Monday, September 17, 2018

NAIBU WAZIRI NDITIYE AIPA WIKI MOJA KAMPUNI YA TANZANIA REMIX KUWAPATIA VIWANJA WALIOKUWA WAKAZI WA KIPAWA

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akizungumza wakati wa ziara yake aliyoifanya huko Msomngola ili kukagua eneo lililotakiwa litolewe kama viwanja kwa wakazi waliopisha upanuzi wa kiwanja  cha ndege cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam Septemba 17, 2018. 
NA MWANDISHI WA TAA

  Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania Richard Mayongela(kulia) akifafanua jambo kwa wananchi wa maeneo ya Msongola, Ilala, Dar es Salaam wanaodai malipo ya maeneo yao kwa Kampuni ya Tanzania Remix ili yaweze kugawiwa kwa wananchi waliopisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere. Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (kushoto) akisikiliza kwa makini

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa kwanza kulia) akimsikiliza mmoja wa wananchi wenye mashamba eneo la Msongola, Ilala, Dar es Salaam, Mrisho Kawete (wa kwanza kushoto) ambao hawajalipwa na Kampuni ya Tanzania Remix iliyochukua mashamba yao kwa ajili ya kuwapatia wananchi waliopisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere

 Mwakilishi wa kampuni ya Tanzania Remix akitoa maelezo kuhusu viwanja 537 wanavyotakiwa kuwapatia wananchi waliopisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere.
Mhandisi Nditiye (kulia), akisikiliza malalamiko ya mmoja wa wananchi wanmaopaswa kufidiwa.(PICHA ZOTE NA MOHAMMED KIMWERI WA K-VIS BLOG)
NAIBU Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye ameielekeza Mamlaka ya Viwanja va Ndege Tanzania (TAA) kufuatilia na kupata viwanja vyake 537 kutoka kwa kampuni ya Tanzania Remix kama makubaliano ya mkataba yalivyo kwa ajili ya kuwapatia wananchi waliopisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salaam (JNIA)
Nditiye ameyasema hayo katika ziara yake ya kukagua viwanja 537 kwenye eneo la Msongola lililopo wilaya ya Ilala, Dar es Salaam ambapo kampuni ya Tanzania Remix  ilipewa jukumu na TAA ya kuandaa viwanja hivyo takribani miaka mitano sasa ili viweze kugawiwa kwa wananchi waishio maeneo ya Kipunguni A na Kipunguni Mashariki, Dar es Salaam waliopisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam kwa nia njema ili Serikali iweze kuendeleza na kupanua uwanja huo.
Nditiye amesema kuwa atafika tena kwenye eneo hilo baada ya wiki moja kukagua hatua iliyofikiwa ya upatikanaji wa viwanja hivyo kwa kuwa jambo hilo limechukua muda mrefu na Serikali haiko tayari kuona jambo hilo likiendelea pasipo kufika mwafaka kwa kuwa lina sura ya ujanja ujanja na uongo uongo ambao hauko wazi ambapo  wananchi wasio na hatia wanaumia bila sababu
Amefafanua kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia TAA imeilipa Kampuni ya Tanzania Remix kiasi cha shilingi bilioni 3.7 ili waweze kuandaa viwanja ambavyo vitakabidhiwa kwa wananchi hao waliopisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa JNIA. “Tumetembelea eneo hilo, tumejionee wenyewe, mmesikia wananchi wakiwa wanalalamika kuwa Tanzania Remix hawajawalipa wananchi mashamba yao ili yapimwe viwanja na kugawiwa wananchi waliopisha upanuzi wa uwanja wa ndege wa JNIA. TAA wana mkataba kati yao na Tanzania Remix na ninaamini TAA wamewavumilia sana Tanzania Remix. Nadhani sasa ni wakati TAA washikilie mkataba unasemaje na muanze kuchukua hatua kwa kuwa jambo hili limechukuwa muda mrefu, wananchi wako tayari kuachia viwanja na kupokea viwanja, hatuwezi kuona wananchi wananyanyaswa,” Nditiye amesema.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania Bwana Richard Mayongela amesema kuwa hadi hivi sasa kampuni ya Tanzania Remix imegawa viwanja 58 tu kwa wananchi kati ya viwanja 537 vinavyohitajika kugawiwa kwa wananchi na kazi hiyo imechukua muda mrefu kukamilika na hivyo wanaichonganisha Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wananchi walioridhia na kupisha upanuzi wa uwanja wa ndege wa JNIA kwa nia njema. Mayongela amewaomba wananchi waendelee kuwapa ushirikiano na kuvumilia jambo hili ili liweze kufanyiwa kazi na hakuna haki ya mwananchi yeyote itakayopotea kwa kuwa wananchi kwa uzalendo wao wamepisha eneo husika ili waweze kuona maendeleo ya taifa lao. “Mkataba huu ulikuwa ni wa miaka miwili ila bahati mbaya huu ni wa mwaka wa nne au wa tano unaenda na mkataba umeisha muda wake japo sisi tulilipa pesa nao watupe viwanja. Nimeelekeza wanasheria wapitie mkataba husika na kama utakuwa haujatekelezwa, TAA na wananchi tutachukua hatua ya kudai kampuni ya Tanzania Remix, hatutaki kesi na wananchi hawatak kesi ila wanataka haki yako,” amesema Mayongela.
Akiwa ziarani humo, Nditiye amezungumza na baadhi ya wananchi ambao maeneo yao ya Msongola  yametwaliwa na Kampuni ya Tanzania Remix ili yaweze kuchukuliwa, kupimwa, kuwekwa miundombinu mbali mbali na kugawiwa kwa wananchi waliopisha upanuzi wa uwanja wa ndege wa JNIA . Akizungumza kwa niaba ya wananchi wenzake mbele ya Mhandisi Nditiye, Bwana Mrisho Kawete amesema kuwa kampuni hiyo haijakamilisha malipo yote kwa wananchi hao hivyo hawako tayari kwa maeneo yao kuchukuliwa na kupatiwa wananchi waliopisha upanuzi. Naye Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Luhanga, Kata ya Msongola iliyopo wilayani Ilala, Dar es Salaam Bwana Lwembu Henjewele amesema kuwa wananchi wanaunga mkono jitihada za Serikali za kupanua uwanja huo na wameridhia maeneo yao wapatiwe wananchi wanaohitajika kulipwa fidia ila tu kampuni ya Tanzania Remix ikamilishe malipo kwa wananchi wake.

No comments :

Post a Comment