Friday, April 3, 2015

Mifuko ya pensheni na hali ya umasikini nchini




Mwanachama wa mfuko wa PSPF na familia yake wakifurahia mafao ya pensheni anayoyapata pamoja na vivutio vingine vinavyotolewa na mfuko huo kwa wanachama wake


Christian Gaya Majira Machi 31, 2015
Hifadhi ya jamii bado inaonekana kuwa kama mkakati mojawapo muhimu unaoweza kuchagia kupunguza umasikini na kuleta maendeleo endelevu nchini.


Lakini kwa Tanzania ambapo uchumi wa sekta isiyokuwa rasmi inazidi......
kuongezeka kuwa kubwa zaidi na sehemu ambayo hata mipango ya miundo mbinu na mikakati ya kuzuia majanga ni mibovu, hivyo kuonekana kuwa na njia ndefu kufikia huko. Umaskini unaongezeka zaidi maeneo ya sehemu za vijijini, kwa matukio ya umaskini wa vijijini ni mkubwa zaidi kuliko umasikini wa mjini.

Ubaguzi wa jinsia nao unaongezeka. Ukiachana mbali na umaskini, watu ambao wanaishi na wako katika maisha hatarishi ni jambo muhimu sana hasa unapozungumzia mambo yanahusiana na hifadhi ya jamii. Maisha hatarishi ni maisha yapoanza kushuka kuwa chini ya mstari wa umasikini



Mafao taslimu yanayotolewa kwa ajili ya mfanyakazi ambaye hajiwezi kwa muda fulani inatakiwa iwe ya kutosha lakini siyo ya juu sana ambayo yanaweza kufanya watu baada ya kupona wasione haja ya kurudi kazini tena haraka iwezekanavyo baada ya kurudia hali yake ya kawaida aliyokuwa nayo kabla ya kuumia     



Viwango vya uchagiaji kwa ajili ya mifuko ya hifadhi ya jamii vinatakiwa siyo tu visiwe kama mzigo kwa wafanyakazi na waajiri lakini ni pamoja na kuhamisha hisa kwa ajili ya vizazi vijavyo, au kutumia ruzuku za mapato ya makusanya ya serikali kwa ajili ya mifuko ya hifadhi ya jamii kwa watu wachache wanaopatiwa huduma ya hifadhi ya jamii



Pamoja na mambo yote yaliyoongelewa hapo juu, kwa watu wanaoishi chini ya msitari wa umaskini, idadi kubwa ya watu wako katika hali hatarishi ya kuwa maskini au wanaelekea kwenye kukutana na umasikini mkubwa na kutisha. Hata ingawa kuna hitaji kubwa, kinga ya hifadhi ya jamii Tanzania ni ndogo sana ukilinganisha na idadi ya watanzania wote. 


Kwa Tanzania hakuna hifadhi ya jamii inayowalinda wananchi wote yaani inayochangiwa kutokana na makusanyo ya kodi ya mapato ya wananchi wenyewe. Hakuna hata jitihada au mikakati ambayo inalenga kusaidia masikini nchini ili angalau hata kuboresha utawala bora na shughuli za sekta za umma, kuwasaidia hata kuwafundisha jinsi ya kutengeneza na kutumia rasilimali zao za asili, kutengeneza na kuwaundia kazi za kufanya, na jinsi ya kujiundia fursa za kujitengezea mapato, hata jinsi ya kufufua au kuboresha mifumo ya kinga za hifadhi ya jamii zile za asili kama vile za kifamilia, za kiukoo, na hifadhi za jamii zingine zisizo rasmi na hata kuboresha na hata jinsi kuwafundisha njia za kufikia huduma muhimu za jamii. Lakini pamoja na hayo kuna baadhi ya mipango ya hifadhi ya jamii inayoendeshwa na serikali, na vile vile na hata na taasisi zisizo za kiserikali na sekta binafsi. 


Kwa sasa, mipango ya hifadhi za jamii zilizo rasmi zaidi hushughulikia makundi ya watumishi wa serikali, askari polisi, jeshi la wananchi, na kwa wale wanaofanya kazi kwenye taasisi za umma na za watu binafsi. Hata hata mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii unaotoa huduma kwa watu ambao wako katika sekta ya kilimo, sekta ya uchumi isiyokuwa rasmi na kwa wale ambao wako sekta rasmi na isiyo rasmi wanaofanya kazi kwa mkataba, na vibarua wengi wao hawajawa wanachama wa mifuko hii ya pensheni ya hifadhi ya jamii. 


