Tuesday, September 30, 2014

Yajue mafanikio ya mfuko wa hifadhi ya jamii Zanzibar

Abdul-wakil H. Hafidh  Mkurugenzi mkuu wa ZSSF

Christian Gaya, Majira Septemba 30, 2014
Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa Zanzibar ulianzishwa chini ya kifungu cha sheria Namba 2 ya mwaka 1998 na baadaye ilirekebishwa chini ya kifungu cha Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar, Sheria Namba 9 ya mwaka 2002 na Sheria Namba 2 ya mwaka 2005. Kabla ya kifungu cha Sheria na uanzishwaji wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar, kulikuwa hakuna rasmi mpango wa kinga ya hifadhi ya jamii katika nchi ya Zanzibar. Wala hapakuwa na umuhimu kwa sekta isiyo rasmi kupatiwa kinga ya hifadhi ya jamii

Kabla ya kuanzishwa kwa mfuko wa hifadhi ya jamii Zanzibar, wafanyakazi wa umma katika serikali ya mapinduzi ya Zanzibar walipata pensheni chini ya Sheria Namba 2 ya 1990

Dira ya mfuko wa hifadhi ya jamii Zanzibar yaani ZSSF unalenga kuwa ni taasisi ya mfano ya utoaji wa hifadhi ya jamii katika ukanda wa Afrika Mashariki inayojumuisha nchi zilizo chini ya jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi na Rwanda. Katika kutekeleza dira hii, mkurugenzi mkuu wa ZSSF anasema dhima ya mfuko ni kwamba umedhamiria Kutoa mafao ya hifadhi ya Jamii endelevu kwa kutumia wafanyakazi mahiri na wenye ujuzi walionao.

Abdul-wakil H. Hafidh ambaye ndiye Mkurugenzi mkuu wa ZSSF anasema lengo kubwa la mfuko ni kuhakikisha ya kuwa linawarejeshea kipato wanachama wake kutokana na majanga kama vile uzee, ugonjwa, kupoteza sifa ya kufanya kazi na kifo.

“Hifadhi ya Jamii ni haki ya kila mtu. Haki hii imeanishwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 11(1). Haki hii pia imeiainishwa kwenye mkataba wa kimataifa wa haki za binadamu wa mwaka 1948 pamoja na mikataba ya shirika la kazi duniani (ILO) ibara ya 102 ya mwaka 1952” mkurugenzi mkuu anasisitiza.
Anaongeza kwa kusema ya kuwa idadi kubwa ya nguvukazi ya Wazanzibar inashughulika na sekta isiyo rasmi na wote wako katika hali hatarishi kwa vile hawana kinga yeyote ya hifadhi ya jamii. Kuziba pengo hilo Abdul Wakil-Haji Hafidhi ambaye ndiye mkurugenzi mkuu anasema Sheria ya Mfuko inaruhusu wanachama kutoka katika sekta rasmi na sekta isiyo rasmi kujiunga na Mfuko yaani. Mfuko unawaandikisha wanachama kutoka sekta isiyo rasmi kwa kupitia mfumo wa hiari unaojulikana kama ZVSS.

Hafidh anataja majukumu makuu ya Mfuko huu wa hifadhi ya jamii Zanzibar  ya kuwa ni, Kuandikisha wanachama; Kukusanya michango kutoka kwa wanachama hao; Kuwekeza michango hiyo kwa kufuata sera ya uwekezaji ya Mfuko ambayo inazingatia  Mwongozo wa Uwekezaji  wa Kimataifa na kulipa mafao kwa wanachama pale wanapotimiza masharti ya kustahili mafao hayo.

 “Kutokana na mikakati tuliyokuwa tumejiwekea  na kuitumia ipasavyo kwa mwaka 2012/2013 mfuko uliweza kuandikisha wanachama wapya wapatao 2,927  na hivyo kufikisha jumla ya wanachama wapatao 67,584 kwa mwaka 2012/2013 kutoka wanachama wapatao 64,657 kwa mwaka wa fedha wa 2011/2012 ambayo hii ni ongezeko wa asilimia 4.5” anabainisha mkrugenzi mkuu.

Anasema ili kuweka usawa wa njinsia zote mfuko wa hifadhi ya jamii Zanzibar ili kuhakikisha ya kuwa kunakuwepo na usawa wa kutoa kinga ya hifadhi ya jamii kwa wazanzibar wote kwa mwaka 2011/2013 mfuko ulikuwa na jumla ya wanawake wapatao 26,733 na wanaume 37,924 kama wanachama hai wachangiaji wa mfuko, wakati kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013  mfuko una jumla ya idadi ya wanawake wapatao 27,984 na jumla ya wanaume wapatao jumla ya 39,600 wote wakiwa wanachama hai wachangiaji wa mfuko.

