Thursday, December 29, 2016

KUFANYIWA KAZI HOJA ZA MWANANCHI ALIYELALAMIKA KWA RAIS


tou
Katika gazeti la Mwananchi toleo la Desemba 16 mwaka huu, ukurasa wa 11, kulichapishwa barua ya Afisa Mifugo mstaafu wilayani  Mpwapwa, Dododma, Bw. Edward Chedego Uledi. Katika barua yake iliyosomeka “Rais Magufuli nisaidie nilipwe stahiki zangu,” mstaafu huyo alilalamikia kupunjwa mafao yake.
Mtumishi huyo aliyestaafu tangu 2008, alilalamikia kitendo cha maafisa utumishi   kuchelewa kurekebisha taarifa zake kwa kuzingatia cheo chake cha mwisho na hivyo kusababisha apunjwe mafao na akalipwa kwa mujibu wa cheo cha zamani.

Serikali imefuatilia kwa kina na kuona kuna ukweli katika sehemu ya madai ya mstaafu huyo. Tunapenda kuutaarifu umma kuwa malalamiko ya mwananchi huyo sasa yameshughulikiwa haraka na Bw. Uledi amejulishwa na kuridhika na hatua zilizochukuliwa. Akiishukuru Serikali kwa hatua hizo alisema:
Nimeeleweshwa vizuri, nimeelewa na naishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kasi hii. Namshukuru sana Rais na nawapongeza watendaji wote waliojitoa kufuatilia na kutatua malalamiko ya mimi mwananchi wa kawaida.”
Serikali inatumia nafasi hii kuvipongeza vyombo vya habari nchini vinavyojitoa na kujikita katika kusaidia kutatua changamoto za kweli za wananchi. Aidha tunawakumbusha watendaji wa Serikali kuendelea kufanyakazi kwa bidii, ubunifu, kasi na kujituma katika kufuatilia na kutatua kero mbalimbali za wananchi.
Imetolewa na:



Dkt. Hassan Abbasi,
Mkurugenzi Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali.

No comments :

Post a Comment