Kwa vijana nguvu kazi wote wanapunguzwa na kuondoa michango ya pensheni kabla haijakomaa kuwa pensheni kamili. Ambalo silo lengo kamili la kuanzisha mifumo hii ya hifadhi ya jamii kulingana na kifungu namba 102 cha ILO cha mwaka 1952. 


Cha kushangaza zaidi ni pale serikali kukubaliana na bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania kupitisha sheria ya kutoa michango ya pensheni kabla hayajaiva na mifuko kukubaliana na kutangaza rasmi kuwa na fao la kujitoa ambapo kulingana na mafao yanayojulikana hapa duniani ya hifadhi ya jamii hakuna fao kama hilo la kujitoa ambalo lipo hapa Tanzania. Kuna baadhi ya sekta zisizo rasmi, na za asili, na mipango ya bima ya jamii. Vile vile kuna ubaguzi wa jinsia na hifadhi ya jamii ambayo zaidi mwerekeo wake ni watu wa mjini tu  


Serikali kwa miaka kadhaa imekuwa ikitekeleza mipango ya kuhudumia jamii kwa makundi fulani fulani kwa ajili ya kutengeneza rasilimali na fursa za kazi. Kuna mipango mingine ya ustawi wa jamii kwa makundi. Mojawapo ya kinga za jamii ni kama vile TASAF na baadhi ya taasisi zisizo za kiserikali yaani NGOs na baadhi ya taasisi za kimataifa zinazotoa ruzuku na misaada kwa watu maskini. Lakini bado vijana na wazee wanakosa hifadhi hii ya jamii na kuendelea kukumbwa na maisha hatarishi kama ya kuvamiwa na majanga kama vile matibabu, kifo, ulemavu, uzee, uzazi, kuumia kazini, magojwa yatokanyo na kazi, kukosa kazi, na majanga ya asili. 


Hifadhi za jamii zilizopo na shughuli zao bado hazina uhusiano wa aina yeyote na zina idadi ndogo sana za wanachama, na mafao ya pensheni zao kutokwenda na ukali wa maisha, ingawa utofauti wa jinsi ya kukokotoa mafao ya pensheni ya muda mrefu na mafao ya muda mfupi umerekebishwa hivi karibuni. Wakati shughuli hizi za hifadhi ya jamii zimeleta faida kwa makundi ya watu fulani, lakini ni mara chache sana yamechangia kwenye mikakati ya kuleta mabadiliko ili kuchangia labda lazima yaunganishwe na sera za maendeleo. Utekelezaji wa baadhi ya sekta za uchumi hata baadhi ya mifuko ya hifadhi ya jamii zimekuwa zikifanya vizuri zaidi. 


Lakini hizo faida za ufanisi huo wa kufanya vizuri zaidi mara nyingi umekuwa ukinufaisha watu wachache mno ukilinganisha na idadi ya watanzania waliopo. Na haufananishwi na kuongezekwa kwa ustawi. Hivyo ukuaji wa hifadhi ya jamii au uchumi lazima uunge mkono wa mikakati ya kupunguza umasikini  


Ni kwa bahati mbaya ya kuwa serikali haiwezi kufanya kila kitu kwa ajili ya raia wake. Hivyo na ndio maana kuna taasisi zisizo za kiserikali, za watu binafsi, za kidini na za hifadhi ya jamii ambazo zina wajibu wa kushughulikia mambo kama haya kwa niaba ya serikali kama vile Mashirika  ya umma yanayotoa pensheni yanayoendesha kwa utaratibu wa kanuni za kibima kama vile shirika la taifa la hifadhi ya jamii NSSF, mfuko wa pensheni wa PSPF, mfuko wa mafao ya kustaafu wa GEPF, mfuko wa pensheni wa PPF, mfuko wa pensheni wa LAPF, mfuko wa bima ya afya wa taifa NHIF kwa Tanzania bara na bila kusahau mfuko wa hifadhi ya jamii wa Zanzibar ZSSF kwa upande wa Tanzania visiwani.


