Monday, May 23, 2016

Serikali yawaunganisha watafuta kazi 20,000 na waajiri

Jamillah-2-620x308 
Frank Mvungi-Maelezo
Serikali imefanikiwa kuwaunganisha Watanzania wanaotafuta kazi wapatao 20,000 ikiwa ni moja ya hatua ya kupunguza tatizo la ajira nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Msemai wa Wakala wa Huduma za Ajira nchini (TaESA) Bi Jamila Mbarouk wakati wa mkutano na vyombo vya habari leo jijini Dar es salaam.
Akizungumzia watafuta kazi waliongushwa tangu kuanzishwa kwa wakala huo Jamila alisema kuwa wengi waliounganishwa walikuwa wahasibu, Makatibu muhtasi, wataalamu wa huduma za jamii.
 “Jukumu letu letu ni kuwaunganisha watafuta kazi na waajiri ndani na nje ya nchi ili waweze kupata huduma hii kwa urahisi kwa kuzingatia sheria na kanuni za Ajira hapa nchini” alisisitiza Jamila.
Katika kupanua huduma ili kuwafikia watanzania walio wengi Jamila amebainisha kuwa (TaESA) imefungua ofisi za Kanda katika Mikoa ya Dodoma,Mwanza, na Arusha .
Mafanikio Mengine ni wakala kuendesha mafunzo ya kuwajengea uwezo watafuta kazi 3185 ili kuweza kuhimili ushindani na changamoto za soko la ajira.
Mafunzo hayo yametolewa mbalimbali ikiwemo chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Taasisi ya Uhasibu (TIA), Chuo cha Ardhi na Taasisi ya Teknplojia Dar es salaam (DIT).
Akieleza Umuhimu wa mafunzo hayo Jamila amesema kuwa yanalenga kuwajengea uwezo watafuta kazi ili waweze kuandika barua za maombi ya ajira kwa ufasaha, kuandaa wasifu binafsi (CV) na kuwajengea uwezo wa namna ya kufanya mahojiano kwa ufanisi kwa kuzingatia mbinu za kisasa.
Kwa upande wake Afisa Kazi wa TaEsa Bw. Amani Kasale amesema kuwa baadhi ya watafuta kazi wamekuwa na kasumba ya kuchagua maeneo ya kufanyia kazi hasa yale yaliyopo katika miji mikuu hali inayozorotesha juhudi za Serikali kuwaunganisha watafuta kazi na waajiri katika maeneo mbalimbali hapa nchini na nje ya nchi.
Akifafanua Kasale alisema kuwa huduma ya kuwaunganisha watafuta kazi na waajiri inatolewa bure kwa watanzania wote wanaotafuta ajira kwa kuzingatia sheria na Kanuni za ajira hapa nchini.
Pia Kasale alitoa wito kwa vijana wote wanaotafuta ajira kuachana na kasumba ya kuchagua maeneo ya kufanya kazi hasa yale yaliyo katika miji mikuu na kutumia fursa zilizopo maeneo ya pembezoni.
Wakala wa huduma za Ajira Tanzania TaESA Ulianzishwa kwa sheria ya wakala Na. 30 ya mwaka 1997 ikiwa na lengo la kuunganisha watafuta kazi na waajiri wenye fursa za ajira ndani na nje ya nchi.
CCM ZANZIBAR YASISITIZA USHIRIKIANO KWA WAJUMBE WA BARAZAM LA WAWAKILISHI.
shei5 
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar.
CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimewataka Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar  kuendelea  kushirikiana ili kuunda nguvu ya pamoja itakayosaidia kuharakisha  maendeleo ya nchi kwa ufanisi zaidi.
Kimesema utendaji mzuri wa viongozi hao ndani ya Baraza hilo ndiyo utakaoweza kukirahisishia kazi Chama cha Mapinduzi katika uchaguzi mkuu wa 2020, hali itakayojenga imani kwa wananchi kuirejesha tena CCM madarakati kutokana na utendaji mzuri wa viongozi hao.
Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Nd. Vuai Ali Vuai  wakati akibadilishana mawazo na Katibu Mpya  wa Kamati ya Wawakilishi wa Chama cha Mapinduzi ndani ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar (Mnadhimu) huko Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Mjini hapa.
Nd. Vuai alimpongeza kiongozi huyo kwa kuaminiwa na Wajumbe wa Baraza hilo na kumchagua kuwa Mnadhimu wa Wawakilishi wote wa CCM ndani ya Chombo hicho cha kutunga sheria za nchi.
Alisema kuchaguliwa kwa Mnadhimu huyo pamoja na msadizi wake kutasaidia kuongeza ufanisi wa kusimamia vyema shughuli za baraza la wawakilishi ili ziende sambamba na mahitaji ya wananchi majimboni.
Alieleza kwamba mbali na viongozi hao kuwa na jukumu la kuandaa miswaada, kutunga sheria na kupitisha Bajeti za nchi bado wana wajibu wa kusimamia kwa vitendo ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2015/2020 pamoja na kulinda maslahi ya Chama hicho.

RAIS DKT. MAGUFULI AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA WAZIRI MKUU NA JAJI MKUU IKULU

 jpm2 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliyefika Ikulu kwa ajili ya mazungumzo na Rais Dkt. Magufuli.PICHA NA IKULU
jpm1 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akifurahia jambo na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa mara baada ya kumaliza mazungumzo Ikulu jijini Dar es Salaam.
jpm4 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na  Jaji Mkuu wa Tanzania Mohamed Chande Othman mara baada ya kumaliza mazungumzo yao  Ikulu jijini Dar es Salaam.
jpm3 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na Jaji Mkuu wa Tanzania Mohamed Chande Othman Ikulu jijini Dar es Salaam.

