……………………….
Na Mwandishi Wetu
KAMPENI ya usajili wa watoto chini
ya Umri wa miaka 18 unaofanywa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF)
kwenye maonesho ya 41 ya Sabasaba, umekuwa kivutio kikubwa
ambapo
wazazi na walezi wamepongeza mpango huo.
NHIF inaendesha kampeni hiyo chini
ya mpango wa Toto Afya Kadi ambapo wazazi na walezi wanawasajili watoto
wao kwa gharama ya shilingi 50,400 na kupatiwa kitambulisho cha
matibabu kitakachomwezesha kupata huduma hizo ndani ya nchi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti
bandani hapo, Mkazi wa Kinondoni Bw. Ally Raymond amepongeza Mfuko kwa
kuja na mpango huo ambao umekuwa ni wa nafuaa kwa wazazi na walezi ambao
hawakuwa na fursa ya kupata huduma hizo.
“Kwa kweli hii ni hatua kubwa
lazima tuwapongeze hasa kwa kuwajali watoto hawa chini ya umri wa miaka
18 ambao hasa ndio wana uhitaji mkubwa wa matibabu hivyo name nitoe wito
kwa wazazi wengine kutumia fursa hii ili kuwa na uhakika wa matibabu wa
watoto wao,” alisema Bw. Raymond.
Mzazi mwingine alipongeza hatua ya
NHIF ya kusajili na kutoa vitambulisho hivyo baada ya siku moja hatua
ambayo imeondoa usumbufu kwa wanaohitaji kusajili watoto wao.
Akizungumza bandani hapo Kaimu
Mkurugenzi wa Masoko na Utafiti, Bi. Angela Mziray alisema kuwa hii ni
fursa nzuri kwa wazazi na walezi ya kupata vitambulisho vya matibabu na
kuwa na uhakika wa kupata matibabu wakati wowote na kuondokana na
usumbufu ambao wangeweza kuupata.
Alisema kuwa NHIF imeanzisha
mpango huo kutokana na umuhimu wa kundi la watoto ambao wameonekana kuwa
na uhitaji mkubwa wa kulindwa kwa kuhakikishiwa huduma za matibabu.
Jumla ya watoto 150 wameshasajiliwa na kupatiwa vitambulisho vyao.
Mbali na huduma ya usajili wa
watoto, Mfuko pia unatoa huduma ya elimu kwa juu ya huduma za Bima ya
Afya lakini pia kushughulikia kero mbalimbali za wanachama.
No comments :
Post a Comment