Thursday, February 26, 2015

Ujue utawala bora wa mfuko wa mafao ya kustaafu GEPF




Mkurugenzi mkuu wa mfuko wa mafao ya kustaafu Daudi Msangi

Christian  Gaya Majira February 17.2015
Mojawapo ya malengo ya mifuko ya pensheni ya hifadhi ya jamii ni kulinda na kuhakikisha ya kuwa pensheni za wanachama ziko katika hali ya usalama na zinapatikana kwa wakati uliopangwa na kuhitajika na mwanachama, na kutoa habari kamili zilizokamilika kwa wanachama wa mifuko ya pensheni na wategemezi wao. 


Uwajibikaji ni sehemu muhimu sana ya utawala bora, bila ya kuwa na mfumo mzuri wa uwajibikaji utawala bora hauwezi kusimamiwa au kongezeka kwa ufanisi wake. Kwa kweli tunaweza kusema kwamba utawala bora unabeba majukumu, uwazi na uwajibikaji mkubwa wa kuendesha kampuni.

Mahitaji ya uwazi na uwajibikaji kwa upande wa mifuko ya pensheni ya hifadhi ya jamii ni kitu kinachojionesha chenyewe. Kama mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii hauna imani na kukosa kusaidiwa na waanzilishi au wachangiaji wa mfuko,  kufanikiwa kwake utakuwa ni kidogo sana hata kama unaendelea kuishi. Ijulikane ya kuwa, uelewo wa umma na kuwa na moyo wa kupenda huenda ikawa ni kitu bora na muhimu sana kwa mfuko wa hifadhi ya jamii. 

Kama kuna uwazi na uwajibikaji mfumo wenyewe utategeneza mahitaji yote ya utawala bora. Utafiti umefanywa kuchambua juu ya uhusiano kati ya mambo mbalimbali ya utawala wa mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii kuhusiana na matokeo ya ufanisi mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii

Ingawa kumeonesha kuna baadhi ya tofauti mbalimbali katika matokeo ya utafiti unaosema ya kuwa utawala bora unasababisha matokeo makubwa kwa upande wa utendaji wa mfuko wa pensheni ya hifadhi ya jamii. Na kwa upande wa matokeo mabaya ya utendaji wa mifuko ya pensheni ya hifadhi ya jamii unasababishwa na viashirio au viindiketa vya kuwa na utawala mbovu ndani ya mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii

Uwazi kwa umma na kutoa taarifa yaani ripoti kwa washika dau wote unatakiwa kuwa ndiyo moyo wa mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii. Mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii unaundwa kwa kutumia fedha zinazotokana na michango ya wanachama zikichangiwa moja kwa moja na mwanachama na mara nyingine zingine kutoka kwa mwajiri wake zikiwa na malengo ya kuja kumwandalia mafao ya kustaafu kwa siku zijazo. Umma au mwananchi ambaye huenda ni mwanachama au mtegemezi anapenda kujua ni mambo gani yanayotokea juu ya utendaji wa fedha au michango yake anayochangia kila mwezi na kunaweza kiungwana kutokea kutegemea kupata nini kwa siku zijazo. mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii unaweza kuwa na aina nyingi ya wadau na uwazi pamoja na uwajibikaji wa ngazi ya juu  vyote  hivi vinaweza kutumika.

Wajibu wa mifuko ya pensheni ya hifadhi ya jamii ni kuhakikisha ya kuwa inawashirikisha wadau wake wote wakuu hasa waajiri, serikali na bila kusahau wanachama na familia zao ambapo makundi hayo matatu yanaunda kitu kinachoitwa utatu. Wananchi lazima watambue kuwa wawekezaji wa mifuko hii ni waajiri na wafanyakazi pale wanapojiandikisha na kuwa wanachama wachangiaji kwa kukatwa asilimia fulani kutoka katika mishahara yao na mwajiri na yeye kuchangia kiasi hicho hicho au zaidi kwa ajili ya mfanyakazi wake kwa makubaliano ya kupata huduma mbalimbali za muda mfupi na za muda mrefu kutoka katika kwa hiyo mifuko.
Na ndiyo maana mkurugenzi mkuu wa mfuko wa kustaafu wa GEPF anatoa taarifa ya utendaji ya unaoishia June 2013

Kwa mwaka 2013 ulikuwa mwaka muhimu sana katika historia ya Mfuko kwani waliweza kuandika upya sheria ya Mfuko ambayo ilibadilisha muundo wa Mfuko kutoka Mfuko wa Akiba na kuwa Mfuko wa Pensheni.

Mabadiliko ya muundo kutoka akiba kuwa pensheni umewawezesha wanachama kupata mafao ya muda mrefu na muda mfupi. Matokeo ya mabadiliko haya ni kuongezeka kwa mafao ikiwemo pensheni ya uzee, pensheni ya warithi, pensheni ya kuumia kazini, fao la kifo, fao la elimu na msaada wa mazishi. Mfuko pia umeanza kutoa mikopo ya nyumba kwa wanachama wake kupitia mafao yao kama dhamana.  Mfuko unaendelea kuwa na ukuaji mzuri wa wanachama na thamani ya mali zake.

