Wanachama wachimba madini
wadogo wadogo kutoka katika sekta isiyo rasmi wakifurahia na kinga dhidi ya
majanga kwa kunufaika na mafao yote yatolewayo na mfuko wa taifa wa hifadhi ya
jamii NSSF. Utafiti wa hivi karibuni unaonesha ya kuwa mifuko ya hifadhi ya jamii
nchini imeweza kuwafikia wakulima na wachimbaji wa madini ambapo hadi sasa
wachimbaji madini zaidi ya 7,000
wamejiunga na baadhi ya mifuko ya hifadhi ya jamii. Picha na mtandao
Christian Gaya Mwananchi Alhamis, Octoba 2015
Idadi
kubwa ya watanzania bado wanaamini ya kuwa hifadhi ya jamii ni stahili ya
wafanyakazi waajiriwa tu, tena wafanyakazi wale wa kipato kikubwa. Ambapo kabla
ya kuwa na sera ya hifadhi ya jamii na msimamizi na mdhibiti wa hifadhi ya
jamii na kabla ya mabadiliko ya sheria za hifadhi ya jamii na maendeleo ya
mifuko ya hifadhi ya jamii kuwa mifuko kamili ya hifadhi ya jamii, sheria
nyingi zilikuwa haziwajumuishi wafanyakazi kutoka katika sekta isiyo rasmi
sheria hizo zilizokuwa zimepitwa na wakati zilishughulika na wafanyakazi
walioajiriwa na kupata mshahara kwa mwezi tu.
Hifadhi ya jamii ni haki ya kila Mtanzania. Haki hii imeanishwa katika Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 11(1) na Sera ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2003.
Haki hii pia imeiainishwa kwenye mkataba wa kimataifa wa haki za
binadamu wa mwaka 1948 pamoja na mikataba ya shirika la kazi duniani (ILO)
ibara ya 102 ya mwaka 1952.
Hivyo
ni jukumu la mifuko kuondoa fikra ndani ya vichwa vya idadi kubwa ya watanzania
kwa kuwaelemisha ya kuwa hivi sasa hifadhi ya jamii haina ubaguzi wa aina
yeyote, kwa sasa hifadhi ya jamii ni fursa huru kwa wote, kwa walioajiriwa na
kwa wale waliojiajiri. Mifuko ya hifadhi ya jamii inatakiwa kujipanga kwa
makusudi ya kuhakikisha ya kuwa inawaelemisha wananchi wote walio kwenye sekta
isiyo rasmi na hata watu binafsi kuwawekea utaratibu wa wao kujiunga, kuchangia
na kunufaika na mafao pamoja na vivutio vinavyotolewa na mifuko hii. Mifuko
inatakiwa kuonesha kwa vitendo na mifano hai ya wakulima, wanafunzi, wavuvi na
wajasiriamali namna wanavyochangia na wanavyofaidika huko mijini na vijijini.
Inajulikana
ya kuwa watanzania wanatambua ya kuwa wengi katika sekta ya kilimo na sekta
isiyo rasmi ambao kwa vipato vyao wanavyopata wangeweza kujiunga na mifuko
nchini. Uzoefu huu unashawishi kuwa mifuko hii sasa itazame katika sekta ya
kilimo. Kilimo ndio sekta mama ya uchumi wetu na mpaka sasa inaajiri zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wetu, lakini
ukuaji wake ni asilimia 4.4
ambayo ni chini ya kiwango kinachotakiwa cha asilimia 6 kwa mwaka kutokana na kukosa uwekezaji wa kutosha. Ndio
sababu, pamoja na kasi nzuri ya ukuaji wa uchumi ya wastani wa asilimia 7, umasikini umepungua kwa asilimia mbili tu.
Utafiti
wa hivi karibuni unaonyesha ya kuwa mifuko hii kwa mipango yao mbalimbali ya
hifadhi ya jamii imeweza kuwafikia wakulima na wachimbaji wa madini ambapo hadi
sasa wakulima 29,000
wachimbaji madini 7,000
wamejiunga na baadhi ya mifuko ya hifadhi ya jamii nchini na wanafaidika na
mafao yanayotolewa yakiwemo ya muda mrefu na ya muda mfupi ikiwemo na mikopo ya
gharama nafuu. Kwa takwimu hizi za utafiti inaonyesha ya kwamba wananchi wengi
wamekosa elimu ya hifadhi ya jamii na taarifa sahihi juu ya utendaji wa mifuko
hii ya hifadhi ya jamii hapa nchini.
Hifadhi
ya jamii katika nchi hii si jambo jipya au la kigeni, hata katika jamii zetu
kabla ya kuja kwa mifumo hii rasmi ya hifadhi ya jamii, kulikuwepo na utaratibu
wa jamii kujiwekea mifumo ya hifadhi ya jamii isiyo rasmi na mpaka sasa
inafanya kazi vizuri na kutoa huduma nzuri ya kinga ya hifadhi ya
jamii. Katika jamii zetu kulikuwepo na utaratibu wa kuwahudumia wazee,
wasiojiweza na watoto mpaka leo ndani ya makabila na familia zetu za kitanzania
bado zinaendelea kutoa huduma hizi za hifadhi ya jamii ingawa kwa kiasi fulani
zimeathiriwa na ujio wageni na nguvukazi kubwa kuhamia mijini kutafuta kazi za
kuajiriwa. Mtu hakupoteza heshima na thamani yake katika jamii kwa kuwa
amepoteza uwezo wake wa kuchangia katika jamii, ama kwa kustaafu, kwa ajali au
kwa kutojaaliwa uwezo wa kuchangia
.
Mabadiliko ya kidunia yameifanya mifumo hii ya
hifadhi ya jamii isiyo rasmi sasa isiweze kuhimili jukumu hilo la kutoa kinga
ya hifadhi ya jamii kwa wale wazee, akina mama wajawazito, walemavu, wajane,
wagane, watoto yatima, na wengineo. Hivyo, mifuko ndio mbadala na salama ya
ustawi wa jamii na utu wake au mtu katika dunia ya leo kuanzia tumboni mwa mama
yake, utotoni, ujana, mpaka utu uzima. Utafiti unaonyesha ya kuwa mara nyingi
shida na majanga huwafika watu wakati ambao hawajajiandaa vema. Na ikumbukwe
wazi ya kuwa maandalizi ya kustaafu huaanzia pale unapoanza kufanya kazi uwe
umeajiriwa au umejiajiri kwenye sekta iliyo rasmi au isiyo rasmi.
No comments :
Post a Comment