SERIKALI YAFAFANUA KUHUSU NDEGE NDOGO ZINAZOENDESHWA NA RUBANI MMOJA

images 
Na Benedict Liwenga, MAELEZO, Dodoma.
SERIKALI imesema kuwa, hakuna kiwango kinachobainisha wazi kuwa ndege yenye uwezo wa kubeba abiria kumi au zaidi ni sharti iendeshwe na marubani wawili.
Kauli hiyo imetolewa leo Bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri. Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Eng. Edwin Ngonyani wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Tambwe, Mhe. Khalifa Issa aliyetaka kujua kuhusu Sheria za nchi na za Kimataifa zisemavyo kuhusu ndege za namna hiyo kurushwa na rubani mmoja.
Eng. Ngonyani amesema kwamba, taratibu zinazoongoza fani ya kuendesha ndege nchini huongozwa na miongozo inayokubalika Kimataifa na ambayo imeridhiwa hapa nchini na Bunge.
Amefafanua kuwa, Katika taratibu hizo, kuna matakwa ya kisheria na kiufundi ambayo yakifuatwa yanawezesha kuwa na uwezekano mdogo sana wa kukumbwa na athari ya kiafya na kushindwa kumudu kuendesha ndege.
Ameeleza kuwa, Marubani hupimwa afya zao na madaktari bingwa kila muda maalum kulingana na umri kama ilivyoainishwa katika Kanuni ya 140 mpaka 177 ya The Civil Aviation (Personnel Licensing) Regulations, 2012.
“Serikali inaruhusu ndege kuendeshwa na rubani mmoja kwa kuzingatia taratibu hizo, Aidha, Kanuni 32(5) inasema kwamba ndege iliyoandikishwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuruka kwa shughuli za kibiashara yenye uzito unaozidi kilo 5,700 itakuwa na marubani wasiopungua wawili”, alisema Eng. Ngonyani.
Pia amefafanua kuwa, shughuli za Usalama wa Anga nchini zinaongozwa na Sheria Namba 80 “Cvil Aviation Act. 80” na Kanuni zilizotengenezwa chini yake, ambapo urushaji wa ndege yenye abiria tisa au zaidi unaongozwa na Kanuni ziitwazo “The Civil Aviation (Operation of Aircraft) Regulations, 2012” ambapo ndege inayotimiza vigezo vilivyowekwa kwenye vifungu (2), (3) na (4) vya Kanuni ya 32 kuwa na uzito wa chini ya kilo 5,700 inaruhusu kuendeshwa na rubani mmoja.
Ameongeza kuwa, katika viwango vinavyotolewa na Shirika la Kimataiaf la Usafiri wa Anga (ICAO) kwenye kiambatanisho namba 19, chini ya Mkataba wa Kimataifa wa Usafiri wa Anga (Chicago Convention) hakuna kiwango chochote kinachobainisha wazi kuwa ndege yenye uwezo wa kubeba abiria 10 au zaidi ni sharti iendeshwe na marubani wawili.
“Pia hakuna hata mapendekezo ya kiutekelezaji kwenye suala hilo, na hata katika Kiambatanisho cha 6 chenye sehemu tatu kianchohusiana na uendeshaji wa ndege ambacho ndicho kinachozungumzia idadi ya marubani katika uendeshaji wa ndege hakina katazo hilo”, alisisitiza Eng. Ngonyani.

WIZARA YA KUDHIBITI MIGOGORO YA ARDHI KWA KUFUNGUA MABARAZA YA ARDHI

nu1
Jengo la Baraza la Ardhi Kiteto.
…………………………………………………………………………………………..
Katika azma ya kuimarisha huduma ya utatuzi wa migogoro ya ardhi nchini, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuboresha na kufungua Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya yatakayohusika na migogoro katika maeneo mbalimbali nchini.
Kwa upande wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mapya,  Baraza ambalo limeshaanzishwa rasmi, ni lile lililopo katika wilaya za Kahama na tayari limepatiwa vitendea kazi muhimu na watumishi.
Wizara imeunda Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya mapya 47 kupitia GN 544/2016, kati ya mabaraza hayo mapya 47, Mabaraza ya Lushoto, Kiteto, Kasulu, Kibondo na Bagamoyo yamepatiwa vitendea kazi na yataanza kufanya kazi mwishoni mwa mwaka huu wa fedha.
Aidha, uimarishaji wa Mabaraza hayo utapunguza mlundikano wa mashauri katika Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya kwa kuwa migogoro isiyo ya lazima kwenda ngazi ya wilaya itasuluhishwa katika ngazi ya kijji au kata.
Katika picha ni baadhi tu ya Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ambayo yapo tayari kufunguliwa; Kiteto, Lushoto, Kigoma mjini na Kibondo.

Serikali yakamata kilo 140 za dawa za kulevya nchini

images 
Na Anitha Jonas – MAELEZO
Dar es Salaam.
Serikali imefanikiwa kukamata takribani kilo 139.69 za dawa za kulevya ikiwemo kilo 53.49 za Heroin, Cocaine kilo 86.2 kuanzia mwaka 2015 mpaka Aprili mwaka huu.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari kutoka Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya iliyotolewa na Mkuu wa Kitengo cha Elimu, Habari na Takwimu wa tume hiyo, Amani Msami, pia tume hiyo imekamata tani 97 za bangi na mirungi.
Alisema mbali na kukamata kilo hizo, takwimu zinaonesha kuwa watumiaji wa Heroin nchini wanakadiriwa kuwa kati ya 200,000 hadi 425,000 ambapo kati ya hao 30,000 hutumia dawa hizo kwa njia ya kujidunga sindano.
“Serikali imefanikiwa kukamata takribani kilo 53.49 Heroin, Cocaine kilo 86.2 kuanzia mwaka 2015 mpaka Aprili mwaka huu” alisema Msami na kuongeza kuwa:
“Watumiaji wa Heroin nchini wanakadiriwa kuwa kati ya 200,000 hadi 425,000 ambapo kati ya hao 30,000 hutumia dawa hiyo kwa njia ya kujidunga”.
Msami alifafanua kuwa mbali na kukamata dawa hizo, tume hiyo ilikamata tani 81.3 za bangi na Mirungi tani 15.7.
Aliongeza kuwa mbali na hayo idadi ya watuhumiwa waliyokamatwa wakijihusisha na usafirishaji wa dawa za kulevya zikiwemo Bangi,Mirungi, Heroin na Cocaine walikuwa 14,503.
Hata hivyo, alisema takwimu hizo zinaonyesha jitihada za serikali katika kukabiliana na biashara ya dawa za kulevya nchini na si ukubwa wa usafirishaji wa Heroin na Cocaine nchini.
“Moja ya jitihada za Serikali katika kukabiliana na tatizo la dawa za kulevya ni kutungwa kwa Sheria ya kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya Na.5 ya mwaka 2015.” Alisema Msami.
Alifafanua kuwa sheria hiyo imeweka adhabu kali kwa makosa ya kujihusisha na matumizi na biashara ya dawa ya kulevya ikiwemo kifungo cha maisha kwa yeyote atakayesafirisha dawa za kulevya.

