Christian Gaya, Majira
Ijumaa Agosti 5, 2016
Moja kati ya haki ya msingi
za kila binadamu ni kufurahia viwango vya juu vya afya viwezekanavyo. Serikali
zina majukumu ya kitaifa na kimataifa kutoa huduma bora za afya zinazofikika
kwa gharama nafuu na zinazopatikana kwa watu wote bila ubaguzi.
Hata hivyo, uhalisi huu
katika nchi zinazoendelea kama vile katika Afrika Mashariki ni matakwa ambayo
bado hayajatimika. Kanuni kuu ni kwamba
haki ya afya inategemea upatikanaji wa rasilimali za serikali.
Ingawa serikali katika kanda
hii zimeweza kuzongwa na ukosefu wa rasilimali na kushindwa kutoa huduma
jumuishi za afya kwa watu wote, huduma
za afya kwa maskini na wale walioathirika si hiari bali wajibu.
Aidha, serikali zina jukumu
la kuendelea kupanua utoaji wa huduma ya afya kila mwaka na ni mzigo uko begani
mwa serikali kuonesha kwamba inafanya hivyo na kwa upeo wa rasilimali zilizopo.
Aidha lazima uwepo
uwajibikaji na uwazi zaidi kutoka kwa serikali katika huduma ya afya.
Baadhi ya sauti za vyama vya
kiraia vinavyoongoza katika ukanda wa
Afrika Mashariki katika kuanzisha shughuli bunifu na za ujasiri za haki za afya
ili kukuza, miongoni mwa mambo mengine, upatikanaji wa dawa muhimu kwa watu
wote, uwajibikaji katika utoaji wa huduma za afya, na kuboresha huduma za
mwisho wa maisha kwa wagonjwa wenye magonjwa ya chungu ya muda mfupi.
Ni kwa bahati mbaya ya kuwa
serikali haiwezi kufanya kila kitu kwa ajili ya raia wake. Hivyo na ndio maana
kuna taasisi zisizo za kiserikali, za watu binafsi, za kidini na za hifadhi ya
jamii ambazo zina wajibu wa kushughulikia mambo kama haya kwa niaba ya serikali
kama vile mashirika ya akiba ya wafanyakazi wa makampuni binafsi ambayo
yanaweza kuanzishwa na kuendeshwa na waajiri wenyewe.
Zingine ni taasisi za bima
za serikali kama vile mfuko wa Taifa wa bima ya afya na taasisi za bima zingine
za watu binafsi zilizoko nchini, pamoja na mashirika ya umma yanayotoa pensheni
za hifadhi ya jamii na bima ya afya zinazoendeshwa kwa utaratibu wa kanuni za
kibima.
Kwa vile haki ya afya ni haki ya kila mtu ndiyo maana mfuko wa pensheni PSPF wana
mpango wa uanachama wa hiari kama mkakati wa makusudi juu ya kupanua wigo wa
hifadhi ya jamii ili kuhakikisha ya kuwa hata wale waliojiajiri kujiunga
na PSPF ili kunufaika na huduma ya bima
ya afya kwa gharama nafuu ya shilingi za kitanzania zipatazo 76,800 tu kwa
mwaka, na mwanachama anaruhusiwa kuingiza wategemezi watano kwa kumlipia kila
mmoja ada ya shilingi 76,800 kwa mwaka
PSPF kupitia mpango wake wa uchangiaji hiari imeanzisha
fao la matibabu kwa ajili ya wanachama wake walioko katika sekta isiyo rasmi.
Mpango huu ni wa ushirikiano kati ya PSPF na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya
(NHIF).
Kwa kupitia mpango huu wanachama wa PSPF walioko katika
sekta isiyo rasmi watanufaika na upatikanaji wa huduma za afya kote nchini kwa
njia rahisi na kwa uchangiaji nafuu zaidi
Ni Mfuko wa kwanza wa hifadhi ya jamii nchini kuingia na
mfuko wa NHIF ambayo yanamwezesha mtanzania aliye katika sekta isiyo rasmi kunufaika
na mpango wa bima ya matibabu kupitia NHIF kwa mwanachama aliyechangia kipindi
kisichopungua miezi mitatu.
Huduma ya matibabu katika mpango huu inapatikana nchi
nzima kwenye vituo vyote vilivyosajiriwa na NHIF kuanzia hospitali ya Taifa,
rufaa, hospitali za mkoa, vituo vya afya na zahanati zote za serikal, vituo vya
mashirika ya dini na hospitali binafsi pamoja na maduka ya dawa yaliyosajiriwa
na NHIF zaidi ya vituo 6,043 nchi nzima.
