Pages

Friday, November 2, 2018

WAGONJWA 23 WAPATIWA HUDUMA YA TIBA YA RADIOLOJIA MUHIMBILI


????????????????????????????????????
Mkuu wa Idara ya Radiolojia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dkt. Flora Lwakatare akizungumza na waandishi wa habari juu ya wataalam kuzibua njia ya nyongo ya mgonjwa kupitia huduma ya kibingwa ya tiba radiolojia kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS), Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) na Chuo Kikuu cha Yale na Emory  nchini Marekani. Kutoka Kushoto ni daktari bingwa wa upasuaji wa Muhimbili, Dkt Godfrey Mchele na mtaalam wa tiba ya radiolojia, Profesa Frank Minja kutoka Chuo Kikuu cha Yale nchini Marekani.
002
Baadhi ya wataalam wa tiba hiyo pamoja na waandishi wa habari wakimsikiliza Dkt. Flora Lwakatare.
003
Wataalam wa radiolojia wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS) pamoja na wataalam kutoka Chuo Kikuu cha Yale na Emory  nchini Marekani wakishirikiana kuzibua njia ya nyongo ya mgonjwa kupitia huduma ya kibingwa ya tiba radiolojia.
004
Mtaalam wa tiba radiolojia, Profesa Frank Minja kutoka Chuo Kikuu cha Yale nchini Marekani akizungumza na waandishi wa habari kuhusu jinsi wataalam wa Muhimbili, MUHAS na MOI walivyofanya maandalizi ya kufanikisha huduma ya tiba radiolojia. Kushoto ni Dkt. Lwakatare na kulia ni mtaalam wa huduma za radiolojia kutoka Chuo Kikuu cha Emory nchini Marekani.
005
Baadhi ya wataalam wa huduma za tiba radiolojia  wakifuatilia mkutano huo leo.
????????????????????????????????????
Dkt Lwakatare akifafanua jambo kwenye mkutano huo leo. Kushoto ni Mkurugenzi wa Huduma za Tiba Shirikishi Muhimbili, Dkt. Praxeda Ogweo, Dkt. Mchele wa Muhimbili, Prof. Minja kutoka Chuo Kikuu cha Yale, Dkt. Prologo kutoka Chuo Kikuu cha Emory na Dkt. Mechiris Mango wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI).
……………………
Dar es salaam                                                      
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS), Taasisi ya Tiba  Mifupa (MOI), Chuo Kikuu cha Yale na Emory nchini Marekani wameendesha kambi maalum ya kutoa huduma za kibingwa kupitia tiba Radiolojia ambapo wagonjwa 23 wamenufaika na tiba hiyo.
Tiba hiyo inahusisha utaalam wa kutumia vifaa vya Radiolojia kama X-Ray, MRI, CT-Scan na
Ultra- Sound kutibu moja kwa moja ugonjwa au kuchukua sampuli kwa ajili ya uchunguzi.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Idara ya Radiolojia MNH, Dkt. Flora Lwakatare amesema huduma hiyo ya kibingwa ilianza kwa mara ya kwanza nchini Novemba mwaka jana ambapo kabla ya uanzishwaji wake wagonjwa waliokuwa wanahitaji huduma hizi walikuwa wakienda nje ya nchi.
Akielezea kuhusu huduma zilizitolewa katika kambi hiyo amesema ni utoaji wa sampuli kutoka kwenye vivimbe katika sehemu mbalimbali za mwili ambazo si rahisi kufikiwa bila upasuaji mkubwa, kuzibua mirija ya nyongo, kuweka mirija kwenye figo ambazo mirija ya mkojo imeziba na unyonyaji wa vivimbe vyenye maji au usaha.
‘‘Kambi hii imehusisha wakufunzi ambao ni madaktari bingwa, mafundi sanifu Radiolojia, wauguzi Radiolojia kutoka vyuo vikuu vya Yale na Emory. Pia, watalaam kutoka Hospitali ya Benjamini Mkapa  na CCBRT nao wananufaika na mafunzo hayo.’’
Akielezea faida ya tiba hiyo amesema inamuwezesha mgonjwa kuepuka upasuaji mkubwa ambao ni hatarishi, kuepuka ukaaji wa muda mrefu hospitalini na kupunguza gharama.
Tangu kunzishwa kwa tiba Radiolojia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili wagonjwa takribani 100 wamenufaika na huduma hiyo.
Naye Dkt. Mchele amesema kuwa ujio wa wataalam hao kutoka Chuo Kikuu cha Yale na Emory umekua msaada mkubwa kwa wataalam wa Muhimbili, MUHAS na MOI kwa kuwa wamejifunza mambo mengi ya kitaalam.
 “Tumejifunza mambo mengi ambayo yatatuwezesha kuendelea sisi wenyewe baada ya timu hii kurejea Marekani. Hii imetusaidia sana kwani  kuna baadhi ya wagonjwa wana usaa kwenye ini, hivyo wametuwezesha kugundua tatizo mapema na kuweza kufanya upasuaji kwa mgonjwa bila kuacha jeraha kubwa,” amesema Dkt. Mchele.
Amesema kuanza kwa huduma ya tiba radiolojia ni hatua nzuri na muhimu kwani mwaka 2022, Muhimbili inatarajia kuanza kupandikiza ini na kwamba tiba radiolojia ni moja ya maandalizi ya kuelekea  kupandikiza ini.

No comments:

Post a Comment