“Tumeongeza ubora wa huduma kwa wateja kulingana na malengo tuliojiwekea kwa mwaka. Kwa miaka mitano mfululizo tumeweza kufikia malengo yetu.  Mafanikio haya ni matokeo ya kazi nzuri iliyofanywa na wajumbe wa Bodi, Menejimenti, wafanyakazi na muhimu zaidi wadau wetu mbalimbali ambao wamekuwa wakituunga mkono wakati wote” mkurugenzi mkuu Daudi Msangi anasema.

Kulikuwa na ongezeko kubwa la uandikishaji wa wanachama na ukusanyaji wa michango. Anasema kwa mwaka 2012/13 wanachama waliongezeka kwa asilimia 12.10 kutoka wanachama 52,670 mpaka wanachama 59,042. Ongezeko hili lilikuwa ni matokeo ya Mfuko kuendelea kufahamika kutokana na elimu inayotolewa na
ubora wa huduma zetu kwa wanachama.

Eneo lingine ni ukusanyaji wa michango ambao kama ilivyokuwa kwa ongezeko la wanachama, ukusanyaji uliongezeka kwa asilimia 22.11 kutoka shillingi millioni 30,149.13 mwezi June 2012 na kufikia shillingi millioni 36,816.18 mwezi Juni 2013. Ongezeko hili lilitokana na wanachama wapya waliojiunga na Mfuko na ongezeko la viwango vya mishahara ya  wafanyakazi.


Skimu ya Lazima
Katika mwaka huu idadi ya wanachama waliojiunga na Mfuko ilishuka, hata hivyo makusanyo yaliongezeka kwa asilimia 4.85 kutoka asilimia 17.26 na kufikia asilimia 22.11. Ongezeko hili ni matokeo ya kuongezeka kwa mishahara ya wanachama na wanachama wapya waliojiunga na Mfuko na waajiri kulipa michango mapema.
Idadi ya wanachama wanaojiunga na Mfuko imekuwa ikiongezeka kila mwaka kutoka mwaka 2008/09 mpaka mwaka 2011/12 kabla ya kushuka mwaka 2012/13. Mwaka huu ulikuwa mwanzo wa ushindani baina ya Mifuko na GEPF ilipata pigo kwa sababu ilikuwa Mfuko pekee wa Akiba na hivyo kuwa na mafao machache. Hali hii inatarajiwa itabadilika baada ya Mfuko kubadili mfumo na kuwa Mfuko wa Pensheni ambapo mafao ya muda mrefu kama pensheni yataanza kutolewa

Skimu ya Hiari
Mfuko uliendelea na utekelezaji wa Mpango wa Hiari wa Kujiwekea Akiba ya Uzeeni ambao uliingia mwaka wa tatu katika kipindi cha 2012/13. Ili kupanua huduma na kuwafikia watanzania wengi zaidi, Mfuko uliajiri wafanyakazi 18 na kufungua ofisi 3. Aidha Mfuko ulianzisha dawati mahsusi kuhudumia wanachama wa hiari na ulipaji wa mafao kwa wanachama wa aina hii na na kuendelea kutoa elimu kupitia warsha, semina na namna nyingine tofauti za kuitangaza Skimu hii.

Kupitia hatua hizi, wanachama wamekuwa wakiongezeka mwaka hadi mwaka kuanzia mwaka 2009/10 mpaka 2012/13. Wanachama waliojiunga na Mfuko kwa mwaka 2012/13 ni 5656 ambao kwa pamoja wanafanya idadi ya wanachama kufikia Juni 2013 kuwa 18,050. Kama ilivyokuwa kwa usajili wa wanachama, michango kutoka kwa wanachama pia imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka kutoka shilingi 1,839.00 milioni na kufikia shilling 3,050.80 milioni

Malipo ya Mafao
Malipo ya Mafao ni moja kati ya gharama zinazototakana na huduma kwa wanachama. Kupitia huduma hii kiasi cha
shilingi milioni 9,162.62 kililipwa kwa wanachama 1,955 ambao miongoni mwao wapo waliostaafu na wengine kujiunga na pensheni. Uhamishaji wa wanachama kujiunga na pensheni umekuwa ukifanyika kwa kuwa wakati huu Mfuko ulikuwa haulipi fao la pensheni.

Kuanzia mwaka 2008/09 hadi 2012/13 wastani wa asilimia 24.88 ya michango ya wanachama ililipwa kama mafao na hivyo kubakiwa na zaidi ya wastani wa asilimia 75 ya makusanyo kwa ajili ya uwekezaji

Mkurugenzi anasema Mfuko utaendelea kuhakikisha kuwa kiasi kinachokusanywa kama michango wakati wote kinazidi mafao, ili kuhakikisha fedha kwa ajili ya uwekezaji zinapatika. “Hili litawezekana kwa kuendelea kuongeza wigo wa wanachama na kuhakikisha kuna  mahusiano bora kati ya Mfuko na waajiri ili michango iwasilishwe kwa wakati” Msangi anabainisha

Uwekezaji na Mapato yake
Mkurugenzi mkuu anasema Mfuko uliendelea kuwekeza katika maeneo manne ambayo ni vitegauchumi vyenye faida inayojulikana kabla ya kuwekeza, hisa za makampuni, majengo (ardhi) na uwekezaji wa pamoja. Jumla ya shilingi milioni 179,552.60 ziliwekezwa katika kipindi cha mwaka huo na kuuletea Mfuko mapato ya shilingi milioni 18,253.99 ambayo ni sawa na asilimia 10.17 ya fedha zote zilizowekezwa.

