Saturday, March 24, 2018

PROF. LUOGA AONGOZA KIKAO CHAKE CHA KWANZA NA WAKUU WA MABENKI NA TAASISI ZA FEDHA

Na Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki Professor Florens LuogaGavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Prof. Florens Luoga.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Prof. Florens Luoga (wa pili kutoka kushoto), akiongoza kikao na watendaji wakuu wa mabenki na taasisi za fedha kilichofanyika BoT makao makuu jijini Dar es Salaam tarehe 23 Machi, 2018. Wengine kuanzia kushoto ni Manaibu Gavana, Bw. Julian Banzi Raphael, Dkt. Bernard Kibesse na Dkt. Yamungu Kayandabila.

The Bank of Tanzania headquarters in Dar es
Makao Makuu ya Benki Kuu ya Tanzania Dar es Salaam.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Prof. Florens Luoga, amesema kipaumbele chake ni kukuza na kuendeleza ushirikiano kati ya mabenki, Benki Kuu na Serikali.
Ameyasema hayo wakati alipoongoza kikao chake cha kwanza na watendaji wakuu wa mabenki na taasisi za fedha kilichofanyika BoT makao makuu jijini Dar es Salaam.
“Lengo langu kuu ni kukuza ushirikiano miongoni mwa mabenki, Benki Kuu na Serikali,” alisema Prof. Luoga wakati akijibu swali kutoka kwa mmoja wa washiriki wa mkutano huo aliyetaka kujua vipaumbele vya Gavana huyo. Hiki ni kikao cha kwanza cha Prof. Luoga na wakuu hao wa mabenki na taasisi za fedha tangu ashike madaraka ya ugavana mwanzoni mwa mwezi Januari mwaka huu.
Katika kikao hicho, Benki Kuu iliwaeleza wakuu hao wa mabenki na taasisi za fedha hali ya uchumi ilivyo hapa nchini, kikanda na duniani na mwelekeo wa utekelezaji wa sera ya fedha katika kipindi kijacho kama ulivyopitishwa na Kamati ya Sera ya Fedha ya Bodi ya Wakurugenzi ya Benki Kuu ya Tanzania.
Baadhi ya wakuu wa mabenki na taasisi za fedha katika kikao hicho.
Kushoto, washiriki wa Benki Kuu katika kikao hicho na kulia, Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, akizungumza na Mwenyekiti wa Chama cha Mabenki Tanzania (TBA) na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya CRDB, Dkt. Charles Kimei, mwishoni mwa kikao hicho.
Katika kikao hicho viongozi hao wa sekta ya kifedha hapa nchini walibadilishana mawazo kuhusu masuala mbalimbali ya kibenki na uchumi kwa ujumla.
Aidha, Mwenyekiti wa Chama cha Mabenki nchini (TBA), Dkt. Charles Kimei, alimpongeza Gavana Luoga kwa kuanzisha utaratibu wa kukutana na viongozi wa benki moja moja na akamuomba aweze kuandaa mkutano kati ya BoT na TBA ili kujadilia masuala mbalimbali yanayowahusu.
Kwa kawaida, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania hukutana na wakuu wa mabenki na taasisi za fedha kila baada ya kikao cha Kamati ya Sera ya Fedha ya Bodi ya Wakurugenzi ya Benki Kuu ya Tanzania na wakati wowote atakapoona inafaa.
Kushoto, Prof. Florens Luoga akizungumza na Ofisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Standard Chartered Bank Tanzania Ltd, Bw. Sanjay Rugani, mwishoni mwa kikao huku Manaibu Gavana, Bw. Julian Banzi Raphael na Dkt. Bernard Kibesse wakisikiliza. Kulia, Naibu Gavana Dkt. Kibesse akizungumza na CEO wa International Commercial Bank (Tanzania) Ltd, Bw. Ramakrishna Marakani, huku Gavana Luoga na Naibu Gavana Raphael wakifuatilia mazungumzo hayo.


No comments :

Post a Comment