Mkurugenzi mkuu anafafanua ya kuwa Mwanachama mnufaikaji yaani mwajiriwa ni yule mtu ambaye amesajiliwa na analipia michango katika Mfuko huu wa ZSSF.

“Mwaajiriwa anaweza kuwa ni mwanachama aliyesajiliwa na ZSSF kutoka Wizara na Idara za Serikali, Mashirika ya Umma, Sekta binafsi ambazo zinajumuisha: Makampuni, taasisi binafsi na asasi zisizo za Serikali pamoja na taasisi zisizo rasmi. Mwanachama aliyechangia katika Mfuko kwa kipindi kisichopungua miezi sitini atastahiki kupatiwa mafao kutoka katika Mfuko huu” Hafidhi  anasistiza.

Mpaka kufikia mwaka wa fedha 2012/2013 mapato kutokana na makusanyo ya michango yameongezeka kutoka shilingi za Kitanzania yaani bilioni 19.81 kwa fedha ya kitanzania kwa mwaka 2011/2012 mpaka kufikia fedha za kitanzania zipatazo bilioni 24.82 hii ikiwa ni ongezeko la asilimia 25. Na kwa upande mwingine mkurugenzi mkuu anasema mapato kutokana na vyanzo mbalimbali vya uwekezaji yameweza kuongezeka kutoka shilingi za kitanzania zipatazo bilioni 13.18 kwa mwaka wa fedha wa 2011/2012 mpaka kufikia shilingi za kitanzania bilioni 16.07 kwa mwaka 2012/2013 ikiwa kama ongezeko la asilimia 22 ukilinganisha na mwaka wa fedha uliopita.

Anasema ya kuwa katika mwaka wa fedha huo huo wa 2012/2013 malipo ya mafao ya wanachama yaliongezeka kwa asilimia 37 kutoka shilingi za kitanzania zipatazo bilioni 4.75 kwa mwaka wa fedha wa 2011/2013 mpaka kufikia fedha za kitanzania zipatazo bilioni 6.50 na ongezeko hili la malipo ya mafao yalitokana na ongezeko la idadi ya wastaafu na wakati shilingi zipatazo million 440.21 zililipwa kwa wanachama wa kigeni au raia wa kigeni.

Mafao ya uzeeni ni moja kati ya mafao ya muda mrefu yanayotolewa na Mfuko wa ZSSF na kulipwa mwanachama aliyetimiza umri wa kustaafu kazi. Mwanachama anaweza kustaafu kazi kwa hiari anapotimiza umri wa kuzaliwa wa miaka 55 hadi 59; au kukastaafu kwa lazima anapotimiza umri wa kuzaliwa wa miaka 60 kwa mujibu wa sheria ya ZSSF. 

Anasema Mafao ya uzeeni hujumuisha Kiinua mgongo ambayo ni mafao ya mkupuo anayolipwa mstaafu aliyetimiza umri wa kustaafu kwa hiari yaani miaka 55 hadi 59 au umri wa kustaafu kwa lazima yaani miaka 60 na pia awe amechangia Mfuko kwa kipindi kisichopungua miezi 60. Wakati Pensheni ya uzeeni 

Ni malipo ya kila mwisho wa mwezi ambayo hulipwa mwanachama kila mwisho wa mwezi tangu alipostaafu mpaka atakapofariki dunia.

Mkurugenzi mkuu anataja ya kuwa thamani ya Mfuko wa hifadhi ya jamii Zanzibar yaani ZSSF imekua kutoka shilingi bilioni 110.72 kwa fedha ya kitanzania kwa mwaka wa fedha 2011/2012 hadi kufikia shilingi bilioni 141.63 za kitanzania kufikia mwaka wa fedha wa 2012/2013, ikiwa ni ongezeko la asilimia 28 ikiwa ni kutokana na ongezeko la .michango ya wanachama, adhabu ya kuchelewesha michango kutoka kwa waajiri na mapato kutokana na vyanzo vya uwekezaji.

Katika mwaka wa fedha wa 2012/2013 mkurugenzi anasema mfuko uliendelea kuwaelemisha wanachama wake na wadau wengine, kuboresha uhusiano, kuwaaandikisha wanachama wapya na kutoa kadi kwa wanachama wapya na lengo kubwa likiwa ni kuwaandikisha wanachama zaidi ili kufikisha malengo pamoja na kupanua wigo zaidi kwa Wazanzibar walioko kwenye sekta rasmi na wale ambao wako kwenye sekta isiyo rasmi na wazanzibar waishio ughaibuni kujiunga na mfuko. 