Atakeyehusisha watoto na dawa za kulevya jela miaka 30

images 
Anitha Jonas – MAELEZO
Dar es Salaam.
SERIKALI imesema kuwa mtu yeyote atakayekamatwa kwa kosa la husisha au kushawishi mtoto kujiingiza katika matumizi au biashara ya dawa za kulevya atahukumiwa kifungo cha miaka isiyopungua 30.
Hayo yamesema na Mkuu wa Kitengo cha Elimu, Habari na Takwimu wa Tume ya kuratibu na kudhibiti wa Dawa za Kulevya, Amani Msami kupitia Taarifa ya tume hiyo kwa vyombo vya habari.
Msami alisema adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Sheria ya kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya Na.5 ya mwaka 2015 tofauti na Sheria ya Kuzuian Biashara Haramu ya Dawa za Kulevya Na. 9 ya mwaka 1995 iliyokuwa na mapungufu.
Alisema mbali na adhabu hiyo, sheria hiyo mpya imeweka adhabu ya kifungo cha maisha na faini ya shilingi Milioni 200 kwa kumiliki mitambo ya kutengeneza dawa za kulevya.
Msami aliongeza kuwa Sheria hiyo pia imeweka adhabu kali ya kifungo cha maisha pamoja na faini isiyopungua Shilingi Bilioni moja kwa watu wanaofadhili biashara ya Dawa za Kulevya.
“Aidha, sheria hii imeweka adhabu kali ya kifungo cha maisha pamoja na faini isiyopungua Shilingi Bilioni moja kwa watu wanaofadhili biashara ya Dawa za Kulevya ambao mara nyingi ni watu wenye uwezo,”alisema Msami.
Mkuu huyo wa Kitengo, alisema Serikali kupitia vyombo vya Dola iliwabaini, kuwakamata na kuwachukulia hatua za kisheria baadhi ya wafanyabiashara wadogo na wakubwa wa dawa za kulevya.
Aliwataja baadhi ya watuhumiwa wakubwa wa dawa hizo waliokamatwa na kuchukuliwa hatua kuwa ni  Ali Khatibu haji (maarufu kwa jina la Shkuba, Mohammed Mwarami (maarufu kwa jina la Chonji na Mwanaidi Mfundo (maarufu kwa jina la Mama Leila).
Msami alisisitiza wito wa Serikali kwa wananchi kutoa ushirikiano wa dhati kwa ajili ya kutoa taarifa kuhusu watu wanaojihusisha na biashara ya dawa ya kulevya  ili waweze kuchukuliwa hatua za kisheria.

SERIKALI KUENDELEA KUONGEZA BAJETI KWA AJILI YA BARABARA.

index 
Na Benedict Liweng, MAELEZO, Dodoma.
SERIKALI imesema itaendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya barabara kadri uwezo wa kifedha utakavyoongezeka.
Hayo yamesemwa leo Bungeni Dodoma na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Miko na Serikali za Mitaa, Mhe. Selemani Jafo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum. Mhe. Sophia Mwakagenda aliyetaka kujua utayari wa Serikali katika kukubali ombi la Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, Mkoani Mbeya na kuongeza fedha katika Bajeti ya mwak 2016/2017.
Mhe. Jafo amesema kwamba, Halmashauri ya Rungwe iliandaaa makisio ya bajeti ya Shilingi bilioni 7.9 kwa ajili ya matenegenzo ya barabara katika bajeti ya mwaka 2016/17, hata hivyo kutokana na ukomo wa bajreti fedha zilizoidhinishwa ni shilingi milioni 920 ambazzo zitatumika kwa ajili ya matenegenezo ya barabara na ujenzi wa madaraja.
“Katika mwaka wa fedha wa 2015/16, Halmashauri hiyo ilitengewa shilingi milioni 870 na tayari Serikali imeshapeleka milioni 157.9”, alisema Mhe. Jafo.
Aliongeza kuwa, fedha za Mfuko wa Barabara katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2016/17 ni shilingi bilioni 247.5 ambazo endapo zingegawanywa sawa kwa Halmashauri zote 181 zilizopo, kila Halmashauri ingekuwa na bajeti ya shilingi bilioni 1.3.
Amefafanua kuwa mara zote mahitaji yamekuwa ni makubwa kuliko uwezo wa rasilimali fedha kukidhi mahitaji hayo ndiyo maana Serikali inaweka vipaumbele ili kutekeleza mambo machache kwanza kulingana na uwezo uliopo kibajeti.
“Serikali itaendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya barabara kadri uwezo wa kifedha utakavyoongezeka”, alisema Mhe. Jafo.

WAZIRI MKUU KUHUDHURIA MKUTANO WA ADB ZAMBIA

MSAMA1 
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa anaondoka nchini leo (Jumatatu, Mei 23, 2016) kwenda Lusaka, Zambia kuhudhuria Mkutano wa 51 wa Mwaka wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (51st Annual Meeting of the Board of Governors of the African Development Bank – AfDB) utakaofanyika kesho (Jumanne, Mei  24, 2016).
Waziri Mkuu anahudhuria mkutano huo kwa niaba ya Mheshimiwa Rais, Dk. John Pombe Magufuli.
Mkutano huo ambao utafunguliwa na Rais wa Zambia, Edgar Lungu utajadili masuala ya Nishati na Mabadiliko ya TabiaNchi. Pia utahudhuriwa na Marais Idriss Deby wa Chad, Paul Kagame wa Rwanda na Uhuru Kenyatta wa Kenya. Nigeria itawakilishwa na Makamu wake wa Rais, Yemi Osinbajo huku Msumbiji ikiwazilishwa na Waziri wake Mkuu, Carlos Agostinho do Rosário.
Watu maarufu waliothibitisha kuhudhuria mkutano huo ni pamoja na Kofi Annan, Ashish Thakkar, John Kufuor, Mary Robinson, Mo Ibrahim, Nancy Lee, Ngozi Okonjo-Iweala na Tony Elumelu.
Mkutano huo utakaofanyika kwenye kituo cha mikutano cha kimataifa cha Mulungushi (Mulungushi International Conference Centre) utahudhuriwa na washiriki zaidi ya 5,000 kutoka nchi  54 ambao ni wanachama wa benki hiyo, washiriki kutoka nchi 26 ambazo si za bara la Afrika (non-regional member countries), wawakilishi wa mashirika ya kimataifa, wadau wa maendeleo na wawakilishi wa asasi za kiraia. Wengine ni Mawaziri wa fedha, biashara na uchumi na wataalamu kutoka vyuo vikuu.
Waziri Mkuu amefuatana na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Asantu Kijaji, wachumi kadhaa pamoja na wataalamu wa sekta ya fedha.

