Kumekuwa na habari zinazoenea na
kujirudia sana katika mitandao ya kijamii kuhusu hali ya afya ya Rais
Mstaafu wa Awamu ya Pili, Alhaji Alli Hassan Mwinyi. Taarifa hizo ambazo
hazieleweki lengo lake, zimekuwa zikidai kuwa Mzee Mwinyi amefariki
dunia.
Tutautaarifu umma kuwa habari
hizo si za kweli, ni za kupuuzwa. Mzee Mwinyi ni mzima wa
afya,
anaendelea na majukumu yake kama kawaida ambapo jana Alhamisi
amehudhuria chakula cha jioni kuadhimisha siku ya Taifa la Kuwait na leo
mchana alitarajiwa kwenda kumjulia hali Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa
David Msuya.
Natumia fursa hii kuendelea
kuwakumbusha watumiaji wa mitandao ya kijamii kuwa waliobuni teknolojia
hii walikuwa na malengo adhimu ya kumpatia mwanadamu uwanja na uwanda
mpana wa mawasiliano-tusiwachezee shere wabunifu hao kwa kuitumia
kinyume cha malengo.
Aidha, jamii ifahamu kuwa ni kosa
kwa mujibu wa kifungu cha 16 cha Sheria ya Makosa ya Mitandaoni, 2015,
kwa mtu yeyote kutangaza, kuchapisha au kueneza habari za uongo au
uzushi katika mitandao.
Kwa niaba ya Serikali nachukua
fursa hii kuwapa pole familia ya Mzee Mwinyi na watanzania wengine kwa
mshtuko walioupata kutokana na uzushi huu. Katika hili hatua kali za
kisheria zitachukuliwa dhidi ya watakaobainika kuhusika na uhalifu huu.
Imetolewa na:
Dkt. Hassan Abbasi
Mkurugenzi, Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali
No comments :
Post a Comment