Pages

Tuesday, June 30, 2020

SERIKALI YAFANIKIWA KUOKOA SHILINGI TIRIONI 11.4



Naibu Wakili Mkuu wa Serikali Mhe. Gabriel Malata akipokea kompyuta mpakato moja kati ya tano zilizotolewa na Shirika la Nyumba la Taifa kutoka kwa Meneja Huduma kwa mteja wa Shirika hilo Bw. Muungano Saguya .ofisini kakwe Jijini Dar es Salaam.
Naibu Wakili Mkuu wa Serikali Mhe. Gabriel Malata akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe waliohudhuria hafla ya makabidhiano ya kompyuta mpakato tano zilizotolewa na
Shirika nyumba la Taifa (NHC). kutoka kulia kwake ni Meneja Huduma kwa Wateja wa NHC Bw. Muungano Saguya, Bi. Yumriheri Ndullah ambaye ni Afisa Habari wa Nhc akifuatiwa na kaimu Mkuu wa kitengo cha manunuzi Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Bw. Emil Emmanuel ktoka kushoto ni Dr. Mussa Abdul Mkurugenzi wa mipango, Aziz Makaburi ambaye ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA pamoja na Bi. Devota Ngulugulu ambaye ni Mhasibu Mkuu wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali. ,Makabidhiano hayo yamefanyika ofisini kwa Naibu Wakili Mkuu wa Serikali iliyopo Jijini Dar es Salaam
………………………………………………………………………………………..
Na. Dennis Buyekwa- OSG 
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imefanikiwa kuokoa kiasi cha shilingi Tirioni 11.4 baada ya kushinda mashauri mbalimbali yaliyoendeshwa katika Mahakama mbalimbali ndani na nje ya nchi. 
Hayo yamezungumzwa mapema leo na Naibu Wakili Mkuu wa Serikali Mhe. Gabriel Malata alipokuwa akipokea msaada wa kompyuta mpakato tano zenye thamani ya shilingi milioni 7.5 zilizotolewa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Mhe. Malata ameeleza kuwa kiasi hicho cha fedha kimeokolewa katika mwaka wa fedha 2019/2020 kufuatia utendaji mzuri wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ambao umepelekea kushinda mashauri mengi yaliyofunguliwa dhidi ya Serikali.
Kiongozi huyo aliongeza kuwa fedha hizo zilizookolewa na Serikali zitasaidia katika kuboresha miradi mbalimbali ya maendeleo inayoendelea kama vile ujenzi wa reli ya kisasa (SGR), ununuzi wa ndege na meli kubwa  za abiria na mizigo katika kuhakikisha tunafikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Amesema kuwa kompyuta hizo zimekuja muda muafaka kwani zitawawezesha watumishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu Mkuu wa Serikali kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kwa haraka zaidi hatua itakayosaidia kuongeza ufanisi zaidi katika majukumu yao. 
Aidha, Naibu Wakili Mkuu ameongeza kuwa kompyuta hizo zitakuwa msaada mkubwa kwa Ofisi yake kwa kuzingatia ukweli kuwa mwaka huu tunaenda kwenye zoezi la uchaguzi hivyo itawawezesha watumishi wake hususani mawakili katika kutekeleza majukumu ya usimamizi wa mashauri.
“Mwaka huu tuna jukumu la uchaguzi na uchaguzi huwa unapelekea kuibuka kwa mashauri mengi yanayofunguliwa kwa ajili ya kupinga matokeo ya uchaguzi”, alisema Mhe. Malata.
Naye Bw. Muungano Saguya ambaye ni Meneja Huduma kwa Jamii katika Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) alisema kuwa wameamua kutoa msaada huo ili kuwasaidia watumishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufasaha zaidi hatua itakayopelekea kuendelea kuokoa fedha nyingi ambazo zingeweza kupotea kutokana na upungufu wa vitendea kazi ofisini hapa.
Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ilianzishwa feburuari 12 mwaka 2018 kwa tangazo la serikali Na. 50 ikiwa na lengo la kuratibu, kusimamia na kuendesha mashauri yote ya madai pamoja na Katiba, Uchaguzi na haki za binadamu yanayofunguliwa dhidi ya Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

No comments:

Post a Comment