DAR YAONGOZA KWA AJALI ZA BARABARANI

images 
Na Fatma Salum- MAELEZO, Dodoma.
Serikali imesema kuwa Jiji la Dar es Salaam linaongoza kwa  kuwa na ajali nyingi za barabarani kwa miaka mitatu mfululizo kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 zilizosababisha vifo vya watu pamoja na majeruhi.
Taarifa hiyo imetolewa leo bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Hamad Yusuf Masauni wakati akijibu swali la Mbunge wa Biharamulo Magharibi Mhe. Oscar Rwegasira  kuhusu kuongezeka kwa vifo vitokanavyo na ajali za barabarani.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Mhe. Masauni kwenye taarifa hiyo Jiji la Dar es Salaam limeongoza kwa kuwa na ajali 18,506 kati ya ajali 46,539 zilizotokea nchi nzima kwa kipindi cha mwaka 2013 hadi 2015.
“Takwimu za nchi nzima zinaonesha kuwa Mwaka 2013 zilitokea ajali 23,842 zilizosababisha vifo 4,002 na majeruhi  20,689. Mwaka 2014 zilitokea ajali 14,360 zilizosababisha vifo 3,760 na majeruhi 14,530 na mwaka 2015 zilitokea ajali 8,337 zilizosababisha vifo 3,468 na majeruhi 9,383.” alisema Masauni.
Mhe. Masauni alieleza kuwa kwa mwaka 2013 Mkoa wa Kipolisi Kinondoni uliongoza kwa kuwa na ajali zipatazo 6,589 ukifuatiwa na Mkoa wa Kipolisi Ilala uliokuwa na ajali 3,464 wakati Mkoa wa Simiyu na Tanga kulikuwa na ajali chache ambapo Simiyu zilitokea ajali 67 na Tanga ajali 96.
Mwaka 2014 Kinondoni na Ilala ziliongoza tena kwa kuwa na ajali 3,086 zilizotokea  Kinondoni  na Ilala ajali 2,516 na mikoa iliyokuwa na ajali chache ni Simiyu ajali 55 na Kagera ajali 29.
Aidha, Mhe. Masauni alisema kuwa mwaka 2015 Mkoa wa Kipolisi Ilala uliongoza kwa kuwa na ajali nyingi za barabarani ambapo ajali 2,516 zilitokea mkoani humo ikifuatiwa na Temeke uliokuwa na ajali 1,420 wakati mikoa ya Rukwa na Arusha ilikuwa na ajali chache.
Mhe. Masauni alibainisha kuwa mfumo endelevu wa wazi uliopo wa kutoa takwimu  hizo ni kupitia taarifa za mwaka za Jeshi la Polisi (Polisi Annual Report) ambapo kila mtanzania anaweza kupata taarifa hizo za ajali.

SERIKALI KUJENGA NYUMBA 9500 KWA AJILI YA ASKARI MAGEREZA

images 
Na Fatma Salum- MAELEZO, Dodoma.
Serikali kupitia jeshi la Magereza imesaini Mkataba na Kampuni ya Poly Technologies ya China kujenga nyumba 9,500 kwenye vituo vyote vya Magereza nchini.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Hamad Yusuf Masauni wakati akijibu swali kuhusu kuboresha makazi ya askari lililoulizwa na Mhe. Devota Minja (Mb) leo bungeni mjini Dodoma.
Mhe. Masauni alibainisha kuwa  kupitia mkataba huo Serikali itapunguza kwa kiasi kikubwa changamoto iliyopo ya uhaba wa nyumba kwa ajili ya askari wa jeshi hilo ambapo mahitaji kwa sasa ni nyumba 14,500 wakati zilizopo ni nyumba 4,221 hivyo kupelekea upungufu wa nyumba 10,279.
“Serikali inafahamu kuwa lipo tatizo la baadhi ya askari wa Jeshi la Magereza na Polisi kuishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi, hivyo katika kukabiliana na tatizo hili Serikali imeendelea kuzifanyia ukarabati mkubwa baadhi ya nyumba na pia kujenga nyumba mpya”. Alisema Masauni.
Mhe. Masauni alifafanua  kuwa mgawanyo wa ujenzi wa nyumba hizo mpya ni Makao Makuu ya Magereza nyumba 472, Arusha nyumba 377, Dar es Salaam nyumba 952, Dodoma 356, Kagera 364, Kigoma 272, Kilimanjaro 390, Lindi 233, Manyara 206, Mara 378, Mbeya 622, Iringa 336, Morogoro 669, Mtwara 215, Mwanza 398, Pwani 384, Rukwa 358, Ruvuma 320, Shinyanga 337, Singida 299, Tabora 408, Tanga 382, KMKGM Dar es Salaam 219, Chuo cha Ukonga 115, Chuo cha Kiwira 183, Chuo cha Ruanda 62, Chuo KPF 27, Bohari Kuu 82 na Bwawani nyumba 84.
Aidha, Mhe. Masauni aliongeza kuwa kwa upande wa Jeshi la Polisi, Serikali inakusudia kujenga nyumba 4,136 katika mikoa 17 ya Tanzania Bara na Zanzibar zitakazosaidia kupunguza tatizo la makazi kwa askari wa jeshi hilo.
Mhe. Masauni alilieleza bunge kuwa Serikali itaendelea kutatua changamoto ya uhaba wa nyumba kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo mikopo yenye riba nafuu, Miradi Shirikishi (PPP) na kwa kutumia fedha za bajeti ya Serikali kadri hali ya uchumi itakavyokuwa inaimarika.

MWENYEKITI WA MTAA WA BABALE ULIOPO WILAYA YA NYAMAGANA AUAWA KWA KUPIGWA RISASI NA WATU WASIOFAHAMIKA WAKATI AKIELEKEA NYUMBANI KWAKE.