Mkurugenzi mkuu anasema misingi ya maadili ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) ni kutoa huduma zake kwa wanachama na umma kwa ujumla chini ya misingi ya: Uadilifu; Uwajibikaji; Umahiri; Heshima; Ufuatiliaji; Kwenda na wakati; Uwazi; Kuwajali wanachama wake na Kufanya kazi kwa mashirikiano.

Anataja sifa za ziada za mafao yatolewayo na ZSSF anasema malipo ya mafao ya mfuko wa ZSSF ni makubwa kuliko Mfuko wa pensheni mwengine wowote wa Hifadhi ya Jamii Tanzania, anaendelea kutaja ya kuwa mafao yanayotolewa na mfuko wa ZSSF hulipwa katika kipindi kifupi sana tokea mwanachama kukamilisha taratibu husika.

Na kwamba malipo ya mafao ya mfuko wa ZSSF hufanyika baina ya ZSSF na mwanachama mhusika na hayapitii kwa mwajiri, taasisi nyengine au mtu mwengine yeyote. Mafao yanayotolewa na ZSSF hayabagui; hutolewa kwa wanachama wote walio raia na wasio raia wa Tanzania kama ilivyoainishwa katika tamko la Umoja wa Mataifa juu ya Hifadhi ya Jamii, na kuongeza ya kuwa mfumo wa hifadhi ya jamii ambayo ni ya lazima kisheria ambapo wafanyakazi pamoja na mwajiri wanatakiwa kuchangia pamoja na kupeleka michango kwenye chombo cha mfuko wa pensheni au mfuko wa akiba ya wafanyakazi. Na anamalizia kusema ya kuwa taarifa za malipo ya mafao huwa siri baina ya ZSSF na mwanachama au mlipwaji muhusika siyo vinginevyo.

Hafidh ambaye ndiye mkurugenzi mkuu wa ZSSF anasema wanayo nia ya kutanua zaidi wigo wa maeneo ya uwekezaji kwa kuongeza miradi ya ubia na miradi mingine inayolenga mapato na rasilimali za mfuko na ili kuhakikisha kuwa mfuko unavutia zaidi, na wataendelea kuboresha katika utoaji wa huduma na mafao yanayotolewa ili kuhakikisha ya kuwa muda wote ZSSF inakuwa chaguo la kwanza kwa wananchi wanaotafuta huduma ya hifadhi ya jamii nchini na kwa Afrika Mashariki nzima, wataendelea kujitangaza ili wananchi wengi zaidi kuelelewa mfuko, pamoja na mafanikio hayo ya mfuko bado unazo changamoto mbalimbali ambazo unakumbana nazo:  changamoto hizo ni pamoja uelewo mdogo juu ya mfumo wa hifadhi ya jamii, maeneo ya uwekezaji kuwa finyu, waajiri kutowasilisha michango kwa wakati muafaka, mfumuko wa bei na kushuka kwa thamani ya fedha, hata hivyo mfuko utaendelea kujipanga ili kuhakikisha kuwa changamoto hizo hazileti athari katika uendelevu wake. 

Mwisho mkurugenzi mkuu wa mfuko wa ZSSF anatoa wito kwa wananchi wote waishio nchini na nje ya nchi walio katika sekta rasmi na isiyo rasmi, pamoja na wageni waishio nchini kisheria kujiunga na  mfuko wa ZSSF ili wanufaike na fursa mbalimbali zilizopo pamoja na mafao bora yanazozingatia thamani ya fedha kwa wakati huo. Anasisitiza ya kuwa mtu yeyote mwenye umri usiopungua miaka 18 anaweza kuwa mwanachama wa ZSSF awe ni mkulima, mfugaji, mvuvi, msanii, mjasiriamali na hata wanafunzi. Anasema hata kwa wale watu ambao wanapata ajira rasmi katika sekta yeyote wanaruhusiwa kujiunga na mfuko wa hifadhi ya jamii ya ZSSF. Hivyo wewe mwajiriwa unafursa kuu ya kujiunga na mfuko wa ZSSF ili utakapostaafu uje uishi maisha yenye kinga ya majanga kamili na ndio maana kauli mbiu yetu inasema mfuko wa ZSSF ni ufunguo wa maisha ya baadaye.
 

No comments :

Post a Comment