ya
mali za Kiwanda cha Kuchakata Korosho Lindi maarufu kama BUKO kilichopo
mkoani Lindi mara baada ya kutwaliwa na kurudishwa katika umiliki wa
Serikali kwa asilimia 100.
Muonekano wa sasa wa baadhi ya
sehemu zilizokua na matanki ya kuhifadhia maji kwa ajili ya uchakataji
wa zao la korosho kama zinavyooneka bila uwepo kwa matanki hayo ikiwa ni
sehemu ya mali za Kiwanda cha Kuchakata Korosho Lindi (BUKO) mara
baada ya kutwaliwa na kurudishwa katika umiliki wa Serikali kwa asilimia
100.
Muonekano wa sasa wa sehemu ya
mali (Mashine na Mitambo) ya Kiwanda cha Kuchakata Korosho Lindi maarufu
kama BUKO kilichopo mkoani Lindi mara baada ya kutwaliwa na kurudishwa
katika umiliki wa Serikali kwa asilimia 100.
Muonekano wa sasa wa sehemu ya
mali (Mtambo wa kutengeneza mvuke – ‘Boiler’) wa Kiwanda cha Kuchakata
Korosho Lindi maarufu kama BUKO kilichopo mkoani Lindi mara baada ya
kutwaliwa na kurudishwa katika umiliki wa Serikali kwa asilimia 100.
Wataalamu kutoka Ofisi ya Msajili
wa Hazina na Ofisi ya Rais chini ya ulinzi na uangalizi wa vyombo vya
usalama wakifunga milango kwa minyororo na kufuli katika sehemu za
kuingilia kiwandani bila kuathiri maeneo ya maghala ya kukusanyia na
kuhifadhi zao la korosho kutoka kwa wakulima ili kusubiri soko na wateja
kabla ya mnada.
Picha zote na Ofisi ya Msajili wa Hazina.
………………………
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania leo kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) yenye dhamana ya
kusimamia mali za Serikali kwa sehemu ambazo Serikali imefanya
uwekezaji, imekitwaa Kiwanda cha Kuchakata Korosho Lindi maarufu kama
BUKO kilichojengwa mwaka 1978 na kufanya uzalishaji kwa kipindi cha
miaka nane tu kikiwa na uwezo wa kuzalisha tani 10,000 kwa mwaka huku
lengo likiwa ni kufikia tani 60,000 kwa mwaka.
Akizungumza katika kikao cha awali
na Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi kuelezea utaratibu mzima ulivyokua
mpaka Serikali kufikia uamuzi huo kabla ya zoezi la utwaaji wa kiwanda
uliofanyika kiwandani eneo la Viwanda la Jamhuri pembezoni mwa barabara
iendayo Mtwara, Kaimu Msajili wa Hazina (TR) Ndg.Peter Gwagilo, amesema
hii ni sehemu tu ya utekelezaji wa kasi na Sera ya urejeshaji viwanda
vilivyobinafsishwa au kuuzwa na Serikali miaka ya nyuma na kubainika
kutofanya kazi kwa tija kama ilivyotarajiwa kwa mujibu wa mikataba
iliyoingiwa na wawekezaji husika hivyo viwanda kufa au kufanya kazi kwa
kusuasua kutokana na uwekezaji hafifu tofauti na makubaliano.
Kaimu Msajili wa Hazina
akitanabaisha nia njema ya Serikali katika urejeshaji wa viwanda vya
mtindo huu amesema utwaaji hufanyika baada ya kujiridhisha kutokana na
zoezi linalofanyika kila baada ya miezi mitatu la ufuatiliaji na
tathmini kuangalia utekelezaji wa mikataba ya uwekezaji iliyoingiwa
lengo mahususi likiwa ni kujiridhisha utekelezaji wa mikataba ambayo
Serikali imeingia na mwekezaji.
Ndg.Gwagilo amewasihi wawekezaji
walioingia mikataba ya uwekezaji na Serikali kutekeleza kama mikataba
inavyoainisha kwani zoezi la urejeshaji viwanda hivi bado ni endelevu na
Serikali inaendelea na taratibu zinazotakiwa katika kupata wawekezaji
wengine wenye uwezo, tija na nia madhubuti ya kuwekeza kwenye viwanda
hivyo na tayari utwaaji huu umeshafanyika kwenye mikoa kadhaa ikiwemo ya
Kilimanjaro (Kiwanda cha kutengeneza madawa ya mimea Moshi na Kiwanda
cha Kukoboa Mpunga Kilimanjaro), Tanga (Kiwanda cha Magogo ya Mbao) na
sehemu nyingine kama Kiwanda cha Maziwa UTEGI mkoani Mara, ambapo kwa
awamu hii jumla ya viwanda 12 kikiwemo hiki cha Korosho Lindi
kilichokwishatwaliwa vinatarajiwa kurejeshwa Serikalini baada ya
kujiridhisha vya kutosha kuwa mwekezaji ameshindwa kuwekeza kulingana na
mkataba.