msa1
MNAMO TAREHE 22.05.2015 MAJIRA YA SAA 20:00HRS KATIKA MTAA WA BULALE KATA YA BUHONGWA WILAYA YA NYAMAGANA JIJI NA MKOA WA MWANZA, MWENYEKITI WA MTAA WA BUBALE ALIYEFAHAMIKA KWA JINA LA ALPHONCE MUSSA NYINZI MIAKA 48, MSUKUMA MFANYABIASHARA NA MKAZI WA BULALE ALIUAWA KWA KUPIGWA RISASI KIFUANI NA KUTOKEA CHINI YA KWAPA UPANDE WA KULIA NA WATU WAWILI WASIO FAHAMIKA. RISASI HIYO PIA ILIMJERUHI NEEMA MARANGULA MIAKA 23 MKAZI WA BULALE KATIKA KIGANJA CHA MKONO WA KULIA.
INAELEZWA KWAMBA SIKU HIYO JIONI ALIKUA AMETOKA KWENYE KIKAO ALICHOFANYA NA WAJUMBE WA KAMATI YA ULINZI NA USALAMA WA MTAA WA BULALE, KATIKA MUDA WA SAA 20:00HRS USIKU AKIELEKEA NYUMBANI AKIONGOZANA NA WAJUMBE WAWILI ALIKUTANA NA NEEMA MARANGULA AKIWA NA MUME WAKE AMBAO WALIKUA WANAWAFUATA MAREHEMU NA BALOZI KWA AJILI YA KUZUNGUMZIA MZOZO WA NDANI YA NDOA YAO KWA HIYO WALIKUA WANAHITAJI KUSULUHISHWA, MAREHEMU NA WAJUMBE WAKE WAWILI WAKIWA PAMOJA NA BI NEEMA PAMOJA NA MUMEWE WAKIWA WANAJADILI TATIZO HILO HAPO BARABARANI MARA GHAFLA WAKATOKEA WATU WAWILI AMBAO WALIKUA WAKIPITA BARABARANI NA KUWAAMBIA MKO CHINI YA ULINZI NA MMOJA WAO AKATOA BUNDUKI NA KUMPIGA RISASI MAREHEMU AMBAYE ALIANGUKA CHINI HUKU WENZAKE WAKIKIMBIA KUJIOKOA KUTOKA ENEO HILO LAKINI PIA WALE WAHALIFU  WAKAKIMBIA NA KUTOKOMEA GIZANI VICHAKANI.
NDIPO WANANCHI WA ENEO HILO WALIJITOKEZA KWA MSAADA WA KUMSAIDIA MAREHEMU, WALIMCHUKUA MAREHEMU KUMKIMBIZA HOSPITALI KWA MATIBABU LAKINI ALIFARIKI DUNIA WAKIWA NJIANI. MAJERUHI BI NEEMA MARANGULA AMELAZWA HOSPITALI YA MKOA WA MWANZA SEKOU TOURE KWA MATIBABU NA HALI YAKE INAENDELEA VIZURI. MWILI WA MAREHEMU UPO HOSPITALI MKOA WA MWANZA SEKOU TOURE KWA AJILI YA UCHUNGUZI WA DAKTARI. CHANZO CHA MAUAJI HAYO BADO HAKIJAFAHAMIKA, UCHUNGUZI TUKIO HILO BADO UNAENDELEA.
KAMANDA WA POLISI MKOA WA MWANZA KAMISHINA MSAIDIZI MWANDAMIZI WA JESHI LA POLISI AHMED MSANGI  ANAWAOMBA WANANCHI WENYE TAARIFA ZOZOTE KUHUSIANA NA TUKIO HILO ZITAKAZO SAIDIA KUFANIKISHA KUKAMATA WAHUSIKA WAZITOE  POLISI LAKINI PIA KUTOA USHIRIKIANO KWA VIONGOZI WAO NA KUHAKIKISHA WANATENGENEZA MAKAZI SALAMA HUKO WANAPOISHI NA MAENEO YA SHUGHULI ZAO. MSAKO MKALI UNAFANYIKA NA KUHAKIKISHA WAHUSIKA WA TUKIO HILO WANAKAMATWA.
IMETOLEWA NA:
SACP: AHMED MSANGI
KAMANDA WA POLISI MKOA WA MWANZA

MATUKIO MBALIMBALI YA PICHA KUTOKA BUNGENI DODOMA

index 
Mbunge wa CCM, Mhe. Mary Mwanjelwa akiwasili viwanja vya Bunge mjini Dodoma kuhudhuria vikao ndani ya Bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
1Mwenyekiti wa Bunge Mhe Najma Murtaza Giga akiwasili Bungeni kuongoza vikao vya Bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
2 
Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Mhe. Ally Keissy akiwasili viwanja vya Bunge mjini Dodoma kuhudhuria vikao ndani ya Bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
3 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye (kulia) akiwa ameongozana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Jumanne Maghembe wakielekea Bungeni kuhudhuria vikao vya bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
4 
Naibu Waziri, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Masiliano, Mhe. Eng. Edwin Ngonyani akiwasili viwanja vya Bunge mjini Dodoma kuhudhuria vikao ndani ya Bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
5 
Naibu Waziri, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Hamis Kingwangalla akiwasili viwanja vya Bunge mjini Dodoma kuhudhuria vikao ndani ya Bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
6 
Naibu Waziri, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Eng. Hamad Masauni (kushoto) akiwa ameongozana na Mbunge wa Viti Maalum CCM, Mhe. Halima Bulembo wakiwasili viwanja vya Bunge mjini Dodoma kuhudhuria vikao ndani ya Bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
7 
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Selemani Jafo akiwasili viwanja vya Bunge mjini Dodoma kuhudhuria vikao ndani ya Bunge hilo leo 23 Mei, 2016 mjini Dodoma.
PICHA ZOTE NA BENEDICT LIWENGA, MAELEZO-DODOMA.

MBUNGE MWIGULU NCHEMBA AANZA KUTIMIZA AHADI ZAKE JIMBONI IRAMBA


Mbunge  wa  jimbo la Iramba Bw Mwigulu  Nchemba  wa  pili  kushoto  akikabidhi bati  zaidi ya 450 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba  za walimu ,zahanati na nyumba  vya madarasa
Wananchi  wa   jimbo la  Iramba  wakimpongeza mbunge wao Bw Nchemba kwa  utekelezaji wa ahadi zake
Na MatukiodaimaBlog  ……………………………………………………..
MBUNGE wa  jimbo la  Iramba wilayani Iramba mkoani Singida Bw Mwigulu Nchemba  ameendelea  kufanya mikutano ya  kuwashukuru  wananchi  wake  kwa  kumchagua  kwa  kishindo  katika  uchaguzi mkuu mwaka 2015 kwa  kutekeleza ahadi  mbali mbali  alizopata kuwaahidi  wakati wa kampeni .
 