Uwekezaji katika vitegauchumi
Vitega uchumi vya aina hii vinajumuisha amana za mabenki, hati fungani, amana za serikali na mikopo. Hadi kufikia. Mpaka Juni 2013 Mfuko ulikuwa umewekeza jumla ya shilingi milioni 154,365.64 ikilinganishwa na shilingi milioni 119,279.03 zilizowekezwa mwaka 2011/12.

Msangi anasema uwekezaji huu ni sawa na asilimia 85.97 ya fedha zote zilizowekezwa ambazo zilikuwa shilingi 179,552.60 milioni na kiasi kilichosalia sawa na asilimia 14.08 kiliwekezwa katika vitegauchumi vingine. Wakati shilingi 80,788.96 milioni za kitanzania ziliwekezwa katika amana za serikali, shilingi 57,316.00 milioni benki za biashara na kadhalika.

Eneo lililoongoza kwa uwekezaji mkubwa ni amana za serikali na amana za mabenki za muda mfupi ambapo kwa pamoja uwekezaji ulifikia asilimia 76.92 ya fedha zote zilizowekezwa. Mapato yanayotokanayo na uwekezaji huo yalikuwa shilingi milioni 17,510.37 sawa na ongezeko la asilimia 60.09 kutoka mapato ya mwaka 2012 ya shilingi milioni 10,938.13. Katika mapato yote ya uwekezaji, asilimia 46.08 ilitokana na amana za serikali na asilimia 43.42 ilitoka na amana za mabenki za muda mfupi.

Uwekezaji katika Majengo
Uwekezaji katika majengo ulifikia  kiasi cha shilingi milioni 13,864.62  hadi kufikia mwezi Juni 2013 sawa  na ongezeko la asilimia 30.75 kutoka shilingi milioni 10,603.88 zilizowekezwa hadi kufikia 2011/12.

Uwekezaji katika Majengo ulifikia asilimia 6.99 ya thamani ya Mfuko. Vile vile katika mwaka 2012/13 Mfuko ulifanikiwa kununua ekari 50 za ardhi katika eneo la Kijaka-Kimbiji Kigamboni jijini Dar-es-salaam na ekari 40.54 za ardhi eneo la Njedengwa Dodoma.

Mkurugenzi anasema ardhi hiyo itatumika kujenga nyumba za gharama nafuu kwa ajili ya kuwauzia wanachama na wananchi kwa ujumla.  Wanachama watauziwa nyumba hizi kwa pesa taslimu au mikopo kupitia mafao yao kama dhamana.

Uwekezaji katika Hisa
Anasema uwekezaji katika hisa unajumuisha hisa katika makampuni yaliyoidhinishwa katika soko la mitaji la Dar-es-salaam (DSE), ambapo hadi kufikia tarehe 30 Juni 2013, uwekezaji katika hisa ulikuwa umefikia shilingi milioni 10,308.45 kutoka shilingi milioni 6,846.46 zilizowekezwa mwaka 2012. Uwekezaji huu ulionesha ongezeko la asilimia 50.57 ambalo lilitokana na kupanda
kwa thamani za hisa

Thamani ya Mfuko
Msangi anasema thamani ya Mfuko imeongezeka kutoka shilingi milioni 154,410.99 mwezi Juni 2012 na kufikia shilingi milioni 198,435.07,  sawa na ukuaji wa asilimia 28.50. “Kukua huku kwa Mfuko kulichangiwa na kuongezeka kwa makusanyo ya michango na mapato kutoka katika vitegauchumi. Ukuaji wa mapato yalitokana na vitegauchumi na matokeo ya uwekezaji makini unaozingatia vitegauchumi vinavyolipa zaidi na salama”.

Gawio kwa Wanachama
Kifungu na. 8 cha Sheria ya GEPF ya mwaka 1942 (R.E.2002), kinaitaka Bodi ya Mfuko kutangaza gawio kwa wanachama kwa mwaka husika. Gawiwo hutolewa mara baada ya hesabu za Mfuko kukaguliwa na kutambua faida iliyopatikana. Kwa mwaka 2012/13 Bodi ya Mfuko ilitangaza gawio la asilimia 6.65. Moja ya malengo ya Mfuko ni kulinda thamani ya fedha za wanachama ambao ndiyo sababu muhimu ya kutoa gawio. Kiasi kilichotolewa ni kiasi kikubwa ikilinganishwa na kiasi kinacholipwa na taasisi nyingine za fedha.

No comments :

Post a Comment