Monday, May 1, 2017

SWANSEA YAIZUIA MANCHESTER UNITED KUSOGEA KATIKA NAFASI YA NNE

Mpira wa adhabu uliopigwa kiufundi na Gylfi Sigurdsson umeipatia Swansea pointi muhimu ikihaha kubakia katika Ligi Kuu ya Uingereza na kuharibu hesabu za Manchester United kutinga katika nafasi ya nne.

Sigurdsson alipiga shuti la kuzungusha kutoka umbali wa yadi 30 lililotinga wavuni huku kipa akibaki anauangalia mpira, na kufanya matokeo kuwa 1-1 baada ya awali Wayne Rooney kufungwa kwa mkwaju wa penati.
Kwa matokeo hayo Manchester United imebakia katika nafasi ya tano, pointi moja nyuma ya mahasimu wao Manchester City ambao wanapointi 66 sawa na Liverpool iliyokatika nafasi ya tatu zikiwa zimecheza michezo sawa.
   Wayne Rooney akifunga kiufundi mpira wa penati kwa kumpoteza mahesabu kipa
     Mpira wa adhabu uliopigwa kiufundi na Gylfi Sigurdsson ukielekea kutinga wavuni

TOTTENHAM HAIJAKATA TAMAA YAENDELEA KUIFUKUZIA CHELSEA

Tottenham imejihakikishia kuwa inaendelea kuwa nyuma ya vinara wa Ligi Kuu ya Uingereza Chelsea kwa tofauti ya pointi nne baada ya kuwafunga wapinzani wao Arsenal kwa magoli 2-0 katika dimba la White Hart Lane.

Ushindi wa Chelsea 3-0 dhidi ya Everton uliipa presha Tottenhma lakini walijibu mapigo kwa staili nao kwa kupata ushindi na kuendelea na kiwango bora, ikilinganishwa na cha Octoba 1960 waliposhinda michezo 13 mfululizo.
Mchezo wao huo dhidi ya Arsenal uliamuliwa na magoli yaliyofungwa na Dele Alli katika dakika ya 55 likiwa ni goli lake la 21 katika msimu huu, na kisha baadaye Harry Kane akafunga goli la pili kwa mkwaju wa penati.
                    Mchezaji nyota kijana Dele Alli akifunga goli la kwanza la Tottenham 
Harry Kane akijipinda na kuachia shuti la mkwaju wa penati aliopiga kiufundi na kufunga goli la pili

CHELSEA IMEDHAMIRIA KUTWAA UBINDWA LIGI KUU YA UINGEREZA

Vinara wa Ligi Kuu ya Uingereza Chelsea wamepiga hatua kubwa katika kuelekea kutwaa ubingwa baada ya kuibuka na ushindi wa magoli 3-0 dhidi ya Everton katika dimba la Goodison Park.

Chelsea ilipata goli la kwanza kwa shuti kali la Pedro la umbali wa yadi 25, kisha Gary Cahill alifunga la pili kwa shuti la karibu kabla ya Willian kufunga la tatu na kuifanya iendelee kuongoza kwa tofauti ya pointi nne.
Kwa ushindi huo Chelsea hata wakipoteza pointi tatu katika michezo minne iliyosalia bado wataweza kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza, hata kama Tottenham watashinda michezo yote iliyosalia.
                                    Pendro akiachia shuti kali lililozaa goli la kwanza la Chelsea
                                      Gary Cahill akiifungia Chelsea goli la pili katika mchezo huo

No comments :

Post a Comment