Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akizungumza na watendaji wa Mkoa wa Mara alipofanya ziara ya kikazi katika
mkoa huo kujionea utekelezaji katika sekta ya Afya na Maendeleo ya Jamii.
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Adam Malima akimuelezea
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine
Ndugulile kuwa anaendelea kuwachukulia hatua wale wote wanaofanya vitendo hivyo
kulingana na Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009 na Katiba ya nchi.
Baadhi ya watendaji wakisikiliza maelekezo
ya Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt.
Faustine Ndugulile alipofanya ziara ya kikazi katika mkoa huo kujionea utekelezaji
katika sekta ya Afya na Maendeleo ya Jamii.(PICHA NA WAMJW)
Na Mwandishi Wetu Musoma Mara
Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya
Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imewaagiza viongozi wa Mkoa wa Mara na Wilaya ya
Musoma kuchunguza tuhuma zinazohusisha kumbi za starehe wilayani Musoma
Mkoani Mara kwa kuruhusu watoto walio chini ya miaka 18 kuingia na kutumia
pombe ndani ya kumbi hizo.
Agizo hilo limetolewa wilayani Musoma na Naibu
Waziri wa Afya, MAendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile
alipotembelea Mkoa wa Mara kwa ziara ya kikazi.
Dkt. Ndugulile amesema kuwa akiwa katika ziara
yake amepokea Malalamiko kutoka kwa wananchi wakidai moja ya kumbi mbili za
starehe kuwaruhusu watoto walio chini ya umri wa miaka
18 na kutumia pombe wakiwa ndani ya kumbi hizo.
“Niwatake uongozi wa mkoa kufuatilia suala hili
kwa undani na kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote watakaobainika
kuhusika katika suala hilo’’ alisisitiza Mhe. Dkt. Ndugulile.
Amesema kuwa kwa mujibu wa wa kifungu cha 17 cha Sheria
ya Mtoto ya mwaka 2009 kinasema mtu ambaye ni mmiliki au anayeendesha au ni
msimamizi wa ukumbi wa muziki, Bar, au klabu ya usiku hatamruhusu mtoto kuingia
katika maeneno yao.
Kifungu kinaeleza kuwa mtu atakayekiuka kifungu
hiki atakuwa ametenda kosa na atakapotiwa hatiani atalipa faini ya kiasi
kisichopungua Sh Millioni moja na kisichozidi Sh Millioni tano au kifungo
kisichozidi miezi 12 au vyote kwa pamoja.
Ameongeza kuwa Serikali haitavumilia kuona watoto
wakishiriki katika shughuli za usiku ambazo zinatahatarisha ustawi wao nchini.
Aidha Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Adam Malima
amemuelezea Naibu Waziri kuwa anaendelea kuwachukulia hatua wale wote
wanaofanya vitendo hivyo kulingana na Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009 na Katiba
ya nchi.
Mhe. Malima ameongeza kuwa katika mkoa wake
hawataruhusu kutokea kwa matukio hayo na kwatahadharisha wamiliki wote wa kumbi
za starehe kuzingatia Sheria inayomlinda mtoto.
Mhe. Malima ameeleza kuwa Serikali ya mkoa
itaendelea kupambana pia na vitendo vya ukatili wa Kijinsia, Ndoa na Mimba za
Utotoni ambazo zinashamiri katika mkoa huo.
No comments:
Post a Comment