Mbunge Nchemba  amekabidhi  bati  hizo  jana  wakati wa mikutano yake ya  kuwashukuru  wananchi wake wa  jimbo la Iramba kwa kumchagua na kuanza utekelezaji wa ahadi  zake.
Alisema   kuwa  lengo la  kuanza  kukabidhi ahadi  zake ni  kuwafanya wananchi kuharakisha  ukamilishaji wa  shughuli za kimaendeleo jimboni hasa katika nyanja ya  elimu  na afya  na kuwa  bati  hizo  zitasaidia  ujenzi wa vyumba  vya  madarasa ,nyumba za  walimu na  Zahanati  .
Kwani  alisema ndoto  yake ya mbeleni   ni kuona jimbo la Iramba na  wilaya ya Iramba  inaendelea  kuwa mbele katika ubora wa vyumba  vya madarasa na  wengine  kufika  kujifunza Iramba
Hivyo  alisema pamoja na  kuchangia  bati  kwa  ajili ya ujenzi  huo bado atajitolea  kununua  tofari  za  kujengea ambazo kwa  kila kijiji  vijana  watafyatua na yeye atazinunua kwa  bei ambayo  wao  watataka  kama  sehemu ya  kutoa ajira kwa vijana  vijijini pia vifaa vyote  vya  viwandani kwa ajili ya ujenzi wa miradi hiyo  ni juu yake wananchi wanachotakiwa kufanya ni  kushiriki katika shughuli za  kimaendeleo .
Pia  aliwataka  walimu na  watumishi  wanaopangwa  kufanya kazi katika  wilaya  ya  Iramba  kujenga  utamaduni wa kupenda  kufanya kazi katika wilaya  hiyo  badala ya  kuripoti na kuondoka .
Nchemba ambae ni waziri wa  kilimo ,mifugo na uvuvi  alisema  kuwa vipaumbele  vyake  kwa  wananchi wake ni maji na umeme ambavyo tayari umeme  umeanza  kusambazwa  vijijini  pia maji anaendelea  jitihada japo  alisema suala la Miundombinu bado ni  changamoto .
Wakati  huo  huo waziri Nchemba ameshauri  uongozi wa Halmashauri  kuruhusu  wanafunzi wanaopata matatizo ya ugonjwa wakiwa shuleni  kupatiwa matibabu ya  bure katika  vituo  vya afya ,Hospitali na zahanati katika  jimbo  hilo  badala ya  kuwarudisha  nyumbani .
Alisema kuna haja ya Halmashauri  kupitia  vyanvzo  vyake  vya ndani  kusaidia  kuwalipia matibabu   wanafunzi hao na kuwa  ofisi yake  itasaidia   kufidia pesa  hizo kwa  kugharamia baadhi ya  miradi ambayo inapaswa  kutekelezwa na Halmashauri kama ambavyo anafanya sasa kwakujitolea kujenga vyumba vya madarasa na  Zahanati .

TAARIFA YA MWENENDO WA UGONJWA WA KIPINDUPINDU NCHINI ILIYOTOLEWA NA MHE. UMMY MWALIMU

logo 
Serikali kupitia Wizara yangu inaendelea na utaratibu wa kutoa taarifa ya mwenendo wa mlipuko wa ugonjwa wa Kipindupindu nchini kila wiki kama tulivyoahidi. Takwimu za ugonjwa huu zinaonyesha kuwa hadi kufikia tarehe 22 Mei 2016, kulikuwa na jumla ya wagonjwa 21,585  ambao wametolewa taarifa ya kuwa na ugonjwa huu, na kati ya hao, ndugu zetu 338 wamepoteza maisha.
Tumefarijika kuona takwimu za wiki iliyopita kuanzia tarehe 16 hadi 22 Mei 2016 zinazoonyesha kuwa, kasi ya ugonjwa wa kipindupindu imepungua kwa asilimia 49 (karibu nusu ya wagonjwa), ambapo idadi ya wagonjwa wapya walioripotiwa ni 108, na hakuna aliyepoteza maisha, ikilinganishwa na wagonjwa wapya 212 walioripotiwa wiki iliyotangulia ya Mei 9 hadi 15.
Mikoa ambayo imeripoti wagonjwa wiki hii ni Morogoro (47), Manyara(16), Lindi (14), Mara (11) Dar es Salaam (9), Pwani (6), Kagera (2), Kilimanjaro (2) na Iringa (1).
Halmashauri zilizoongoza kutoa wagonjwa wengi ni Kilosa (27),  Mvomero (15), Kilwa (14), Tarime Mjini (11), Babati Vijijini (10), Kinondoni (9), Babati Mjini (5), Morogoro Mjini (5), Kibaha Mjini (4), Bukoba Mjini (2), Chalinze (2), Same (2), Iringa Mjini (1) na Mbulu (1).
Katika wiki iliyopita, mikoa ambayo haikuwa na wagonjwa wa kipindupindu ni Kigoma, Dodoma, Mwanza, Geita, Singida, Shinyanga, Arusha, Tanga, Tabora, Rukwa, Katavi, Mbeya, Simiyu na Mtwara. Na mikoa ambayo haijawahi kuripoti mgonjwa wa kipindupindu tangu mlipuko uanze ni Ruvuma na Njombe
Kupungua kwa idadi ya wagonjwa kusirudishe nyuma juhudi za kuuzuia ugonjwa huu, bali tunatakiwa kuzidisha jitihada ili tuweze kuuondoa, tusiwe na wagonjwa kabisa. Ni vema kuchukua tahadhari zaidi, hasa katika msimu wa masika, ambapo kuna uwezekano mkubwa wa maji ya mvua kusambaza vimelea vya ugonjwa huu. Tuendelee kuzuia maambukizi, na pia kuendelea kutoa taarifa za ugonjwa kila siku, hata kama hakuna wagonjwa, na kusimamia kikamilifu hatua mbalimbali za udhibiti wa mlipuko huo

TBC yafanikiwa kufanya upembezi yakinifu wa kufunga mitambo ya FM eneo la Mbambabay.

