=
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa
amesema Serikali inatambua umuhimu wa lugha ya Kiswahili kwa ustawi wa
Taifa na katika kulinda umoja wa Kitaifa.
Ametoa kauli hiyo leo mchana
(Jumatatu, Juni 19, 2017) wakati akizungumza na wabunge, viongozi wa
Serikali na wananchi waliohudhuria uzinduzi wa Kamusi Kuu ya Kiswahili
uliofanyika kwenye
ukumbi wa Bunge mjini Dodoma.
“Serikali inatambua umuhimu wa lugha
ya Kiswahili kwa ustawi wa nchi yetu na katika kulinda umoja wa
Kitaifa. Hakika lugha ya Kiswahili ndiyo inayotufanya tuwe Watanzania.
Hivyo, tunaithamini sana na kwetu hii ni lulu na tunu ya Taifa,”
amesema.
Waziri Mkuu amesema uzinduzi wa Kamusi
hiyo unaenda sambamba na azma ya Serikali ya kutumia Kiswahili kwenye
shughuli zote za kitaifa kama vile mikutano, mijadala, semina na
ufundishaji shuleni.
Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo
kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuhimiza
matumizi ya Kiswahili kwenye mikutano na matukio muhimu ya kitaifa, kama
vile dhifa za kitaifa anazowaandalia wageni wake kutoka nje ya nchi.
“Hata alipokuwa kwenye Mkutano wa
Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika wa mwaka 2017, Mheshimiwa
Rais alitumia Kiswahili kuhutubia mkutano huo. Amekuwa akifanya hivyo,
hata kwenye mikutano ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Lengo lake ni
kuitangaza lugha hii ya Kiswahili,” alisema.
Aliwasihi wazazi kote nchini
wahakikishe kuwa watoto wao wanapata kamusi hiyo kama moja ya nyenzo zao
za kujifunza lugha ya Kiswahili. “Vilevile, ninashauri, makundi mengine
kama vile waheshimiwa wabunge, wanahabari, wakalimani, wafasiri,
waandishi na wahariri wa vitabu, maofisa mawasiliano wa kwenye ofisi
zetu, muone umuhimu wa kununua Kamusi hii, ili iwasaidie kujiimarisha
kwenye matumizi ya Kiswahili fasaha na sanifu,” aliongeza.
Mapema, akizungumza katika hafla hiyo
fupi, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison
Mwakyembe alisema Kiswahili ni lugha ya pili inayotumiwa na watu wengi
zaidi barani Afrika lakini pia ni lugha ya 10 kati ya lugha 6,000
zinazozungumzwa na watu wengi duniani.
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa
Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA), Dk. Seleman Sewangi alisema kazi
ya kuandaa kamusi hiyo ilianza Agosti 12, 2011 na kukamilika mwaka 2015
ambapo toleo la kwanza lilichapishwa.
Alisema kamusi hiyo imekusanya maneno
mengi makuu (vidahizo) kuliko kamusi zilizotangulia na kwamba ya sasa
ina maneno hayo 45,500.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
- L. P. 980,
40480 – DODOMA.
JUMATATU, JUNI 19, 2017.
No comments :
Post a Comment