Pages

Friday, June 24, 2016

Madaktari bingwa na changamoto za afya vijijini


Madaktari wa Tanzania katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, wakishirikiana na wenzao wa India walifanikiwa kufanya upasuaji wa moyo wa aina yake Tanzania.Upasuaji huo ujulikanao kama ‘bypass surgery’ ulishirikisha kupandikizwa kwa mishipa ya damu kutoka sehemu nyingine ya mwili moyoni bila kutumia mashine ya kusimamisha moyo na mapafu.Kwa kawaida madaktari wanasema upasuaji wa moyo hufanyika baada ya moyo na mapafu kusimama.

Christian Gaya, Majira Ijumaa Juni, 24, 2016
Utafiti kutoka nchi kumi na tano za Kiafrika ikiwemo Tanzania unaonesha idadi kubwa ya watu wa kipato cha chini wanakimbilia kukopa na kuuza rasilimali zao ili kuweza kwenda pamoja na gharama za matibabu. Hali hii imepelekea familia nyingi kuingia kwenye janga la umasikini zaidi na afya zao kuwa mbaya zaidi huko vijijini. 

Pia utafiti uliofanywa kutoka katika nchi sita za Kiafrika unaonesha kuwa idadi ya asilimia zaidi ya nne (4%) ya wazee wanasumbuliwa na magonjwa sugu ya moyo na kisukari hasa pale wanapofikisha umri wa miaka zaidi ya sitini ukilinganisha na wale ambao wako chini ya umri wa miaka sitini.
Pamoja na hayo bado serikali kama ya Tanzania, inatumia kiwango kidogo sana cha kipato kwa kichwa cha mtu kwa matumizi ya afya ukiachilia mbali hifadhi ya jamii ukilinganisha na nchi zilizoendelea.
Gharama hasa ya matibabu mara nyingi anaachiwa mwananchi ambaye hana uwezo wa kubeba mzigo bila msaada wowote kutoka serikalini au jumuia yeyote.
Afya maana yake ni hali ya ukamilifu kimwili, kiakili, kijamii na kutokuwepo kwa maradhi. Wote tunajua ya kuwa afya bora ni nguzo na raslimali muhimu katika kuchangia maendeleo ya mtu binafsi, familia na nchi hususan katika kuleta maisha bora na kupunguza umaskini.
Kwa mantiki hii afya inalenga kuwa na ustawi endelevu kwa jamii kwa kuzingatia mchango wa mtu binafsi kulingana na nafasi, uwezo na fursa zilizopo katika kuleta maisha bora.
Mwaka 2014 jopo la Madaktari bingwa wa magonjwa ya macho, kisukari na shinikizo la damu, lililokuwa linazunguka nchi nzima lilibaini kuwa asilimia 79 kubwa ya watanzania waliopimwa magonjwa hayo ni wazee kati ya mamilioni ya watanzania waliofikiwa na huduma hizo, ambao wamepata matibabu pamoja na kupewa elimu ya kukabiliana na magonjwa hayo.
Magonjwa ya mara kwa mara na ya muda mrefu, ni hali ya kawaida kwa wazee walio wengi wakiwemo akina mama na watoto. Hali hii inahitaji uangalizi na matunzo maalum ya kitaalam. Pamoja na ukweli huo, huduma za afya hazipatikani kwa urahisi kwa wazee na watoto walio wengi na mara nyingi ni ghali.

Utaratibu wa kutoa huduma bure kwa wazee bado una mapungufu. Wazee walio wengi hasa wa vijijini wanaachwa nje ya utaratibu wa kupata huduma kutokana na kushindwa kuthibitisha kwamba wana umri wa miaka 60 na hawana uwezo wa kuchangia gharama hizo.

Mfuko wa bima ya afya umeanzisha mradi wa kuwasogezea huduma mbalimbali wateja wake zikiwemo huduma za madaktari bingwa katika maeneo ya pembezoni.

Uchache wa madaktari bingwa hapa nchini umekuwa ni changamoto kubwa sana umekuwa ukisababisha matatizo makubwa kwa wazee, vijana na watoto kwa kupoteza maisha kwa kukosa matibabu sahihi au kushindwa kuzifikia huduma ziliko kutokana na umbali wa kijiografia

Na ndiyo maana mfuko wa bima ya afya mwaka 2013 walianzisha mpango wa huduma za madaktari bingwa maalumu wa kuwapeleka wataalamu katika mikoa ambayo miundo mbinu yake ni mibovu ili wazee, vijana na watoto wa maeneo hayo nao waweze kunufaika na huduma za NHIF zikiwemo za upasuaji na aina za magonjwa makubwa.

Taarifa zinaonesha ya kuwa kwa kipindi kuanzia Januari mpaka Machi 2015 mfuko ulifanikiwa kupeleka madaktari bingwa katika mkoa wa Tabora ambapo jumla ya wagonjwa 634 wakiwemo wazee, vijana na watoto walionwa na wataalamu hao ambapo kati ya hao wagonjwa 27 walifanyiwa upasuaji, huduma ambazo zisingeweza kufanyika mkoani hapo bila huduma hii ya madaktari bingwa wa vijijini.

Pia utafiti unaonesha ya kuwa tangu mpango huu uanze wagonjwa 6,535 wamenufaika na huduma za wataalamu hao huku wagojwa 238 wakifanyiwa upasuaji, huduma ambazo wangetakiwa kuzifuata Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Bugando Mwanza, KCMC Moshi, Mbeya au maeneo mengine ambapo wangetumia muda mwingi na gharama kubwa katika kuzipata huduma kama hizi.
Mpaka sasa kuna uhaba mkubwa wa madaktari bingwa hasa wa wanawake na watoto katika maeneo ya nje ya mijini, hali inayowafanya wanaoishi kwenye vijiji mbalimbali nchini kuikosa huduma ambayo kimsingi ni haki yao.
Madaktari bingwa wasio na vituo maalumu, inatakiwa wapelekwe kila mkoa nchini ikiwa kama utekelezaji wa moja ya mikakati ya Mfuko huu ya kuboresha huduma za afya kwa wanachama wake, ili kusaidia wanachama kupata huduma za madaktari bingwa kutoka maeneo yao, hasa wa vijijini, ili kupunguza gharama na muda wa kusafirisha wagonjwa nje ya mkoa au nchi.

Kuimarishwa kwa utoaji huduma za madaktari bingwa kutachangia kuhamasisha wanachama wenye sifa za kujiunga na Mfuko  kuongezeka, na kufanya Watanzania wengi kunufaika na huduma za Mfuko huo.

Jambo la muhimu ni kuhakikisha ya kuwa mfuko unawahamasisha wananchi wa vijijini ili wajiunge na mifuko ya afya ya jamii, kwani kwa sababu kwa kufanya hivyo utakuwa  na mchango mkubwa katika kusaidia huduma za matibabu vijijini kwa njia ya huduma za madaktari bingwa na huduma nyinginezo.
Watanzania wanategemea mpango kuwa endelevu zaidi kwa sababu umeonesha huduma kama hizi kusaidia kuokoa maisha ya watanzania wengi ambao hawana uwezo wa kifedha na gharama za kuzifuata zinakopatikana. Hivyo ni juu ya wananchi kuhakikisha ya kuwa fursa kama hii inatumiwa vizuri na siyo vinginevyo.




No comments:

Post a Comment