Musabila Nyanda ambaye ni mfanyakazi wa wizara ya kilimo makao makuu ni mwanachama hai wa mfuko wa pensheni wa PSPF anasema mwaka jana alipata mkopo kwa ajili ya kukabarabati makazi yake. “Kwa vile nategemea kustaafu mwakani niliona nafuu nikianza kujiandaa kustaafu kwa kuomba mkopo wa nyumba toka PSPF ambapo mimi ni mwanachama wa mfuko huu tangia ulipoanzishwa mwaka 1999.” Musabila Nyanda anasema.



Anasema tangia alipoomba mkopo huo wa kukarabati nyumba yake ilichukua wiki tano tu “Baada ya kufungua maombi yangu ya nyumba baada ya wiki ya tatu nilifika ofisi ya PSPF kuwauliza kama tayari, niliambiwa baada ya wiki mbili watanitaarifu na kweli baada ya wiki mbili nilipigiwa simu ya kuwa mkopo wangu upo tayari” anasema Musabila



Anasema mpaka sasa ameweza kukarabati nyumba yake, na ziada ya pesa ya mkopo iliyobaki anasema ameweza kununulia shamba na kuanzishia biashara yake ambayo mpaka sasa inaendelea vizuri.

Mkopo huu umenisaidia kuanza kuandaa kujipanga vizuri kwa ajili ya kustaafu kwa sababu mwisho wa mwaka ujao nategemea kustaafu kwa maana hiyo mafao yangu nitakayopata hayatetereke hata kidogo na wala sitakuwa na  msongo wa akili kuhusiana na maisha yangu baada ya kuataafu. “Nimeanza kufanya mazoezi ya kustaafu kabla kwa kuanza ujasiriamali na kuandaa makazi yangu ya kudumu” Nyanda anasema  



Mfuko wa PSPF unatoa mikopo ya nyumba kwa ajili ya makazi kwa wanachama wake pamoja na mikopo ya pensheni kwa wale waliostaafu kwa masharti nafuu. Na mkopo huo wa nyumba unatolewa kwa wanachama wake baada ya kuchangia kwa muda wa miaka 5 tu. Na mkopo wa nyumba  zilizojengwa na mfuko wa pensheni wa PSPF unaweza kurejeshwa hadi kwa muda wa miaka 25 Lengo la mkopo ni kumwezesha wanachama kupata nyumba ambazo zimejegwa na mfuko ili kumhakikishia mwanachama kuwa na uhakika wa makazi yake wakati anapoendelea kufanya kazi na baada ya kustaafu. “Mkopo kwa mwanachama wa PSPF aliyechangia chini ya miaka mitano  ambapo atatakiwa kulipia kiasi cha shilingi milioni tano za kitanzania kama malipo ya mwanzo ya nyumba na kiasi kilichobaki anaweza kurejesha hadi muda wa miaka 25. Mwanachama anaweza kununua nyumba kupitia akaunti ya mfuko na kisha kusaini makubaliano kabla ya kuhamishiwa umiliki. 



Mfuko huu wa PSPF ni mfuko pekee unaotoa mkopo wa fedha taslimu kwa mwanachama aliyebakiza miaka 5 kustaafu kwa lazima kwa ajili ya kujenga, kukarabati na kununua nyumba ya makazi popote anapotaka hapa Tanzania, ili kuandaa makazi mazuri mara tu anapostaafu. Na mikopo hii ya pensheni ya kila mwezi huwa inatolewa bila kutozwa riba ambapo mstaafu au mtegemezi ataweza kukopa hadi pensheni ya miezi kumi na miwili bila hata kutozwa riba hata kidogo. 


Nyanda anawashauri wanachama wa mifuko hii ya hifadhi ya jamii kutoondoa mafao yao kabla ya muda wake ili waje wanufaike na mafao ya muda mrefu na mafao ya muda mfupi ikiwa ni pamoja na baadhi ya vivutio mbalimbali vinavyotolewa na mifuko hii ya hifadhi ya jamii nchini pamoja na fursa mbalimbali kama hizi anazozitumia Nyanda kwa sasa kwa sababu mpaka sasa hana wasiwasi na kustaafu mwakani.  “Najisikia kuwa na faraja kubwa sana kuzitumia fursa hizi za mikopo zenye riba nafuu kwa wanachama na wastaafu wa mifuko ya pensheni ya hifadhi ya jamii nchini” Nyanda anasema. 

Anawakumbusha wanachama na wastaafu sehemu za kuwekeza mafao yao ya pensheni kabla ya kupata ushauri wa jinsi ya kuwekeza na badala yake kutumbukiza mafao yote ndani ya shimo refu

No comments :

Post a Comment