Sehemu ya washiriki wa Mkutano wa kwanza wa Afrika wa kudhibiti Sumukuvu (Alfasafe) kwenye vyakula wakifuatilia hotuba ya Waziri
wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) wakati akisisitiza mkakati wa
serikali katika kukabiliana na Sumukuvu nchini, uliofanyika katika
Hoteli ya Mount Meru Jijini Arusha tarehe 4 Novemba 2019.
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) akifuatilia mawasilisho mbalimbali ya washiriki wa Mkutano wa kwanza wa Afrika wa kudhibiti Sumukuvu (Alfasafe) kwenye vyakula uliofanyika katika Hoteli ya Mount Meru Jijini Arusha tarehe 4 Novemba 2019.
Waziri wa Kilimo Mhe Japhet
Hasunga (Mb) akisisitiza mkakati wa serikali katika kukabiliana na
Sumukuvu nchini wakati akifungua Mkutano wa kwanza wa Afrika wa
kudhibiti Sumkuvu (Alfasafe) kwenye vyakula uliofanyika katika Hoteli ya
Mount Meru Jijini Arusha tarehe 4 Novemba 2019. (Picha Zote Na Mathias
Canal, Wizara ya Kilimo)
Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Arusha
Hivi karibuni,
Serikali ya Tanzania ilipata fedha za kutekeleza mradi wa kuzuia kuenea
kwa
sumukuvu hapa nchini (TANIPAC). Mradi huo unalenga kupunguza kutokea
kwa madhara ya sumukuvu katika mfumo wa chakula kupitia udhibiti
husishi kwenye mnyororo wa thamani wa mazao ya mahindi na karanga, hivyo
kuboresha uhakika na usalama wa chakula na hatimae kuimarisha afya na
lishe ya jamii yetu na kuimarisha biashara kati ya Tanzania na nchi
zinazotuzunguka.
Mradi huo
unatekelezwa kwa kuzingatia mkakati Madhubuti kwa kushughulikia masuala
yote yanayohusu sumukuvu hapa nchini. Mkakati huo unazingatia udhibiti
wa sumukuvu katika hatua za uzalishaji, uvunaji, udhibiti wa kibilojia,
teknolojia baada ya kuvuna na njia za ukaushaji, uhifadhi, kujenga uwezo
wa kitaasisi, uratibu na kutoa elimu ya kuhamasisha wadau muhimu.
Ushiriki wa sekta binafsi ni muhimu katika uhaulishaji wa teknolojia
pamoja na kuhakikisha mradi unakuwa endelevu.
Waziri wa Kilimo
Mhe Japhet Hasunga (Mb) ameyasema hayo leo tarehe 4 Novemba 2019 wakati
akifungua Mkutano wa kwanza wa Afrika wa kudhibiti Sumkuvu (Alfasafe)
kwenye vyakula uliofanyika katika Hoteli ya Mount Meru Jijini Arusha.
Mhe Hasunga
amesema kuwa Ushirikiano wa kiutafiti, kati ya sekta binafsi na watunga
sera, ni muhimu katika kufanikisha mageuzi ya kilimo.
Waziri Hasunga
amesema kuwa Tangu kuibuka kwa tatizo la sumukuvu mwaka 2016, Tanzania
imechukua hatua mbalimbali za kupunguza kusambaa kwa sumukuvu hapa
nchini. Kwa kutambua changamoto za kukabili sumukuvu, ambapo
kunahitajika kutumia njia mbalimbali kuanzia kwenye hatua za uzalishaji,
uvunaji, uhifadhi, usindikaji na kuhusisha sekta za Umma na Binafsi
katika kupunguza upotevu wa chakula na kuongeza upatikanaji wa chakula
salama na lishe bora.
Amesema, Tanzania
imeanzisha Kamati Jumuishi ya Uendeshaji inayohusisha sekta na taaluma
kutoka taasisi mbalimbali chini ya Uenyekiti wa Wizara ya Kilimo ambayo
ina mamlaka ya kusimamia masuala yote yanayohusu sumukuvu.
Kadhalika,
amewahakikishia washiriki hao kuwa kinga ya sumukuvu – Alfasafe TZ01;
imeshasajiliwa kwa matumizi hapa nchini Tanzania. “Aidha, nimefarijika
kuwa kazi hii inafanywa na Kampuni Binafsi ambayo imewekeza katika
uzalishaji, na usambazaji wa bidhaa hii ambayo itaokoa Maisha ya watu
hapa nchini” Alisisitiza
“Napenda
kuwahakikishia utayari wa Wizara yangu katika kuyatumia maazimio
mtakayokubaliana katika mkutano huu. Aidha, Serikali ya Tanzania,
inatilia maanani na inaunga mkono hatua zinazochukuliwa katika kuhimiza
biashara ya chakula salama, usalama wa chakula na lishe” Alisema Mhe
Hasunga
Tanzania kwa sasa
inatekeleza Awamu ya Pili Programu ya Uendelezaji wa Sekta ya Kilimo
(ASDP II) yenye lengo la kuleta mageuzi ya sekta ya kilimo kuwa na
kilimo chenye tija na kibiashara, pamoja na kukuza uchumi wa wakulima
wadogo na kuboresha maisha, uhakika wa chakula na lishe bora.
Uhakika wa
chakula na lishe ni muhimili ambao ni muhimu wa ASDP II Katika kufikia
malengo hayo, uwekezaji katika utafiti wa kilimo ni muhimu katika kuleta
matokeo kwa wakulima na wadua wengine katika mnyororo wa thamani.
Waziri Hasunga
amesema kuwa kutokana na takwimu za Shirika la Chakula na Kilimo la
Umoja wa Mataifa (FAO) za mwaka 2017, Tanzania inaongoza katika
uzalishaji wa mahindi na karanga katika ukanda wa nchi za Afrika
Mashariki, kwa kuzalisha tani milioni 6 na tani milioni moja mtawalia.
Amesema, Pamoja
na mafanikio hayo, Serikali inatambua kuwa, ingawa mazao hayo ni muhimu
kwa chakula cha kila siku, lakini yanakabiliwa na ukubwa wa tatizo la
sumukuvu ambalo linahatarisha usalama wa chakula na kuwa kikwazo cha
biashara ya mazao hayo kwa nchi jirani na Tanzania.
Mkutano huu ambao
umewaweka pamoja watafiti, wafanyabiashara, watunga sera na wadau wa
maendeleo, ambao unalenga kupanga mikakati ya kuongeza kasi ya matumizi
ya kinga ya sumukuvu (Alfasafe), na kukabili sumukuvu barani Afrika,
unadhihirisha mabadiliko chanya ya kimtazamo tunayoyahitaji.
No comments:
Post a Comment