Nae Mkuu wa Mkoa wa Lindi
Ndg.Godfrey Zambi akipokea ujumbe wa wataalamu Wilayani Kilwa kutoka
Ofisi ya Msajili wa Hazina na Ofisi ya Rais tayari kwa zoezi hilo
amesema, “Naishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina kufanya
maamuzi haya sahihi kwani kiwanda hiki hakijawahi kufanya uzalishaji
wenye tija kwa Taifa kama tulivyotarajia na hii inatokana na madhaifu
yaliyobainika katika zoezi zima la ubinafsishaji lililofanyika awali
miaka ya nyuma ambapo kwa sehemu kubwa mikataba hii ndiyo imeigharimu
Serikali yetu.”
Aidha, Mkuu wa Wilaya ya Lindi
Ndg.Shaibu Issa Ndemanga ameitaka Ofisi ya Msajili wa Hazina kutokata
tamaa kutokana na changamoto mbalimbali inazokumbana nazo katika mazoezi
haya ya ufuatiliaji, kufanya tathmini na utwaaji pale inapolazimu kwani
Serikali ni moja na hivyo ni vema kuwa na utaratibu wa mawasiliano ya
moja kwa moja na Msajili wa Hazina katika kuyazungumzia haya kuepusha
wazungumzaji wengi kwa jambo moja jambo linaloweza kuleta upotoshaji wa
taarifa.
Hali kadhalika nae Katibu Tawala
wa Mkoa wa Lindi Ndg.Rehema Madenge ameishauri Serikali kufanya maamuzi
ya kukiendesha yenyewe kiwanda hiki kutokana na uwekezaji na uendeshaji
duni kabisa wa mwekezaji katika kiwanda hiki uliopelekea kutokuwepo kwa
uzalishaji na badala yake kutumia majengo kama maghala ya kuhifadhia
mazao na vitu mbalimbali kwa kuyakodisha kitu ambacho ni tofauti kabisa
na lengo la Serikali katika ubinafsishaji na uuzaji wake kwa wawekezaji.
Pamoja na hilo Ndg.Madenge amekiri
kuwa nyota njema sasa inaonekana kwani ni mwanzo mzuri kuanza kwa zoezi
la utwaaji viwanda hasa katika mkoa wake wa Lindi kwani bila hivyo
Serikali itakua haiwatendei haki wakulima na wananchi wake kwa ujumla
kama viwanda vilivyo karibu nao havifanyi kazi ili kupata soko la
malighafi zao ambazo ni mazao yao.
Aidha, Katibu Tawala ameisihi pia
Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina kuhakikisha inawafanyia
upekuzi wa kina sana kabla ya kuwachagua wawekezaji wanaojitokeza na
kuonyesha nia ya kutaka kupatiwa viwanda kwa kubinafsishwa au kuuziwa
ili kufanya uwekezaji wenye tija ili kuleta faida itakayochagiza ukuaji
wa uchumi wa nchi, kuboresha kipato na hali ya maisha ya mwananchi mmoja
mmoja hali kadhalika kukua kwa pato la Taifa.
Taarifa hai ya ufuatiliaji na
tathmini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina imeeleza kuwa, “Kulingana na
Kifungu 7.1 na 7.2 cha Mkataba, mwekezaji alitakiwa kuwekeza kiasi cha
USD 600 kwa ajili ya kufanya ukarabati na kuboresha kiwanda ndani ya
miezi sita baada ya kukabidhiwa kiwanda tarehe 11 Mei, 2005; kulingana
na kifungu cha Mkataba 5.1. Mwekezaji alifanya uwekezaji mdogo kwa
kukarabati baadhi ya mashine pamoja na majengo. Hata hivyo, kiwanda
kilifanya kazi kwa mwaka mmoja 2007/08 na kusimamisha uzalishaji hivyo
mpaka kufikia siku hii ya kutwaliwa hakuna uzalishaji unaoendelea hivyo
Serikali imefanya maamuzi ya kukirejesha kiwanda hiki Serikalini
kufuatia kusimama kufanya kazi kwa muda mrefu na mwekezaji kutoonesha
jitihada zozote za uendelezaji wa kiwanda.”
No comments :
Post a Comment