Pages

Thursday, November 19, 2015

Mifuko ya pensheni na changamoto za vijana




Mkulima mdogo mdogo wa nyanya ambaye ni mwanachama wa mfuko wa pensheni wa hifadhi ya jamii ambao humwezesha mwanachama kupata mikopo ya riba nafuu sana kwa ajili ya kununulia pembejeo, kusomesha watoto wao,na shughuli nyingine za maendeleo. Kilimo ndio sekta mama ya uchumi wa Tanzania na mpaka sasa inaajiri zaidi ya asilimia 70 ya wananchi.

Christian Gaya Mwananchi, Alhamisi, Novemba 12, 2015
Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa wastani wa nguvukazi hasa vijana wasomi wanaotafuta ajira kwa mwaka ni takriban 800,000 hadi 1,000,000. Hata hivyo, ajira rasmi zinazopatikana nchini katika sekta ya umma na sekta binafsi ni kidogo, takriban ajira 80,000 hadi 100,000 kwa mwaka. 


Takwimu pia zinaonyesha kuwa kundi la vijana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 24 wanakadiriwa kufikia milioni 8.3, sawa na asilimia 19.8 ya watanzania.Vijana wasomi ndiyo wapo kwenye kundi hili. Vijana wengine watarajiwa ni wale walio kwenye umri chini ya miaka 15.
Taarifa za idadi ya watu nchini zinaonesha kuwa asilimia 44.4 ya Watanzania wote wana umri chini ya miaka 15. Hili ni kundi lingine kubwa mno la Vijana watarajiwa ambao inabidi kuwaandaa kama nguvukazi ya Taifa letu. Pamoja na mafunzo ya ujasiriamali yanayotolewa, vijana na wanachama inatakiwa wawezeshwe na kuwekewa mifuko ya uwezeshaji yenye utaratibu maalum ulio wazi na mwepesi wa kupatikana kwa mikopo.
Miongoni mwa changamoto kubwa ambayo Vijana wengi wajasiriamali wanaopenda kujiajiri wanakumbana nayo ni ukosefu wa mitaji na mikopo yenye masharti nafuu. Taasisi nyingi za fedha nchini na benki za biashara zinatoa mikopo kwa riba kubwa na masharti mengi, ambayo vijana na wanachama wa mifuko wengi hawawezi kuyamudu.

Mifuko inatakiwa kusaidia kuleta maendeleo kwa nchi kwa kuchangia kuanzisha miradi mbalimbali ambayo inaweza kuajiri vijana ambao kama asilimia 90 ya vijana wa kitanzania hawana kazi na kusaidia vijana wajasiriamali kuanzisha miradi yao ambayo baadaye husaidia tena kuajiri baadhi vijana wengine. Idadi ya watanzania mpaka sasa imefikia milion 45 na asilimia 63 ya nguvukazi ni vijana. 

Tatizo kubwa linalowasumbua vijana ni ukosefu wa ajira. Hivyo mifuko inatakiwa kuwa na malengo ya makusudi ya kuhakikisha kuwa inakuwa na miradi mbalimbali ambayo itasaidia vijana wa kitanzania kupata kazi kuajiriwa au kujiajiri wenyewe. Vijana wanatakiwa kuwa wajasiriamali wazuri wenye ujuzi mbalimbali, na kuwa wavumbuzi na wabunifu wa vitu mbalimbali vitakavyoweza kukuza uchumi wetu.

Lakini ieleweke wazi ya kuwa lengo la mifuko hii ya hifadhi ya jamii ni kwa ajili ya kumsaidia mfanyakazi kumudu mahitaji yake ya uzeeni pindi anapostaafu ili kumsaidia uzeeni kwani ilibainika kuwa wakati wa ujana, wafanyakazi wengi hushindwa kujiwekea akiba ya kutosha wao wenyewe.  Mifuko ni kama ilivyo sera ya bima yaani mtu hulipwa pale anapopatwa na janga, na mahususi kumsaidia mfanyakazi kununua vitu vya thamani kama vile viwanja au kujenga nyumba anapostaafu au anapoelekea kustaafu.

Kutokana na umuhimu huo mifuko inatakiwa kuwasaidia vijana na wanachama jinsi ya kuanzisha miradi mbalimbali wakati bado wapo kazini kwa kutoa mikopo ya gharama nafuu kabla na pale wanapostaafu na ndio maana mifuko inatakiwa kutoa kwanza malipo ya mkupuo wa pensheni ya miezi kadhaa ili kuanzisha miradi ya aina mbalimbali kwa kusaidiwa na wataalamu kutoka katika mifuko hiyo hiyo ya hifadhi ya jamii hasa kwa kutoa ushauri wa kitaalamu juu ya uanzishwaji na uendesheshaji wa miradi. Lengo iwe kutoa huduma zote muhimu pale wanachama na familia zao wanapopatwa na majanga ya aina mbalimbali ambayo kwa sasa yamekuwa yakitokea mara kwa mara yakiwemo majanga yanayosumbua wanachama kiuchumi na kijamii.

Mifuko hii inatakiwa kuhahakikisha kuwa vijana na wanachama wake wanaopatiwa mikopo ya gharama nafuu wanapata elimu ya ujasiriamali ya kutosha kwa kushirikiana na taasisi husika ili wajue malengo ya mikopo ya biashara na hata pia kuelemishwa juu wajibu wao kwenye mifuko, wajibu wa mwajiri, mafao yatolewayo na mifuko hii, jinsi ya kuwekeza na kwa nini michango yao inawekezwa na faida ya riba wanayopata kutokana uwekeza

Mifuko inatakiwa kuwa na mbinu za ubunifu wa hali ya juu hasa kwa kufanya utafiti kwa kwenda mbele zaidi  kwa kuwatumia mawakala mbalimbali ambao wanaweza kutumika kuwaandikisha wanachama kutoka katika sekta isiyo rasmi na walioko ughaibuni na hata katika utoaji wa mikopo ya riba nafuu kwa wanachama wao kupitia waajiri wao kama baadhi ya mifuko ilivyoanza kutekeleza mikakati, lengo kubwa likiwa kutaka kuwafikia wanachama wengi zaidi kuliko kupitishia kwenye SACCOS ambapo wengi wa wanachama sio wanachama wa SACCOS na hivyo kuwarahisishia kupata mikopo kwa muda mfupi zaidi kuliko ilivyo sasa kwa mifuko mingi inavyotegemea SACCOS kama chombo cha kuwafikishia mikopo wanachama wao ingawa kinaweza kuwa kivutia kizuri cha kupata wanachama wapya kujiunga na mifuko

Hatimaye kwa kufanya hivyo itasaidia hata kujenga mshikamano zaidi sehemu za kazi, na kuwasaidia waajiri kuongeza uzalishaji wenye tija zaidi na hivyo kusaidia msukumo wa kuwasilisha michango ya wafanyakazi wao kwa wakati muafaka, kuwapunguzia ukali wa maisha wanachama na hivyo kupunguza umasikini kama sio kuondoa kabisa, kinachotakiwa hapa ni mifuko kuweka utaratibu wa masharti na kanuni nzuri zinatakazowavutia hata waajiri kutoa vibali vya udhamini kwa wafanyakazi ambao ni wanachama wa mifuko hii kupata mikopo ya gharama nafuu.

No comments:

Post a Comment