index 
Na Benedict Liwenga, MAELEZO, Dodoma.
SHIRIKA la Utangazaji la Taifa (TBC) limefanya upembuzi yakinifu wa kufunga mitambo ya FM yenye uwezo wa Kilowati moja katika eneo la Mbambabay Wilayani Nyasa Ili kuongeza usikivu wa Redio za TBC.
Kauli hiyo imetolewa leo Bungeni Dodoma na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye wakati akijibu swali la Mbunge wa Mbinga Vijijini, Mhe. Martin Msuha aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuongeza uwezo wa kurusha matangazo ya Kituo cha TBC Songea ili wananchi wa tarafa hizo wapate habari kupitia TBC.
Mhe. Nape ameeleza kuwa Matangazo ya Redio ya Taifa kupitia mtambo wa masafa ya kati yaani ‘’Medium Wave’’ wenye nguvu ya Kilowati 100 yalikuwa yakisikika vizuri katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Ruvuma wakati mtambo huo ulipokuwa ukifanya kazi.
‘’Tangu mwezi Julai, 2013 mtambo huo haufanyi kazi kutokana na uchakavu na hivyo kuathiri usikivu wa matangazo ya TBC katika maeneo kadhaa”, alisema Mhe. Nape.
Alisema kwamba, kwa kutambua umuhimu wa Wananchi katika kupata matangazzo, TBC ililazimika kuhamisha mitambo yake miwili ya Redio yenye uwezo wa Kilowati moja kwa kila moja iliyokuwa imefungwa eneo la Mshangano, Songea na kuifunga eneo la juu la mlima wa Matogoro-Songea ili usikivu Wake usambae katika eneo kubwa zaidi.
‘’Baada ya kufunga mitambo hiyo, matangazo ya TBC Songea yameboreshwa”, aliongeza Mhe. Nape.
Ameongeza kuwa katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2016/17 Wizara yake imetenga fedha za maendeleo kwa ajili ya kufunga mtambo eneo la Mbambabay.
‘’Kazi hiyo ya uboreshaji wa matangazo katika eneo Hilo itaanza mara tu fedha za kununua na kufunga mitambo hiyo zitakapotolewa”, alisema Mhe. Nape.
Aidha, alisema kwamba kutokana na uwezo mdogo wa mitambo ya FM inayotumika kwa sasa, mawimbi yake ya sauti hayafiki mbali sana ukilinganisha na yale ya mitambo ya ‘’Medium Wave’’ iliyokuwa ikitumika awali ambayo yanafika eneo kubwa zaidi la Mkoa wa Ruvuma zikiwemo Tarafa za Hagati, Mbuji na Mkumbi.
‘’Kukabiliana na changamoto za usikivu hafifu katika maeneo kadhaa Mkoani Ruvuma, TBC imeshafanya upembuzi yakinifu wa kufunga mitambo ya FM yenye uwezo wa Kilowati moja katika eneo la Mbambabay Wilayani Nyasa Ili kuongeza usikivu wa Redio za TBC,”alisema Mhe. Nape.

WAZIRI NCHEMBA ATUMBUA MAJIPU JIMBONI KWAKE AVUNJA BODI YA MAJI ILIYOFANYA UFISADI WA MAMILIONI

Waziri  wa  kilimo , mifugo na uvuvi Bw Mwigulu Nchemba  akipokelewa na  wananchi wa  kata ya Tulia jimboni kwake  Iramba jana
Waziri Mwigulu  akilakiwa na  wapiga kura  wake wakati wa mikutano yake ya kuwashukuru
Waziri Nchemba  akiwapungia mikono wananchi wake
waziri Nchemba  akiteta jambo na mmoja kati ya  walemavu katika  kata ya Tulia jimboni Iramba
Waziri wa  kilimo ,chakula na uvuvi Bw Mwigulu Nchemba  akitangaza  kuwasimamisha kazi viongozi wa bodi ya maji Mingela Iramba  kwa ufisadi wa mamilioni ya maji

WASIFU WA TIMU ZA MEXCO, ARGENTINA NA CHILE KABLA YA KOMBE LA COPA AMERICA

CHI1 
Timu ya taifa ya Chile ni maarufu kama “La Roja”. Timu hii ilitengeneza historia kwa mara ya kwanza mwaka jana ilipoifunga Argentina magoli 4-1 katika fainali ya Copa America na kuchukua ubingwa wa ligi hiyo tangu kuanziashwa kwa Ligi hii.
Timu ya taifa ya Chile “La Roja” yenyewe iko kwenye kundi D ikijumuishwa na timu za taifa za Panama, Bolivia na Argentina, bado hili ni moja kati ya kundi gumu kwenye michuano ya mwaka huu. Je itafanikiwa kuingia fainali mwaka huu na hata kuchukua ubwingwa tena katika kombe hili? Majibu yote tutayapata katika Copa America 2016 StarTimes pekee
CHI2
Timu ya taifa ya Mexico ni maarufu kama “El Tri”, ni timu yenye historia ya kipekee kwenye fainali za kombe la dunia. Imeshiriki mara 14, haijawahi kushinda taji hili, iko katika nafasi ya 19 kwenye viwango vya FIFA
Katika copa America iko kundi C ambalo ni kundi gumu haswa! Ikiwemo Uruguay, Jamaica na Venezuela. Mwaka 1991 ilifanikiwa kuingia fainali na kucheza na Argentina lakini wakagonga mwamba na kupigwa bao 2-1. Hivyo hivyo kwa mwaka 1999 ilipocheza na Colombia katika fainali na kupigwa 1-0.
Je mwaka huu watajitahidi kuchukua ubingwa? Yote utayapata StarTimes
CHI3 
Argentina ni nchi inayopatikana barani America ya kusini. Mwaka jana timu hii ilifanikiwa kuingia katika fainali na kutolewa na mabingwa Chile waliochukua ushindi wa bao 4-1 katika kombe la COPA America na kuifanya chile iibuke kidedea katika fainali hiyo. Mwaka huu Argentina itashiriki katika mashindano ya Copa America, bila kumsahau kiungo mchezaji Messi ndani, je watafanikiwa kuingia katika fainali au hata kuchukua Ubingwa? StarTimes tutarusha mechi zote LIVE ndani ya channel za michezo 

