Makamu wa Rais Mhe.Samia Hassan
Suluhu amewataka wanachama wa bonde la mto Nile (NBI) kuongeza
ushirikiano na kuanzisha programu za maendeleo ili kuwa na matumizi
sahihi ya maji ya bonde la mto huo.
Mhe.Samia ameongea hayo wakati
akizungumza katika maadhimisho YA 18 ya siku ya Nile (Nile day)
yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam hivi karibuni.
“Ningependa kuona kuna programu
mbalimbali zinawekwa ili kupata picha halisi ya wapi tunaelekea kwa
sababu watu milioni 350 wapo katika Bonde la Mto Nile na wanalitumia kwa
ajili ya Maji,Nishati na Chakula,kwahiyo ni lazima kuwepo na programu
zitakazosaidia kuhifadhi mazingira ya bonde hili”,alisema Mhe.Samia
Aidha ameeleza kuwa kipengele
muhimu katika kufanikisha suala la kulinda mazingira ya mto Nile ni kwa
wanachama kukaa pamoja na kuweka sawa masuala ya usimamizi wa
maji,matumizi mazuri ya rasilimali zilizopo, utawala bora,ukuaji wa
idadi ya watu na mabadiliko ya hali ya hewa katika eneo hilo la bonde la
mto Nile.
Pia ametoa wito kwa Sekta binafsi
na washirika wa maendeleo kushiriki kwa karibu katika suala hili na
hasa watu wa utafiti kufanya utafiti wa kisayansi katika kupata majibu
ya masuala mbalimbali yanayojitokeza katika Bonde hili.
Kwa upande wake, Waziri wa Maji
na Umwagiliaji, Mhandisi Gerson Lwenge amesema kuwa maadhimisho haya ya
siku ya Nile yana lengo kuu la kujenga uelewa kwa jamii na nchi
wanachama juu ya umuhimu wa kulinda vyanzo vya maji yanayopeleka katika
mto Nile na hivyo kuyalinda kwa hali na mali kwani eneo hilo lina idadi
ya watu 350 milioni na hivyo ushirikiano zaidi unahitajika kulinda
mazingira yake.
Katika maadhimisho haya ya 18 ya
Bonde la mto Nile pia mawaziri mbalimbali kutoka nchi kumi(10) wanachama
walisisitiza katika kulinda mazingira,usalama,ushirikiano bora,kulinda
mazingira ya bonde ilo,kuzuia mmomonyoko wa ardhi na ulinzi wa vyanzo
vya maji ya mto Nile
No comments :
Post a Comment