Pages

Tuesday, March 3, 2020

RC AOMBA NGUVU YA WANANCHI MAPAMBANO DHIDI YA VITENDO VYA UKATILI



Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri akizungumza na wananchi wa mkoa huo wakati alipokuwa akiupokea msafara wa kijinsia ulifika mkoani humo kwa lengo la kutoa elimu ya kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Baadhi ya Wananchi mkoani Tabora waliojitokeza katika kuupokea msfara wa kijinsia unaolenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya vitendo hivyo.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri akiwa na wasanii Shetta na G nako wakitumbuiza katika Mtaa wa Toronto Mkoani Tabora wakati Msafara wa kijinsia unaolenga kutoa elimu ya mapambano dhidi ya vitendo vya kikatili uliposimama mkoani hapo.
Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini WAMJW
**************************
Na Mwandishi Wetu Tabora
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri amewataka wananchi wa Mkoa huo kuunga
mkono juhudi za Serikali katika mapambano dhidi ya vitendo vya kikatili hasa kwa wanawake na watoto.
Mkuu wa mkoa huyo ameyasema hayo jana mkoani humo wakati akiupokea Msafara wa Kijinsia kutokomeza ukatili unaolenga kutoa elimu kwa jamii kuhusu madhara ya kufanya vitendo vya ukatili wa kijinsia kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yatakayofanyika Kitaifa Simiyu Machi 08, 2020.
Mwanri amesema kuwa Mkoa wa Tabora ni miongoni mwa mikoa inayoendekeza vitendo hivyo kwani kumekuwa na mimba na ndoa kwa  watoto wadogo wa kike na vilikuwa vinazidi kushamiri ila kwa kiasi kikubwa wamekabiliana navyo.
“Sisi hatuna utani na wale wanaofanya vitendo hivi nilishasema nitasukuma ndani wahusika wote watakaohusika na vitendo vya ukatili wa kijinsia” alisema
Ameongeza kuwa suala la wananchi kushiriki katika kutoa taarifa juu ya matendo ya ukatili sio suala la hiari bali ni lazima kwani vitendo hivyo vinatokea na kufanywa na wanafamilia kwa kiasi kikubwa.
“Wanaofanya vitendo hivi ni watu wa karibu na familia zetu wanawabaka na kuwalawiti watoto wetu tunanyamaza kisa ndugu haiwezekani tukaruhusu haya” alisema
Pia Mkuu wa mkoa huyo amewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawapeleka shule watoto wao hasa watoto wa kike ambao walisahaulika ili kuwawezesha kupata elimu itakayowasidia kuondokana na vitendo vya kikatili katika ukuaji wao na ustawi wa maisha kwa ujumla.
Msafara wa kijinsia kutokomeza ukatili wa kijinsia upo katika mzunguko ulioanzia mkoa wa Katavi, Rukwa, Songwe, Mbeya, Iringa na umefika mkoani Tabora kuelekea Shinyanga na utapokelewa mkoani Simiyu kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.

No comments:

Post a Comment