Samatta sasa kupewa eneo Juni 5

MZ1Mwenyekiti wa SHIWATA, Cassim Taalib (aliyesimama) akizungumza na wanachama (hawapo pichani) maandalizi ya sherehe za kumkabidhi eneo mchezaji bora wa Afrika , Mbwana Samatta katika mkutano uliofanyika Dar es Salaam juzi
MZ2 
Mwigizaji maarufu nchini, Ahmed Olotu maarufu kama mzee Chilo akizungumza na wanachama wenzake wa SHIWATA katika mkutano huo
……………………………………………………………………………………………………………….
Na Mwandishi Wetu
MTANDAO wa Wasanii Tanzania (SHIWATA) umesogeza mbele kwa siku moja sherehe za kumkabidhi eneo mchezaji bora wa Afrika, Mbwana Samatta hadi Juni 5, 2016 ili kupisha pambano kati ya Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) na timu ya Taifa ya Misri.
Mwenyekiti wa SHIWATA, Cassima Taalib alisema jana Dar es Salaam kuwa  maandalizi ya sherehe hizo ambazo awali zilipangwa kufanyika Juni 4, 2016 yamekamilika na Mbwana atakabidhiwa hekari tano za eneo ambazo atalitumia kujenga Kituo cha wanamichezo katika eneo la Mwanzega, Mkuranga mkoa wa Pwani.
Alisema hivi karibuni baba mzazi wa mchezaji huyo, Mzee Ali Samatta alishukuru SHIWATA kutambua mchango wa mwanae katika medani ya soka nchini na kuahidi kusaidia kusimamia juhudi za mwanae katika kuendeleza michezo nchini.
Mkurugenzi wa Ufundi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Salum Madadi alithibitisha kufanyika mchezo wa Stars na Misri siku ambayo awali ilipangwa Mbwana kukabidhiwa eneo hilo.
Samatta anayecheza soka ya kulipwa Ulaya atatumia mapumziko ya mechi ya Stars na Misri kukabidhiwa eneo hilo na kadi ya uanachama wa SHIWATA katika kutambua mchango wake kuitangaza Tanzania kuwa mchezaji bora Afrika kati ya wachezaji wanaocheza mpira wa kulipwa ndani ya bara la Afrika.
Katika sherehe hizo wasanii 35 watakabidhiwa nyumba zao kati hiyo, wanachama watatu watakabidhiwa nyumba ndogo, 31 watakabidhiwa misingi na nyumba kubwa moja na kufikia idadi ya nyumba 185 ambazo zimekwisha jengwa kijijini hapo mpaka sasa.
Akizungumza katika mkutano wa wanachama kujiandaa na sherehe hizo walimuomba Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Mnauye awe mgeni rasmi ambapo pia waliomba dua la kumuombea Rais John Pombe Magufuli katika juhudi zake za kupambana na wabadhirifu wa mali ya umma.

MKUU WA MKOA WA KILIMANJARO SAID MECKY SADICK AFANYA ZIARA MAMLAKA YA MAJI SAFI NA USAFI WA MAZINGIRA MJINI MOSHI (MUWSA)

Mkuu wa Mko wa Kilimanjaro,Said Mecky Saidick akiwa ameongozana na Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) John Ndetico (mwenye tai) alipofanya ziara katika mamlaka hiyo .
Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) John Ndetico akitoa taarifa ya Mamlaka hiyo kwa Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Said Mecky Sadick alipotembelea ofisi za MUWSA.
Baadhi ya Viongozi wa Serikali pamoja na Wakuu idara katika Mamlaka ya maji safi na Usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) wakisikiliza kwa makini taarifa iliyokuwa ikitolewa.
Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro na viongozi wengine wakiwa katika chanzo cha maji cha Nsere .
Chanzo cha Maji cha Nsere ambacho kiwango cha maji kinatajwa kushuka kutoka lita za ujazo Milioni 12 hadi Milioni 9.5.
Mkuu wa mkoa Saidi Mecky Sadick akitembelea maeneo ya chanzo hicho.
Mkuu wa Mko wa Kilimanjaro,Said Mecky Saidick akiwa ameongozana na Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) John Ndetico (mwenye tai) alipofanya ziara katika mamlaka hiyo .
Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) John Ndetico akitoa taarifa ya Mamlaka hiyo kwa Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Said Mecky Sadick alipotembelea ofisi za MUWSA.
Baadhi ya Viongozi wa Serikali pamoja na Wakuu idara katika Mamlaka ya maji safi na Usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) wakisikiliza kwa makini taarifa iliyokuwa ikitolewa.
Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro na viongozi wengine wakiwa katika chanzo cha maji cha Nsere .
Chanzo cha Maji cha Nsere ambacho kiwango cha maji kinatajwa kushuka kutoka lita za ujazo Milioni 12 hadi Milioni 9.5.
Mkuu wa mkoa Saidi Mecky Sadick akitembelea maeneo ya chanzo hicho.

WEMA AZINDUA MOBILE APLICATION YAKE, HABARI ZAKE ZITAPATIKANA HUMO

1 
 Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Nnauye pamoja na  Miss Tanzania 2006 na Muigizaji maarufu wa Filamu nchini Wema Sepetu wakifunua pazia  kuashiria uzinduzi rasmi wa Wema Sepetu Mobile Application ya msanii Wema Sepetu  kwenye hoteli ya Hyyat Regency jijini Dar es salaam jana , Katika Aplication hiyo kutapatikana habari mbalimbali za msanii huyo mwigizaji wa filamu pamoja na habari zinazohusu masuala mbalimbali ya kazi zake hii ni kwa mara ya kwanza katika nchi za Afrika Mashariki kwa msanii kuwa na Mobale Aplication yake hivyo msanii mwingine atakayekuja atakuwa anafuata nyayo za Wema Sepetu.
2 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Nnauye akimpongeza msanii  Wema Sepetu mara baada ya kuzindua Mobile Application ya msanii huyo jana.
3 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Nnauye akihutubia wakati wa uzinduzi wa Wema Sepetu Mobile Application ambapo alimpongeza Wema kwa hatua kubwa aliyofikia ya kuwa msanii wa kwanza wa Filamu nchini kuwa na Mobile App na kuwataka wasanii wengine kuwa wabunifu na kuja na mipango ambayo itawanufaisha zaidi.
4 
Msanii wema Sepetu akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mobale Aplication yake kwenye hoteli ya Hyyat Regency.
6 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Nnauye akimpongeza msanii  Wema Sepetuwakipiga picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi huo.
7 
Mtaalamu wa Mobile Application Ndugu Haji Yussuf akizungumza wakati wa uzinduzi wa Wema Sepetu Mobile Application
8 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Nnauye akizungumza jambo na Miss Tanzania 2006 na Muigizaji maarufu wa Filamu nchini Wema Sepetu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Nnauye akipiga picha ya pamoja na Miss Tanzania 2006 na Muigizaji maarufu wa Filamu nchini Wema Sepetu 
9 
Mama yake Wema Sepetu pamoja na baadhi ya wageni waalikwa wakijiunga na huduma hiyo.
11 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Nnauye akipiga picha ya pamoja na Miss Tanzania 2006 na Muigizaji maarufu wa Filamu nchini Wema Sepetu na mama yake kushoto pamoja Mkurugenzi wa Biashara wa kampuni ya Hartman Traders Ndugu Cecil  na Mtaalamu wa Mobile Application Ndugu Haji Yussuf wa pili kutoka kushoto wakati wa uzinduzi wa mobile Application yake ambayo itawasaidia wapenzi na mashabiki wake kupata habari sahihi na za uhakika.

No comments :

Post a Comment