Na
ndiyo maana mfuko wa pensheni wa PSPF
unakaribisha wananchi wote wenye umri wa kufanya kazi, kuanzia miaka 18 na
zaidi waliojiajiri kwenye sekta isiyo rasmi kama vile Wakulima, wafanyabiashara,
ndogondogo, wasusi, vinyozi, mamalishe, mafundi cherehani n.k. kuwa wote wana
haki ya kujiunga na mpango wa uchangiaji wa hiari wa mfuko
wa pensheni wa PSPF.
Lengo ni kuwafikia
Watanzania wengi zaidi na kufungua milango kwa kundi kubwa la Watanzania ambao
kwa namna moja au nyingine hawakuwa na uhakika wa matibabu kwa kuwa hawakuwa
wanachama PSPF.
Mwanachama
aliyechangia kwa kipindi cha miezi 6 na zaidi anaweza kuomba kwa ridhaa yake
sehemu ya michango yake itumike kulipia ada ya bima ya afya ili mradi tu
kiwango cha mipango yake kitakachosalia katika akaunti yake kisiwe chini ya
kiwango kilichotolewa kwa ajili ya bima ya afya.
Uanachama
wa bima ya afya utadumu kwa kipindi cha mwaka mmoja tangu alipojiunga na
utauhishwa kila baada ya mwaka mmoja.
Mwanachama
mpya atakayehitaji kujiunga na huduma hii mara tu anapojiunga na mpango wa
uchangiaji wa hiari wa PSPF anatakiwa kuchanga kiasi ambacho ni mara mbili ya
ada ya mwaka ya bima ya afya, ambapo sehemu ya mchango huo wa awali itatumika
kama mchango wa uanachama wa mpango wa hiari na kiasi kinachobaki kitalipwa
NHIF kama ada ya mwaka kwa ajili ya bima ya afya.
Tofauti
na bima zingine za matibabu, fao la matibabu kwa mwanachama wa mpango wa
uchangaji wa hiari wa PSPF halina kiwango cha kikomo cha gharama za matibabu
kwa ajili ya huduma zilizoainishwa.
Mwanachama
wa mpango wa uchangiaji wa hiari wa
PSPF anayejiunga na fao la matibabu
atanufaika na mafao yote ya bima ya afya sawasawa na mwanachama mwingine yoyote
wa mfuko wa bima ya afya (NHIF).
Lengo kubwa ni kumjengea
uwezo mjasiliamali mdogo awekeze kwa ajili ya afya yake huku akiendelea na
shughuli nyingine za kujitafutia kipato
Kupitia mpango wa hiari mfuko
wa pensheni wa PSPF wajasiriamali wote wanaojiunga na mfumo huu watanufaika na
Bima ya Afya. Mfuko wa pensheni wa PSPF una uhakika kuwa wajasiliamali
wanaojiwekea akiba kwa ajili ya pensheni watapata fursa ya kupata huduma za
matibabu zinazotolewa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na kuwa na uhakika na
usalama wa afya zao wakati wanapojishughulisha na shughuli mbalimbali za
ujasiliamali
Mpango huu
wa hiari ni mahususi kwa ajili ya kuwapatia huduma ya hifadhi ya jamii wale wote
ambao awali kutokana na matakwa ya kisheria hawakuweza kujiunga na Mifuko ya
Hifadhi ya Jamii.
PSPF imeamua kuongeza fao hili
muhimu la matibabu kwa upande wa mpango wa uchangiaji hiyari ili kuchangia
katika huduma za afya kwa watanzania na pia kutekeleza lengo lake la kuwafikia watanzania
wengi zaidi na kufungua milango kwa kundi kubwa la watanzania ambao kwa namna
moja au nyingine hawakuwa na uhakika wa matibabu kwa kuwa hawakuwa wanachama wa
PSPF.
Itakuwa ni jambo jema
kuwahimiza wastaafu wengine popote walipo
kujiunga na PSPF ili wawe na uhakika wa kupata matibabu wakati wowote
hata kama hawana fedha mfukoni.
Christian Gaya ni
mwanzilishi wa Kituo cha HakiPensheni Tanzania, mshauri na mtaalamu wa masuala
ya pensheni. Kwa maelezo zaidi wasiliana kwa gayagmc@yahoo.com
www.hakipensheni.co,tz
au hakipensheni.blogspot.com Simu namba +255 655 13 13 41
No comments:
Post a Comment